LATEST HEADLINES👉

Your Ad Spot

Feb 2, 2020

MACHINGA WASHAURIWA KUTOKATA TAMAA, WATEMBEE KIFUA MBELE

PWANI, Tanzania
WAFANYABIASHARA wadogo wadogo maalufu kama “Machinga” wametakiwa kutokata tamaa na badala yake watembee kifua mbele kwa kujiamini kwamba hawana tofauti na wenye mitaji mikubwa.

Rai hiyo imetolewa jana na Mshauri Mkuu wa Shirika la Umoja wa Machinga Tanzania Christopher Sanya wakati akizungumza na uongozi wa juu wa shirika hilo mkoani Pwani.

Alisema wafanyabiashara hao ni nguzo muhimu sana kiuchumi hasa katika kipindi hiki cha Serikali ya awamu ya Tano iliyojikita katika uchumi wa viwanda.

Sanya alisema kwa kutambua hilo, ndio maana Serikali imeweka mkakati maalumu wa kuwtambua Machinga kwa kuwapa vitambulisho ili wasiweze kubugudhiwa hovyo.

“Ni wakati wenu wa kujiamini na kutembea kifua mbele kwa kuwa Serikali hii ya Rais John Magufuli inawajali sana na kufikia hatua ya kuwawekea mazingira mazuri tofauti na hapo awali ambapo  Machinga alionekana kama mtu muhuni tu na kukimbizwa kimbizwa kila wakati huku wakipoteza mali zao,” alisema Sanya.

Alisema ni wajibu wa wafanyabiashara hao sasa kutumia vizuri nafasi hiyo kwa kujenga uaminifu kwa serikali yao ili kujikwamua kiuchumia zaidi.

“Ninyi ni wawakilishi wa Serikali. Hakikisheni mnaitumia vizuri fursa hii mliopewa tofauti na zamani ambapo mlikuwa mkitumiwa na wafanyabiashara wakubwa kuwauzia bidhaa zao kwa lengo la kukwepa kulipa kodi.

“Hakikisheni kwamba kila mnapokwenda kununua bidhaa zenu kwenye maduka makubwa mnapewa risiti halisi inayolingana na bidhaa iliyonunuliwa. Kwa kufanya hivyo mtakuwa mabalozi wazuri wa serikali hii katika kukuza uchumi wake na kulifanya Taifa lizidi kuinuka kichumi,” alisema Sanya.

 Haya hivyo, Sanya alisema kwa nafasi yake kama Mshauri Mkuu wa shirika hilo, atahakikisha atashirikiana na Serikali na wadau wengine wapenda maendeleo kutoa elimu ya biashara kwa Machinga.

Alisema elimu ya kibiashara kwa Machinga itawafanya wawe na uelewa mkubwa na kuweza kutunza mitaji yao ili isitumike kiholela.

“Lazima tushirikiane na wadau husika ili mpate elimu ya kufanya biashara. Kinyume na hapo hamtafika mbali maana nimeshuhudia vijana wengi wamekuwa wakichukua mikipo na kuitumia kwa mambo mengine kama vile anasa badala ya malengo yaliyokusudiwa kuomba mkopo huo,” alisisitiza Sanya.

Kwa mujibu wa Sanya, hakuna mfanyabiashara aliyezaliwa au kuanza biashara zake akiwa bilionea bali ni kwa mtaji mdogo na hatimaye kufikia hatua ya juu zaidi.

Sanya ameishukuru na kuipongeza Serikali kwa kitendo chake cha kuwatambua Machinga kama ni kiungo muhimu katika kukuza uchumi wake.

‘Naiopongeza Serikali yangu ya CCM hasa hii ya Awamu ya Tano chini ya Rais John Magufuli kwa jitihada zake za kuinua uchumi. Ni wajibu wa kila Mtanzani kuunga mkono juhudi hizi ili tuondokane na umaskini,’ alisema.

Katika hatua nyingine Sanya aliikumbusha CCM kuhakikisha inakuwa karibu na Serikali yake na isisite kuikosoa pale inapoona inakwenda kinyume na Ilani yake.

Alisema Serikali iliopo madarakani ni ya CCM hivyo inapaswa kutekeleza ipasavyo Ilani yake kwa kuwaletea wananchi maendeleo mbalimbali.

Mshauri huyo aliongeza akuwa endapo Ilani ya CCM itatekelezwa ipasavyo, ana imani kuwa Watanzania wataendelea kuiamini zaidi na kuichagua tena katika chaguzi nyingine zijazo.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Shirika hilo Filemon Maliga aliishukuru Serikali kwa kuwatambua na kuongeza kuwa shirika lake linakabiliwa na changamoto nyingi.

Alizitaja baadhi ya changamoto kuwa ni ukosefu wa vitambulisho kwa wafanya biashara hao na kukosa elimu kuhusu kuendesha mitaji yao.

Maliga alisema katika mkoa wa Pwani kuna upungufu mkubwa sana wa vitambulisho hivyo na kuiomba Serikali ifanye jitihada za haraka ili viweze kuwafikia wengine.

Alifafanua kuwa katika mkoa huo vilitolewa vitambulisho 60,000 ambavyo kimsingi havikukidhi haja ya wahitaji.

No comments:

Post a Comment

MAONI (COMMENTS)👇

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages