LATEST HEADLINES👉

Your Ad Spot

Jun 30, 2024

VIJANA WATAKIWA KUTENDA MEMA


 Na HEMEDI MUNGA, Iramba 


VIJANA wamekumbushwa wajibu wao wa kumkumbuka Mwenyezi Mungu ambae amewaumba hususan katika kipindi hichi  ambacho wanazo nguvu za kufanya mengi ikiwemo ibada.


Aidha, wametakiwa kula rizki za halali ambazo Mungu amewajalia na kutenda matendo mema ya kumpendeza Mungu kwa sababu kufanya hivyo itakua sababu ya wao kwenda peponi.


Wito huo,  ameutoa Shekhe wa wilaya ya Igunga mkoani Tabora, Hassan Dahir  alipokua akiongea na waumini wa Kata ya Shelui, wilayani Iramba mkoani Singida katika walima wa harusi.


Amesema mwanadamu ameheshimishwa sana na Mwenyezi Mungu  kuliko viumbe wengine wote.


"Sisi binadamu tumetukuzwa na mfumo wetu ni ibada, hivyo tuzidi kumuogopa Mwenyezi Mungu," ameomba.


Akizungumzia kuhusu ndoa, Shekhe Dahir ameeleza lengo la ibada hiyo, ni kuendeleza kizazi kwa kuwa zipo sababu mbalimbali zinazowachukuwa wanadamu ikiwemo mauti kutokana na  magonjwa, vita na ajali.


Pia, ameonesha mshangao dhidi ya wale wanaodaiwa kuwakataza  watu kuzaa sana licha ya  kuwepo kwa sababu hizo.


"Vinavyotuchukua vipo vingi, hivyo lazima tuzaliane kwa lengo la kuendeleza kizazi na udugu," amesisitiza.


Hata hivyo, amewataka wanaume kuendelea kutulia kwa lengo la kuchunga familia zao ikiwemo uchumi wao kwa kuepukana na kila aina ya koloni.


Ameweka wazi  tabia ya kutumia ujana na kumzalisha mtu  zaidi ya mmoja au sita bila utaratibu wa ndoa, hiyo ni fujo na haikubaliki katika jamii.


Pia,  amewataka wazazi kuacha tabia ya ubaguzi wa kiuchumi hususan vijana wanapokua wamependana na kutaka kuoana.


"Wale ambao hamjaoa msitake kujipanga sana, oweni kwa sababu kutofanya hivyo mtajikuta  katika kuongeza watoto wa mitaani," amesema.


Ameongeza tabia hiyo imekua ikileta shida ya upangaji wa bajeti  sio tu kwa mtu mmoja moja hata kwa serikali kwa kuto fuata utaratibu wa kisayansi aliouelekeza muumba.


Mbali na hayo, amewapongeza waumini wa dini hiyo kwa kuvaa mavazi ya heshima kwa sababu wanaisalimisha na kuifundisha dunia maadili mema huku akionya na kulaani  wale wanaotumia mavazi hayo kufanyia uchafu.

Shekhe wa wilaya ya Igunga mkoani Tabora,  Hassan Dahir akiwataka vijana kumcha Mwenyezi Mungu, wakati wa  hafla fupi ya walima wa harusi iliyofanyika katika kata ya Shelui wilayani Iramba mkoani Singida. (Picha na Hemedi Munga)

Shekhe Ponda Rukumbwe wa Msikiti wa Taqwa mjini Kiomboi akiteta jambo na Shekhe Abdi Kilita wa Shelui, wakati wa  hafla fupi ya walima wa harusi iliyofanyika katika kata ya Shelui wilayani Iramba mkoani Singida, Kulia ni Shekhe wa wilaya ya Igunga mkoani Tabora,  Hassan Dahir. (Picha na Hemedi Munga)

Baadhi ya Viongozi wa dini wakiwa katika walima wa harusi katika kata ya Shelui wilayani Iramba mkoani Singida. (Picha na Hemedi Munga)


No comments:

Post a Comment

ANDIKA MAONI (COMMENTS) HAPO👇

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages