Samir Ibrahim

Kijana mtanzania Samir Ibrahim amepata fursa ya kuingia katika orodha ya vijana 20 bora katika tuzo za Jack Ma foundation kwa wajasiriamali wa Afrika.

Samir mwenye makazi yake mjini Nairobi ni mjasiriamali wa pembejeo za kilimo zinazowezesha uzalishaji wa mazao kwa wakulima wadogo.

Tuzo za Jack Ma zinalenga kuwainua mashujaa wa biashara kote Afrika ili kupambana na vizuizi mbalimbali vya maendeleo.

''Kuwa miongoni mwa vijana wafanyabiashara waliongia katika hatua ya ishirini bora katika tuzo za Jack Ma imenipa moyo sana.

Ni heshima kubwa sana kwangu kuwa miongoni mwa watu hao.

Lakini kikubwa zaidi ni kwamba Jack anafahamu kwamba Afrika ina matatizo ya upatikanaji wa chakula , Sasa virusi vya corona pia vimeendelea kusababisha uhaba mkubwa, zaidi ya watu milioni 265 wanaweza kuwa na uhaba wa chakula.

Kwa hivyo tuzo niliyopewa ambayo inatambua umuhimu wa kampuni yangu katika kuwasambazia vifaa vya kilimo wakulima nchini Kenya inaashiria kwamba wakulima wadogo wanaweza kusaidia kuilisha dunia''.

Aliomgeza kusema: ''Nafikiri ujasiriamali ni kitu muhimu sana kwa sababu unaniruhusu kuwafikia watu wengi ambao wasingeliweza kufikiwa.

Unanisaidia pia kutumia rasilimali ambazo nimebarikiwa kuwa nazo kusaidia kutatua changamoto zao, kwa hivyo huwa tunasema tunatafuta suluhisho na wateja wetu kwa wateja wetu.

Kwa hivyo tuzo na nafasi hii inanifanya kuendelea kuwa mbunifu zaidi ili kuleta Amani kwa watu duniani kote''