LATEST HEADLINES👉

Your Ad Spot

Feb 24, 2020

TUNDURU WAANZA KUWATUMIA WAGANGA WA TIBA ASILI KUWAIBUA WAGONJWA WA KIFUA KIKUU


Mganga wa tiba asili na tiba mbadala, Huasi Mohamed aliyevaa shuka nyeupe ambaye ameepata mafunzo ya kuwaibua na kuwahisi wagonjwa wa kifua kikuu wanaofika katika kilinge akiwa katika picha ya pamoja na mratibu wa kifua kikuu,ukoma na tiba asili katika Hospitali ya wilaya Tunduru Dkt Mkasange Kihongole wa pili kushoto na baadhi ya wazazi wake,Mganga huyo amekuwa msaada mkubwa katika kuwaibua wagonjwa wa kifua kikuu wanaofika kwake kwa ajili ya kupata huduma ambapo wale wanaohisiwa wanapewa rufaa ya kwenda Hospitali kwa ajili ya uchunguzi na matibabu.

Na Mwandishi Wetu, Tunduru

BAADHI ya wananchi wa wilaya ya Tunduru mkoani Ruvuma,wameipongeza Serikali kupitia kitengo cha kifua kikuu na ukoma Hospitali ya wilaya ya Tunduru kuanza kuwatumia waganga wa Tiba asili na tiba mbadala waliosajiliwa kuibua wagonjwa wa kifua kikuu na kutoa rufaa ya kwenda  hospitali kupata matibabu.

Wananchi hao waliokutwa katika  kitongoji cha Mdingula kijiji cha Namasalau wakipata tiba katika moja ya kilinge cha mganga maarufu wa tiba asili na tiba mbadala  Hausi Mohamed wakipata huduma, wameishauri Serikali iendelea kuwaamini na kuwaunga mkono waganga hao  kwani wana  mchango mkubwa katika  kutokomeza ugonjwa huo na kuokoa maisha ya watu.

Rahim Hussen na Mohamed Abdala walisema, iwapo Serikali  itawatumia waganga wa Tiba asili  kwenye kampeni na mkakati dhidi ya ugonjwa wa kifua kikuu, mafanikio yake yatakuwa makubwa  kutokana na kuwepo kwa idadi kubwa ya watu kutoka maeneo mbalimbali wanaofika kwa waganga hao kwa ajili ya kupata huduma kutokana na shida zao.

Rahim alisema,  kwenye vilinge vya waganga wa tiba asili kuna makundi makubwa ya watu kutoka mikoa mbalimbali ya Tanzania Bara na visiwani na hata nchi jirani ya Msumbuji.

Alisema,ushiriki wao katika kuibua wahisiwa  wa kifua kikuu wanaofika katika vilinge vyao na kuwapa rufaa ya kwenda Hospitali kwa ajili ya vipimo na matibabu wataokoa maisha ya wananchi wengi wenye maradhi hayo wanaokimbilia kwa waganga wa tiba asili.

Mohamed Abdala alisema, jamii kubwa inaaamini sana tiba mbadala kama suluhisho la matatizo waliyonayo kwani  baadhi ya maradhi  hayana tiba za kitaalam,lakini wanapofika kwa waganga wanapona kabisa  na kuungana na familia zao  na kushiriki katika kazi za maendeleo.


“sisi kama wananchi tunashukuru sana katika kijiji chetu kupata mganga wa tiba asili ambaye amekuwa mkombozi mkubwa wa shida zetu,tulikuwa na shida ambazo  tulikwenda hospitali  lakini  hatukupona, na mara  baada ya kuja kwa mganga  afya  zetu zimeimarika,naiomba Serikali iendelea kuwatumia na kushirikiana na waganga kwani ni msaada mkubwa kwetu sisi wananchi”alisema.


Kwa upande wake Mratibu wa kifua kikuu na ukoma Hospitali ya wilaya Tunduru Dkt Mkasange Kihongole alisema, tayari  kuna waganga wa tiba asili zaidi ya arobaini  wamepata mafunzo ya namna  ya kuwaibua  wagonjwa wenye maambukizi ya kifua kikuu na kuwapa rufaa kwenda Hospitali kwa ajili ya uchunguzi.

Dkt Kihongole ambaye ni mratibu wa tiba asili na tiba mbadala alisema,kutokana na tatizo kubwa la kifua kikuu katika jamii yetu Serikali imeona umuhimu wa kuwatambua na kuwashirikisha waganga hao katika kampeni yake ya kutokomeza TB ifikapo mwaka 2035.

Alieleza kuwa, lengo la kuwashirikisha waganga hao ni baada ya kubaini asilimia sitini  kati ya mia moja ya Watanzania wanaamini na kukimbilia kwa waganga hao kupata matibabu kulingana na shida walizo nazo na asilimia arobaini tu ndiyo wanaofika Hospitali.

Alisema, moja kati ya mkakati wa Serikali katika kutokomeza TB ni kushirikiana na waganga ambao  utasaidia  kuwahisi wale wenye  vimelea vya ugonjwa wa kifua kikuu na kuwapa rufaa kwenda Hospitali kwa ajili ya matibabu zaidi badala ya kuwakumbatia jambo ambalo ni hatari kubwa kwa maisha ya waganga wenyewe na watu wengine.

Aidha Kihongole,amewataka waganga hao kuacha kufanya shughuli zao kwa kujificha bali wafanye katika mazingira rafiki, bora na safi  ili kufikiwa kwa urahisi na watu wengi zaidi.

Alieleza wananchi waliokutwa katika Kilinge hicho kuwa, tiba asili ni salama kwani ilianza kutumiwa tangu enzi za  Yesu Kristo  na kuwataka viongozi  kuanzia ngazi ya kijiji kuweka utaratibu mzuri utakao wezesha vijiji vyao kupata fedha kutokana na  uchimbaji mizizi na miti dawa inayotumika kwa ajili ya tiba, badala ya kuwaachia waganga na watu kutoka nje ya wilaya hiyo wakinufaika na rasilimali za mitidawa inayopatikana kwa wingi katika wilaya ya Tunduru.

Mmoja wa Waganga wa tiba asili    Hausi Mohamed(Babu Manjenje), ambaye ni  mingoni mwa waganga waliopata mafunzo ya kuwaibua wagonjwa wa kifua kikuu, ameishukuru Serikali kwa kuwatambua na kuona umuhimu wa kushirikisha  katika kampeni ya kutokomeza ugonjwa wa kifua kikuu.

Alisema, kuna watu wengi  wenye shida mbalimbali wanaofika katika Vilinge vyao kwa ajili ya kupata tiba, hivyo uamuzi wa Serikali kuwatumia waganga katika  mapambano dhidi ya ugonjwa huo utasaidia kuokoa maisha ya Watanzania wengi ambao wako hatarini kupoteza maisha kwa ugonjwa wa TB huku baadhi yao  wakihusisha maradhi yao na Imani za kishirikina.

Babu Manjenje alisema, waganga wa tiba asili katika wilaya hiyo wote kwa pamoja wamekubali kushiriki kikamilifu katika kampeni ya  kutokomeza ugonjwa huo ili kuokoa  maisha ya watu Watanzania wenzao ambao  bado wanaendelea kutokana na kukosa tiba sahihi ya magonjwa yanayowasumbua.

Ameipongeza Hospitali ya wilaya kwa kutoa mafunzo kwa waganga kwani yatasaidia wao kuwatambua wagonjwa wenye viashilia vya ugonjwa huo wanaofika katika vilinge kupata tiba na kusisitiza kuwa,mafunzo hayo yataepusha waganga wa tiba asili kuuwa watu wanaofika katika vilinge huku wakiwa na matatizo ambayo  matibabu yake ni ya kitaalam.

No comments:

Post a Comment

ANDIKA MAONI (COMMENTS) HAPO👇

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages