LATEST HEADLINES👉

Your Ad Spot

Mar 21, 2021

VILIO, SIMANZI KUANGUKA NA KUPOTEZA FAHAMU VYAENDELEA KUTAWALA JIJINI DAR ES SALAAM, KATIKA KUAGA MWILI WA KIPENZI CHA WATANZANIA DK. MAGUFULI, LEO

Na Bashir Nkoromo, CCM Blog

Vilio, simanzi, kuanguka na kupoteza fahamu vimeendelea kutawala wakati wananchi wakiendelea leo kutoa heshima zao kwa mpendwa wao aliyekuwa Rais wa Tanzania na Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Dk. John Magufuli katika Uwanja wa Uhuru, Temeke jijini Dar es Salaam.


CCM Blog imeshuhudia kwamba idadi ya wananchi kutoa heshima na kuuanga mwili wa Hayati Dk. Magufuli leo imekuwa kubwa zaidi  ikilinganishwa na jana kiasi cha kusababisha vyombo vya ulinzi na usalama kuongeza umakini kuhakikisha wananchi hao wanakuwa salama kwa kuwa Uwanja wote umejaa pomoni kiasi cha kusababisha mageti kufungwa ili walioko ndani wamalizike ndipo walioko nje waruhusiwe.


Kufuatia hali hiyo ya wingi wa wananchi, Mkuu wa Wilaya ya Temeke, Dar es Salaam ulipo Uwanja huo Godwin Gondwe kuna wakati amelazimika kutoa tangazo kwa wananchi kwamba watu ni wengi ambao wamefika kumuaga Dk.Magufuli na hivyo kuomba watu wote wakae chini ili kuwepo na utaratibu mzuri utakaowezesha wote waliofika kutoa heshima zao.


" Ndugu wananchi wote wa Dar es Salaam, tunawashukuru wote kwa kuja kwa ajili ya kumuaga Mpendwa wetu na kutoa heshima, tunawahakikishia wote mtapata nafasi, lakini kwa idadi ya watu walioko hapa naomba walioko majukwaani wasinyanyuke hadi watakaporuhusiwa, walioko nje wasiingie wabakie huko  hadi wa ndani wapungue, " akasema Gondwe.


Kufuatia watu kuanguka na wengine kupoteza fahamu baada ya kutoa heshima zao za mwisho kwa mwili wa Dk. Magufuli watoa huduma ya usaidizi wamelazimika kuwa na kazi ya mara kwa mara ya kuwabeba na kuwaondoa watu wanaoanguka ili kuwezesha wengine nao kupata nafasi ya kuaga.


Bila shaka wingi huo wa watu umetokana na kila mwananchi kuhakikisha anauaga mwili wa Dk. Magufuli kwa kuwa kwa mujibu wa ratiba leo ndiyo siku ya mwisho kwa wananchi wa Dar es Salaam kumuaga Dk. Magufuli kipenzi cha Watanzania.


Kwa mujibu wa raiba hiyo baada ya Mwili kuagwa jijini Dar es Salaam kwa mara ya mwisho, jioni mwili utasafirishwa kwa ndege kwenda Jijini Dodoma ili wananchi wa jiji hilo na mikoa ya jirani wamuage na baadae mwili kupelekwa Zanzibar halafu Mwanza na kumalizia Chato mkoani Geita ambako atapumzishwa kwenye nyumba yake ya milele.


Wananchi kadhaa waliozungumza na Mwendeshaji Mkuu wa Blog hii ya Taifa ya CCM kwa nyakati tofauti, wamesema kifo cha mpendwa wao Dk. Magufuli kimewaumiza mno kwa kuwa alikuwa akiwapenda wananchi wote na hasa wanyonge wakisema watamkubuka kwa maono yake ya kuivusha Tanzania kwenye neema huku akisimamia maono yake hayo kwa ujasiri na uthubutu na kufanya maamuzi ambayo kuna mengine yalionekana kama ni magumu.


Zifuatazo ni picha za taswira ya matukio mbalimbali wakati wananchi wakiaga Mwili wa Dk. Magufuli katika Uwanja wa Uhuru, Temeke jijini Dar es Salaam

No comments:

Post a Comment

MAONI (COMMENTS)👇

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages