LATEST HEADLINES👉

Your Ad Spot

Aug 21, 2022

NAIBU WAZIRI WA AFYA NCHINI MALAWI AFANYA ZIARA JKCI KUJIFUNZA UTOAJI HUDUMA ZA MATIBABU YA MOYO NCHINI

  Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Jakaya Kikwete (JKCI) Prof. Mohamed Janabi akielekeza huduma zinazotolewa na Taasisi hiyo wakati wa ugeni wa Naibu Waziri wa Afya kutoka nchini Malawi Mhe. Enock Phale kwa ajili ya kuona huduma za matibabu ya moyo zinazotolewa pamoja na kuangalia mifumo ya Tehama inayotumika katika uendeshaji wa Taasisi hiyo leo Jijini Dar es Salaam. (PICHA ZOTE NA KHAMISI MUSSA).
  Mkurugenzi wa Kurugenzi ya Upasuaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Angela Muhozya akielezea huduma zinazotolewa katika chumba cha upasuaji mkubwa wa moyo kwa Naibu Waziri wa Afya Mhe. Dkt. Godwin Mollel pamoja na Naibu Waziri wa Afya Nchini Malawi Mhe. Enock Phale wakati wa ziara yake katika Taasisi hiyo kwa ajili ya kuona huduma za matibabu ya moyo zinazotolewa pamoja na kuangalia mifumo ya Tehama inayotumika katika uendeshaji wa Taasisi hiyo leo Jijini Dar es Salaam.
  Naibu Waziri wa Afya Nchini Malawi Mhe. Enock Phale akimjulia hali mtoto aliyelazwa katika wodi ya watoto wenye magonjwa ya moyo Herieth Mapunda wakati wa ziara yake katika Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) kwa ajili ya kuona huduma za matibabu ya moyo zinazotolewa pamoja na kuangalia mifumo ya Tehama inayotumika katika uendeshaji wa Taasisi hiyo leo Jijini Dar es Salaam. 
  Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Prof. Mohamed Janabi akimuonesha Naibu Waziri wa Afya Nchini Malawi Mhe. Enock huduma mbalimbali za Taasisi hiyo zinavyofanyika wakati wa ziara yake katika Taasisi hiyo kwa ajili ya kuona huduma za matibabu ya moyo zinazotolewa pamoja na kuangalia mifumo ya Tehama inayotumika katika uendeshaji wa Taasisi hiyo leo Jijini Dar es Salaam. 
: Naibu Waziri wa Afya Mhe. Dkt. Godwin Mollel katika picha ya pamoja na Naibu Waziri wa Afya Nchini Malawi Mhe. Enock Phale wakati wa ziara yake katika Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) kwa ajili ya kuona huduma za matibabu ya moyo zinazotolewa pamoja na kuangalia mifumo ya Tehama inayotumika katika uendeshaji wa Taasisi hiyo leo Jijini Dar es Salaam.

Na: Genofeva Matemu – JKCI

18/08/2022 Naibu Waziri wa Afya wa nchini Malawi ametembelea Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) kwa ajili ya kuona huduma za matibabu ya moyo zinazotolewa pamoja na kujifunza mifumo ya Tehama inayotumika katika uendeshaji wa huduma za matibabu katika Taasisi hiyo.

Akizungumza na waandishi wa habari leo Jijini Dar es Salaam kwa niaba ya Waziri wa Afya Naibu Waziri wa Afya Mhe. Dkt. Godwin Mollel alisema kuwa ugeni wa naibu waziri wa afya kutoka nchini Malawi umelenga kupata uelewa wa huduma zinazotolewa na JKCI pamoja na kujifunza mifumo ya Tehama ambayo Tanzania inaitumia kwenye sekta ya afya ili nao waende kuboresha mifumo ya afya nchini mwao.

Mhe. Mollel alisema kuwa uwekezaji mkubwa uliofanywa katika taaluma ya afya na vifaa tiba imeleta tija kubwa kwani sasa nchi za Afrika na nchi ambazo zinaizunguka Tanzania zimeanza kujifunza kupitia Tanzania na kuona badala ya kuwapeleka wagonjwa wao India, Ulaya na Marekani waanze kuwaleta hapa nchini.

 “Upande wa upasuaji mdogo wa moyo kupitia tundu dogo kwenye paja wataalamu wetu wameweza kufanya aina tofauti tofauti za upasuaji ambapo hadi sasa asilimia 92 ya upasuaji mdogo wa moyo unafanywa na wataalamu na asilimia nane iliyobaki inafanywa na wataalam kutoka nje ya Tanzania ambapo tunawachukua wataalam hao kuja hapa kwetu kwasababu vifaa tunavyo tunachotaka kutoka kwao ni ujuzi ambao utatuwezesha kwenda hatua ya juu zaidi”,

“Upasuaji mkubwa wa kufungua kifua asilimia 85 za upasuaji huo inafanywa na wataalam wa afya wazawa huku asilimia 15 za upasuaji huo inafanywa na wataalam wa afya kutoka nje ya nchi ambao wamekuwa wakituachia ujuzi kwa wataalamu wetu”, alisema Dkt. Mollel

Mhe. Dkt. Mollel alisema kuwa hivi sasa Taasisi ya Moyo inapokea wagonjwa kutoka nchi 25 duniani ikiwemo Visiwa vya Comoro, Zambia, Kenya, Congo, Malawi na nyinginezo hii inatokana na Uongozi wa Mhe. Rais Samia ambaye tokea Mwanzo alisema kuwa anaifungua nchi kwa maana ya kufungua fursa ya ujuzi, utalii wa kimatibabu na uduma za kibobezi za afya zinazopatikana hapa Tanzania.

Mhe. Dkt Mollel alisema kuwa Mhe. Samia Suluhu Hassan Rais wa Jamhuri ya Muuungano wa Tanzania amewekeza kwenye eneo la afya ambapo Afrika hadi sasa zipo nchi chache ambazo zinafanya upasuaji wa moyo mbalimbali hivyo kuzivutia nchi ningine kama Malawi kuona ni vyema leo kuja kujifunza kwetu.

“Mhe. Naibu waziri wa Afya kutoka Nchini Malawi Mhe. Enock Phale amekuja hapa kwetu kwa ajili ya kuona huduma tunazizitoa na kujifunza mifumo ya Tehama tunayoitumia katika sekta ya afya hii inaonyesha adhma ya Mhe. Samia ya utalii wa kimatibabu inavyotekelezeka”,

Tukiwa wabunifu wakutosha kwa kuwatengenezea wataalamu wetu ujuzi na kuvisimamia vizuri vifaa vyetu tukapata wagonjwa wengi kutoka nje ya Tanzania mapato ya Taasisi zetu yataongezeka hivyo kuziwezesha Taasisi zetu kujiendesha zenyewe na kupunguza kuitegemea serikali”, alisema Dkt. Mollel

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Prof. Mohamed Janabi alisema kuwa ugeni wa Naibu Waziri wa Afya wa nchini Malawi umelenga kujifundisha JKCI inachokifanya na itawasaidiaje kama nchi na wao kuweza kufika Tanzania ilipo katika Sekta ya Afya.

“Malawi wanapita njia ambayo sisi tumepita huko nyuma ambapo wagonjwa wote wa moyo, figo, saratani, mifupa na magonjwa ya damu tulikua tunawapeleka India, Afrika ya Kusini, Ulaya na Marekani lakini baada ya uwekezaji huu mkubwa uliofanywa na Serikali JKCI imepunguza kupeleka wagonjwa wa moyo nje ya nchi kwa asilimia 95”,

“Katika hii miezi mitatu tumeshapata ugeni kutoka Afrika ya Mashariki, ugeni kutoka Zambia, na tukapata ugeni kutoka Mozambique, hii ni nchi ya nne sasa inakuja JKCI kwa ajili ya kuona nini tunafanya ili na wao wakafanye kama sisi”, alisema Prof. Janabi

Aidha Prof. Janabi alisema kuwa Serikali ina nia kubwa katika utalii tiba hivyo katika lile lengo la kufikisha watalii milioni 5 sekta ya afya chini ya usimamizi wa Wizara imekusudia afya ichangie katika kuleta watalii kupitia huduma bora na bobezi za matibabu yanayotolewa hapa nchini yakiwemo matibabu ya moyo.

“Tunaishukuru Serikali kwa ushirikiano waliotupatia kwa kuwekeza wataalamu na vifaa tiba vya kisasa katika Taasisi yetu, sisi kama wataalam kazi yetu ni moja tu ya kuwahudumia wananchi wa Tanzania na nchi za jirani za SADC ikiwemo kutangaza utalii kupitia afya”, alisema Prof. Janabi

Naye Naibu waziri wa afya Nchini Malawi Mhe. Enock Phale alisema kuwa amekuja Tanzania kwa ajili ya kujifunza Tanzania imewezaje kufanikiwa katika kutoa huduma za kibingwa za matibabu ya moyo na kuangalia namna ambavyo nchi yake itaweza kuwaleta wagonjwa wa moyo badala ya kuwapeleka nchi za India na Ulaya.

“Natamani na sisi Malawi tuwe kituo cha ubora katika kutoa huduma za matibabu ya moyo kwani sasa tunatumia fedha nyingi kuwapeleka wagonjwa wetu nchini India kwa ajili ya matibabu ya moyo wakati majirani zetu hapa mmefanikiwa kwa kiasi kikubwa katika kutoa huduma za matibabu ya moyo”,

“Naamini kwa kuwaleta wagonjwa hapa Tanzania kutapunguza gharama za matibabu, Malawi ni nchi wanachama wa SADC hivyo kupitia mwavuli huo tunaenda kufanikiwa kwa wagonjwa wetu kuja kutibiwa hapa JKCI”, alisema Mhe. Phale

                                                                             

No comments:

Post a Comment

MAONI (COMMENTS)👇

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages