LATEST HEADLINES👉

Your Ad Spot

Mar 31, 2020

MAKALA: AWAMU YA TANO IMEKOLEZA RADHA YA TANZANIA


Na Mwl. Salehe S. Msonga
UVCCM CHAMAZI

UTANGULIZI:
Kidumu Chama Cha Mapinduzi!!
Mnamo 02/06/2018 niliandika Makala iliyoitwa ‘SIRI KUBWA YA CCM HII HAPA, ni Makala iliyosambazwa kwenye makundi ya WhatsApp na ilijikita zaidi katika kuonesha ni siri gani inayoifanya CCM kushinda na kuwa na uhakika wa kushinda kila chaguzi kuu nchini, ambapo mwandishi aliivujisha siri hiyo hadharani ya kuwa ni KUHANGAIKA NA SHIDA ZA WATU kupitia utekelezaji mzuri wa ilani yake. Leo mwandishi yule yule nakuja na Makala hii nyingine inayoonesha ni kwa jinsi gani serikali ya awamu ya tano ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inavyokoleza radha ya nchi yetu ya Tanzania kwa watanzania.
Tangu kuundwa kwake toka kwenye muungano wa Tanganyika na Zanzibar mnamo 1964, Tanzania imekuwa na jumla ya awamu tano za uongozi wa nchi ambazo kwa bahati nzuri zote zimetokana na Chama Cha Mapinduzi (CCM). Tanzania imekuwa ni nchi yenye tunu nyingi za taifa ambazo zinatutangaza kama nchi kimataifa sambamba na kumnufaisha mtanzania mwenyewe. Baadhi ya tunu hizo ni Amani na Utulivu, Madini mbalimbali, Ardhi yenye rutuba, Lugha moja ya kitaifa licha ya kuwa na makabila na tamaduni zaidi ya 120, Hifadhi kemkem za wanyama pori, Bahari, Maziwa na Mito mikubwa, Milima mirefu na miundo mbinu mikuu muhimu kwa uchukuzi na usafirishaji. Kuna baadhi ya tunu hizi adimu katika baadhi ya nchi za afrika na hata nje ya afrika. AMANI na UTULIVU ni tunu kuu kwa nchi yetu kwani tunashuhudia mataifa mengi duniani yamekuwa yakivutiwa nayo na hata Tanzania kuwa ndiyo kipenzi chao kiutalii na hata kimbilio lao pale wapatapo  matatizo mbalimbali nchini mwao mfano wakimbizi.
RADHA YA TANZANIA YAKOLEA
Radha ya u-tanzania imezidi kukolezwa na kuongeza ufahari wetu na kujivuia kuwa watanzania, hii ni kutokana na awamu ya tano ya serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ilivyo na inavyojidhatiti katika kuongeza kasi ya kuzigeuza tunu za taifa (Transformation) kuwa mkombozi wa mtanzania hasa yule wa hali ya chini ili naye si aionje tu, bali ale keki ya taifa lake. Haya yanaonekana pale tunaposhuhudia utendaji na usimamizi makini wa viongozi mbalimbali wa serikali wakiongozwa na Rais John Pombe Magufuli katika sekta mbalimbali kwa lengo la kumsogezea karibu mtanzania wa kawaida fursa, nyenzo na njia za kujifanyia maendeleo yake ya kila siku
Mnamo mwezi oktoba, 2020, serikali ya awamu ya tano inaelekea kutimiza miaka mitano kamili huku ikiwa imeshashughulikia karibia kila sekta muhimu kwa ustawi wa mwananchi wa leo na hata wa kesho.
Tukianza na sekta ya nishati, tunaona hatua kubwa tuliopiga kama nchi, kwani ndani ya miaka minne tu, tumeona mafanikio yafuatayo katika sekta ya nishati: Ongezeko la megawati 480 za umeme katika gridi ya Taifa, Bilioni 138 zimeokolewa kwa kutokana na kuachana na matumizi ya mitambo mikubwa ya kufua umeme wa mafuta, Uwepo wa ziada ya umeme usiopungua megawati 280 kwa siku, Kusitisha uagizaji vifaa vya umeme nje ya nchi, Tanesco kutoka kampuni inayopata hasara na kuwa inayotengeneza faida na kujiendesha pasipo ruzuku, Ongezeko la asilimia 400 uunganishaji wa umeme vijijini, Gesi asilia imefikia futi za ujazo trilioni 57.54  na pia Uwepo wa mafuta yanayotosheleza mahitaji pamoja na akiba. Haya yote ni mafanikio ya kujivunia ambayo nchi za wenzetu hususani majirani zetu pengine huumiza kichwa ni kwa namna gani Tanzania tumeweza kuyafikia kwa muda mfupi huu. Nasema ni mafanikio ya kujivunia ni kwa kuwa mtanzania amepunguziwa mzigo mkubwa uliomuelemea katika kuijenga nchi yake.
Pia serikali ya awamu ya tano imeifanya Tanzania kuwa ni nchi ya kwanza barani Afrika kwa kusambaza umeme karibia nchi nzima. Sote tunashuhudia jinsi mpango wa REA ulivyomfikishia huduma ya umeme mwananchi wa kijijini tena kwa gharama nafuu kabisa hali iliyompelekea mwananchi kuutumia umeme huo katika shughuri za uzalishaji na biashara hatimaye kumuinua kiuchumi huku serikali ikipata kodi yake (mutual relationship). Kwa mujibu wa waziri wa nishati, Tanzania imeongoza barani Afrika kwa usambazaji wa umeme vijijini kwa asilimia 73.4 ikifuatiwa na nchi ya Nigeria. Binafsi ni shuhuda kwa hili kwani nilistaajabishwa pale disemba 2019, niliporudi nyumbani Mwaya-Mang’ula wilayani Kilombero kusalimia ndugu na jamaa na kukuta vile vijiji vya zamani na vya nje ya mji na maeneo ya mbali yaliyokuwa ni mashamba ya wanakijiji tuliyokuwa tukilima kipindi hicho ya Msalise, Mhelule, Mikoleko n.k. navyo vyote vikiwa vimesambaziwa umeme wa uhakika na shughuri za kiuchumi zikiongezeka hali iliyovibadili vijiji na maeneo hayo kuwa si mashamba tena bali ni makazi ya uhakika na yenye kukua kwa kasi. Kama hiyo haitoshi, pia serikali ya awamu ya tano iko katika ujenzi wa mradi mkubwa wa umeme wa bwawa la Mwl. Nyerere katika mto Rufiji, mradi ambao utazalisha zaidi ya megawati 2000 za umeme na kuziingiza katika gridi ya Taifa na kufanya gharama za umeme nchini kushuka mara dufu na pengine hata kuweza kuuza umeme wa ziada kwa nchi nyingine za jirani. Hii kwa upande mwingine itachochea zaidi kasi ya Tanzania ya viwanda kwani rasilimali ya nishati itakuwa ya uhakika na ya bei ya chini pia kusababisha ongezeko la upatikanaji wa ajira viwandani. Hakika huku ni kuzigeuza tunu za taifa za mito mikubwa kuwa mkombozi kwa mtanzania mwenyewe.
Tukija katika sekta ya afya na maendeleo ya jamii, kwa ufupi hapa tunajionea jinsi serikali ilivyowahurumia mwananchi wake kwa kuongeza idadi ya zahanati nchini kutoka 6,044 hadi kufikia 6,400, idadi ya vituo vya afya kutoka 718 hadi 1169, idadi ya hospitali za halmashauri kutoka 186 hadi kufiki 321 na kukarabati hospitali za rufaa  za mikoa 23. Kutokana na miundombinu iliyojengwa , idadi ya vituo vya  kutolea huduma za afya nchini imeongezeka kutoka  7,014 hadi 8,446 ndani ya miaka 4 ya awamu hii ya tano. Pia tumeshuhudia upanuzi na uongezwaji wa vifaa tiba na vitendea kazi vya kisasa kwa hospitali ya taifa ya muhimbili na zinginezo mfano hospitali moyo ya Jakaya Kikwete, hospitali ya kansa ya Ocean road, hospitali ya Benjamin Mkapa Dodoma na hospitali ya MOI sambamba na uimarishwaji wa bohari kuu ya dawa nchini, Medical Store Department (MSD). Hii imepelekea idadi ya wagonjwa wanaosafiri kwenda nje ya nchi kwa ajili ya matibabu kupungua kulinganishwa na hapo awali, pia hii imeifanya serikali kuokoa pesa nyingi baada ya wagonjwa wengi kutibiwa hapa hapa nchini. Vivo hivyo kwa upande wa ustawi wa jamii, serikali imeongeza fedha zaidi kwenye mfuko wa TASAF kwa ajili ya kaya zisizojiweza sambamba na uimarishwaji / uboreshwaji wa utoaji bure wa huduma za afya kwa wazee. Binafsi hili naitafsiri kama ni kudhihirisha kwa vitendo ile moja ya imani ya CCM ya kwamba BINADAMU WOTE NI SAWA, hivyo kila mtu anastahili kupata huduma sawa kama wengine.
Katika sekta ya elimu, awamu hii ya tano imewatua jukumu na mzigo wazazi wote nchi nzima wa kuwalipia watoto wao karo za shule katika shule za umma na badala yake serikali imebeba mzigo huo na inatumia zaidi ya shilingi bilioni 23 kila mwezi kuwalipia wanafunzi hao. Pia serikali imewajengea uwezo na mazingira rafiki walimu wakuu, wakuu wa shule na maafisa elimu kata katika kusimamia vyema sera hii ya utoaji elimu bure. Serikali inafanya hivyo kwa kuamini ya kuwa elimu ndio ufunguo wa maisha ya mtoto. Sera ya elimu bure kuanzia darasa la kwanza hadi kidato cha nne ilianza rasmi mnamo mwaka 2016 na ikapelekea ongezeko kubwa la udahili wa wanafunzi shuleni. Hii inamaanisha ya kuwa kabla ya sera ya elimu bure kuna watoto wa kitanzania wa hali ya chini walikuwa wanakosa haki yao ya kupata elimu kutokana na wazazi kukosa pesa za kulipia karo, hivyo ujio wa sera hii ikaleta usawa kwa wote kwamba kila mtu apate elimu na hatimaye kuendana na lengo endelevu namba nne la dunia yaani Sustainable Development Goals (SDGs) la elimu bora kwa wote ambapo serikali kila uchwao inajitahidi kuifanya elimu yetu iwe bora zaidi kwa kuboresha usimamizi, miundo mbinu, na vifaa vya elimu. Huku nako ni kulekule kudhihirisha ya kuwa CCM ni chama kinachojali usawa wa watu kwa kuamini ya kuwa BINADAMU WOTE NI SAWA hivyo kila mtu anastahili huduma sawa kama mwengine.
Tukiiangazia sekta ya ujenzi, uchukuzi na usafirishaji, nayo imezidi kwa kasi kubwa kumfungulia fursa za kimaendeleo mwananchi. Hii ni kutokanana na ujenzi wa miundombinu rafiki kwa shughuri za uzalishaji mali, kilimo, utalii, na biashara kwa watanzania wengi.
Kwa upande wa usafiri wa chini/ardhi, msukumo mkubwa wa Mhe. Rais John Pombe Magufuli juu ya usimamizi makini wa majukumu ya TANROAD na TARURA umekuwa chachu ya uboreshwaji wa miundombinu ya barabara nchini hasa ukizingatia miundo mbinu ya usafirishaji na mawasiliano ni msingi mkuu wa maendeleo ya kiuchumi kote duniani.. Hapa tunaona barabara kuu na za kawaida karibia nchi nzima zikiwa zimejengwa kwa kiwango cha lami, zikiunganisha makao makuu ya wilaya na vijiji mbalimbali. Uboreshwaji huo umerahisisha usafirishwaji wa bidhaa na mazao ya kibiashara kutoka yanakozalishwa kwenda kwenye masoko mbalimbali na hata kurahisisha/kuongeza ukaribu na mawasiliano zaidi kati ya wananchi vijijini na makao makuu ya wilaya zao kwa mahitaji ya huduma mbalimbali za kiutumishi na kiraia. Kwa wakazi wa jiji la Dar es Salaam, kwa miaka mingi wamekuwa wahanga na kupoteza muda wao mwingi wakiwa barabarani kwa ajili ya foleni kubwa za magari, lakini hivi punde wananchi wameshuhudia ufanisi uliopatikana kwa kujengwa daraja la Mwl. Nyerere pale Kigamboni na barabara inayopita juu katika makutano ya barabara ya Mandela na Nyerere (Mfugale fly over). Hii imepelekea wananchi kutopoteza tena muda wao mwingi katika shughuri zao za uzalishaji mali na hata hivyo itakapokamilika “fly over” ya pale Ubungo hivi karibuni na za sehemu zingine, upanuzi wa barabara ya Morogoro na ujenzi wa barabara ya mwendokasi ya Mbagala, ndipo tatizo la foleni jijini Dar es Salaam litakapokwisha kabisa na kuwa historia ya nchi. Kubwa lao katika haya, ni ujenzi wa reli ya treni ya kisasa, Standard Gauge Railway (SGR) inayoanzia Dar es Salaam hadi Dodoma kwa awamu ya kwanza na ya pili kuanzia Dodoma hadi Mwanza na Kigoma. Kukamilika kwa treni hii ya SGR kwa awamu ya kwanza, kutawafanya watanzania kutumia takribani saa 3 tu kutoka Dar es Salaam hadi Dodoma na kurahisisha shughuri zote za kiuchumi kwani watu wataweza kuishi Dodoma na kufanya kazi/biashara zao Dar es Salaam ambapo kwa usafiri wa basi hutumia si chini ya saa 8 kati ya Dar es Salaam na Dodoma. Lakini pia SGR itakuwa ni mwarubaini wa usafirishaji wa mamia ya tani za mizigo inayotoka bandarini na kuelekea mikoani au nchi jirani na kuiletea serikali biashara na faida kubwa na ya haraka hivyo kukuza uchumi kwa kasi. Huku kote ni kumlenga mtanzania aweze kufanya shughuri zake za kiuchumi kwa wakati stahiki, katika mazingira rafiki na hatmaye kuifurahia radha halisi ya nchi yake sambamba na kujivunia kwa fahari kubwa kuwa mtanzania katika dhana ya ushindani wa kimaendeleo na nchi zingine za kiafrika, lakini pia kupata huduma zote za msingi kwa ubora zaidi kwani serikali itakuwa ni yenye pato kubwa na la uhakika la kuweza kubuni, kuboresha na kusambaza zaidi huduma hizo mfano maji, elimu, pembejeo n.k.
Kwa upande wa usafiri wa anga napo moto ni uleule, awamu ya tano imefufua ile tunu ya taifa iliyofifia kwa nchi kutokuwa na ndege zake yenyewe. Serikali ya awamu ya tano kupitia pesa zake yenyewe, imeweza kunua ndege 11 za kisasa na za aina tofauti tofauti na hatimaye kulipa uhai shirika la ndege nchini, ATCL sambamba na kuipandisha heshima ya nchi yetu kimataifa. Hii pia imeongeza idadi ya watalii kuja nchini kwani ndege zetu zitakuwa zikienda nchi fulani za ughaibuni na kuja moja kwa moja nchini pasipo kupitia nchi zingine hivyo kupunguza safari ndefu na ya kuunga unga kwa watalii kuja nchini. Hili limeenda sambamba na upanuzi na ujenzi wa viwanja mbalimbali vya ndege nchini na kuifanya sekta ya anga nchini kutengemaa hatmaye kurahisisha usafiri wa haraka n.k. Hii ni fahari kwa mtanzania.

MWISHO
Kwa kumalizia ni vyema nigusie umakini na maono ya kweli ya serikali katika suala zima la kupunguza matumizi yasiyo ya lazima serikalini mfano safari za holelaholela za nje ya nchi, gharama za uendeshaji wa vikao, uwepo wa wafanyakazi hewa serikalini, wanafunzi hewa kuanzia shule za misingi hadi vyuo vikuu na hata ufisadi katika ofisi nyeti za umma. Lakini pia, serikali imejitahidi kwa kiasi kikubwa sana kudhibiti upotevu mkubwa wa mapato na nyara za serikali mfano kuufanyia marekebisho usimamizi wa mamlaka ya mapato Tanzania (TRA), kuijengea nguvu na makali TAKUKURU, kudhibiti ujangiri wa wanyama pori na ujenzi wa ukuta kuuzunguka mgodi kule Mererani ili kudhibiti utoroshaji wa madini ya Tanzanite. Upotevu huo wa mapato ulikuwa ukiiletea hasara kubwa nchi yetu na hatmaye kufifisha jitihada za kuharakisha maendeleo ya watanzania walio wengi na hata kuzimisha matumaini ya kesho yao sambamba na uzalendo kwa taifa lao. Pia ukawa ni  mzigo mkubwa kwa mlipa kodi kwani pesa nyingi ilikuwa ikipotea. Hakika awamu ya tano ndani ya miaka michache hii, imeweza kumulika kila sekta na kuondoa kwa asilimia kubwa uzembe uliokuwa ukiigharimu nchi na kuirudisha nyuma katika safari ya kujiimarisha kiuchumi na katika kumkomboa mwananchi. Kwa kufanya hivyo, (kukomesha uzembe huo), nafuu huja kwa mwananchi wa kawaida ambaye anaitegemea serikali imjengee mazingira rafiki ya kimiundo mbinu ya usafirishaji na uchukuzi, afya, elimu, kilimo na kibiashara ili yamrahisishie shughuri zake za kiuchumi ziende vizuri na kukuza kipato chake na cha familia yake, hatmaye ndio maendeleo ya taifa zima. Huku ndiko nakokuita kuzigeuza tunu za taifa kuwa mkombozi wa mtanzania hasa yule wa hali ya chini ili naye si aionje tu, bali ale keki ya taifa na kuifurahia fahari ya nchi yake hatimaye kuongeza kiwango cha uzalendo kwa taifa lake. Hakika AWAMU YA TANO YAKOLEZA RADHA YA TANZANIA, mweeeh!!

Mungu ibariki Tanzania!
Mungu ibariki Afrika!
Ameen!
xxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxx
 REJEA
 Jarida la Nishati-Toleo Na.11   www.nishati.go.tz
TUNATEKELEZA 2020, Video clip. Channel ten TV

No comments:

Post a Comment

ANDIKA MAONI (COMMENTS) HAPO👇

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages