LATEST HEADLINES👉

Your Ad Spot

Jun 27, 2021

YAFANYIENI KAZI KIKAMILIFU MAONI YA WADAU UBORESHAJI MITAALA YA ELIMU-NAIBU WAZIRI KIPANGA


Naibu  Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Omari Kipanga, akizungumza wakati akifungua Mkutano wa kupokea maoni ya Wadau kuhusu Uboreshaji wa Mitaala ya Ngazi ya  Elimu ya Awali, Msingi na Sekondari nchini ,ulioandaliwa na Wizara ya Elimu Sayansi na Teknolojia kupitia Taasisi ya Elimu Tanzania (TET) uliofanyika Juni 26,2021  kwenye Ukumbi wa Mikutano wa Jakaya Kikwete  jijini Dodoma.
Mwenyekiti Baraza la Taasisi ya Elimu Tanzania (TET), Prof.Bernadeta Killian akitoa neno la shukrani kwa Naibu Waziri wa Elimu Sayansi na Teknolojia, Omari Kipanga  baada ya kufungua Mkutano wa kupokea maoni ya Wadau kuhusu Uboreshaji wa Mitaala ya Ngazi ya  Elimu ya Awali, Msingi na Sekondari nchini.
Mkurugenzi Mkuu Taasisi ya Elimu Tanzania, Aneth Komba,akizelezea mitaala mbalimbali iliyopo na inayopendekezwa wakati wa Mkutano wa kupokea maoni ya Wadau kuhusu Uboreshaji wa Mitaala  hiyo.

Katibu Mkuu,Wizara ya Elimu,Sayansi na Teknolojia Dk.Leornad Akwilapo,akizungumza wakati wa Mkutano wa kupokea maoni ya Wadau kuhusu Uboreshaji wa Mitaala ya Ngazi ya  Elimu ya Awali, Msingi na Sekondari nchini

Mhadhiri wa Chuo cha St.John Dkt.Shadidu Ndossa ,akitoa maoni yake wakati wa mkutano wa kupokea maoni ya Wadau kuhusu Uboreshaji wa Mitaala ya Ngazi ya  Elimu ya Awali, Msingi na Sekondari hapa nchini.
Mbunge wa Viti Maalum (CHADEMA),Mhe.Grace Tendegu akitoa maoni kuhusu maboresho ya Mitaala ya Elimu wakati wa Mkutano wa kupokea maoni ya Wadau kuhusu Uboreshaji wa Mitaala ya Ngazi ya  Elimu ya Awali, Msingi na Sekondari nchini.
Baadhi ya wananchi na wadau kutoka taasisi mbalimbali wakifuatilia maoni wakati wa mkutano wa Mkutano wa kupokea maoni ya Wadau kuhusu Uboreshaji wa Mitaala ya Ngazi ya  Elimu ya Awali, Msingi na Sekondari chini.





Mwanafunzi wa Shule ya Sekondari Kiwanja cha Ndege,Shabani Masudi akitoa maoni yake kuhusu uboreshwaji wa Mitaala.

 PICHA NA RICHARD MWAIKENDA


NAIBU Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, ameiagiza  Bodi ya Taasisi ya Elimu Tanzania kuhakikisha inafuatilia kwa karibu na kuyafanyia kazi kikamilifu maoni yanayotolewa na wadau wa elimu kuhusu uboreshaji wa mitaala hiyo ili lengo la uboreshwaji mitaala hiyo liweze kufanikiwa.

 

Kipanga ambaye alimwakilisha Waziri wa wizara hiyo, Profesa Joyce Ndalichako aliyasema hayo wakati wa ufunguzi wa Mkutano wa kupokea maoni ya Wadau kuhusu Uboreshaji wa Mitaala ya Ngazi ya  Elimu ya Awali, Msingi na Sekondari nchini ulioandaliwa na wizara hiyo kwa ushirikiano na Taasisi ya Elimu Tganzania kwenye Ukumbi wa Jakaya Kikwete jijini Dodoma Juni 26,2021.

“Niwahimize Bodi ya Elimu Tanzania kuhakikisha inafuatilia kwa karibu maoni ya wadau na kuyafanyia kazi kikamilifu na kwa umakini mkubwa ili tuweze kufanikiwa katika uboreshaji mitaala hii,” amesisitiza Mhe. Kipanga.

Mhe. Kipanga amewataka wadau wa elimu kuendelea kutoa maoni na mapendekezo yao kupitia majukwaa yaliyopo ya kutolea maoni ili kuisaidia Serikali kuwa na mitaala bora na inayokidhi matarajio ya Watanzania.

Hata hivyo amewataka  washiriki wote wa kongamano hilo kushiriki kikamilifu kutoa maoni yao ambayo yatafanyiwa uchambuzi wa kitaalamu kwa lengo la kupata mitaala bora itakayolenga kwenye ujenzi wa ujuzi kwa wahitimu.

“Ni imani yangu kupitia mkutano huu mtatoa maoni na mapendekezo yatakayowezesha Serikali kuwa na mitaala iliyo bora zaidi na itakayokidhi matarajio ya Watanzania kwa ujumla,” amesema Mhe. Kipanga.

Amesema uamuzi wa kuboresha mitaala hiyo umetokana na kukua kwa maendeleo na mabadiliko ya dunia huku akisisitiza kuwa  serikali imezingatia pia malalamiko ya wadau.

“Mimi niwaombe tu muwe huru katika kutoa maoni kwa sababu yatasaidia katika kufanya elimu yetu kuboreka na kupata wahitimu tunawataka ambao watamaliza shule wakiwa na ujuzi wao tayari”amesema Mhe.Kipanga

Kwa upande wake,Katibu Mkuu, Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Dkt. Leonard Akwilapo amewashukuru wadau waliofika kwenye mkutano huo na kuwataka wadau wote nchini ambao hawakuweza kuhudhuria mkutano huo, kuwasilisha maoni yao kupitia fomu zilizopo kwenye tovuti ya Taasisi ya Elimu Tanzania (www.tie.go.tz) na namba ya simu 0735041169.

“Kwa kuzingatia hili napenda kumshkuru  Rais Samia kwa maelekezo ambayo ametoa kwa niaba ya Wizara kuhakikisha kazi hii inafanyika kwa weledi mkubwa,wadau wote mshiriki kikamilifu katika kutoa maoni,”amesema Dk Akwilapo.

Awali Mkurugenzi Mkuu wa TET, Dk. Aneth Komba amesema wanatarajia kuwa wadau watapata uelewa wa pamoja kuhusu maboresho ya mitaala hiyo ili watoe maoni yenye tija kwa elimu yetu nchini.

“Na imani kuwa tutapata maoni mengi yatakayoboresha Elimu yetu nchini,hivyo tushirikiane kuhakikisha tunafanikisha ubora wa elimu yetu kwa watoto ambao ni viongozi wajao wa taifa hili,” amesema Dk. Komba.

Naye Mwenyekiti wa Bodi ya TET, Profesa Bernadetha Killiani, amesema taasisi hiyo imejipanga kuhakikisha inaboresha mitaala kuendana na mahitaji ya sasa na kuzingatia maendeleo ya sayansi na teknolojia.

Akitoa maoni yake katika mkutano huo, Diwani wa Kata ya Mtumba, Edward Maboje (CCM) amesema kuwa haoni kama kuna tatizo kwenye mitaala bali anaona tatizo lipo kwenye utekelezaji wake kwa kuwa kuna uhaba wa madawati, vitendeakazi na miundombinu hafifu.

Habari kwa hisani ya Alex Sona wa Fullshangwe Blog


No comments:

Post a Comment

MAONI (COMMENTS)👇

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages