LATEST HEADLINES👉

Your Ad Spot

Jan 13, 2021

HOSPITALI YA UHURU DODOMA YAANZA KUTOA HUDUMA KWA WAGONJWA+video

Hospitali ya Uhuru iliyopo Chamwino, Dodoma.
Mganga Mkuu Mfawidhi wa Hospitali ya Uhuru, Dkt. Pius Kagoma.

Dkt. Pius Kagoma akizungumza na wanahabari kuhusu kuanza kwa huduma  katika hospitali hiyo. Picha na Richard Mwaikenda


 

Na Richard Mwaikenda, Dodoma

HOSPITALI  ya Uhuru iliyopo wilaya ya Chamwino, Dodoma tayari imeanza kutoa huduma kwa wagonjwa tangu Desemba 21, mwaka jana.

 

Akizungumza na waandishi wa habari hospitalini hapo jana, Mganga Mfawidhi wa hospitali hiyo, Dkt. Pius Kagoma, amesema kuwa hadi juzi Januari 11, wamehudumia takribani wagonjwa 239.

 

Amesema  hadi sasa watumishi 50 wamesharipoti kazini na wengine wanaendelea kuwapokea kwa ajili ya kutoa huduma kwa wagonjwa hospitalini hapo.

 

Aidha, Dkt. Kagoma amesema licha ya miundominu michache kuwa katika hatua za mwisho kukamilishwa, lakini hadi sasa  asilimia 99 hospitali hiyo imekamilika na wanasubiri ufunguzi rasmi.

 

Dkt. Kagoma ametaja wagonjwa wanaoendelea kuwatibia kuwa ni; wagonjwa wanachama wa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF), Mfuko wa Afya ya Jamii (CHF),  na wagonjwa wanaotibiwa bure ambao ni wazee, wajawazito na watoto chini ya umri wa miaka mitano pamoja na wananchi wengine.

 

Kuhusu vifaa vya tiba, Dkt. Kagoma amebainisha kuwa vipo vya kutosha vikiwemo vya vifaa vya mionzi, madawa na vya kujifungulia na kwamba vingine  vinaendelea kuletwa.

 

Alitaja baadhi ya changamoto zilizopo kuwa ni; kutokamilika kwa ujenzi wa barabara ya kuingia hospitalini hapo, baadhi maboma ya maji kutotoa maji lakini anaamini kwa muda mchache uliobakia mambo yote yatawekwa sawa.

 

Hospitali hiyo  ambayo imejengwa baada ya Rais John Magufuli kuelekeza huko fedha zilizotakiwa kutumika katika maadhimisho ya Sikukuu za Uhuru na gawio la serikali  kutoka Kampuni ya Simu ya Airtel, itakuwa na uwezo wa kuhudumia wagonjwa kati ya 500,000 hadi 1,000,000 kwa mwaka.

 

Dkt. Kagoma amesema kuwa kwa asilimia kubwa itakuwa inahudumia watumishi wa Ikulu ya Chamwino, watumishi kutoka Mji wa Kiserikali wa Mtumba, wananchi wa vijiji  jirani pamoja na wananchi wote kwa ujumla.

 

Alisema amefurahi sana kuwa miongoni mwa watumishi wa kwanza kuhudumia hospitali hiyo mpya na kuahidi kwamba yeye na watumishi walioko chini yake watafanya kazi kwa bidii ikiwa ni sehemu ya kuunga mkono juhudi za Rais Magufuli za kufanikisha hospitali hiyo kujengwa.


Kwa uhondo zaidi wa tukio hili naomba uendelee kusikiliza kupitia kwenye video hii....

IMEANDALIWA NA;
 RICHARD MWAIKENDA
 MHARIRI BLOG YA TAIFA YA CCM
 0754264203

No comments:

Post a Comment

MAONI (COMMENTS)👇

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages