LATEST HEADLINES👉

Your Ad Spot

Nov 25, 2019

MSAJILI HAZINA AELEZA WALIVYOFANIKIWA KUONGEZA KIWANGO CHA MAKUSANYO YA MAPATI YASIYO YA KODI


Msajili wa Hazina, Athumani Mbuttuka akitoa hotuba yake katika hafla ya kupokea Gawio la Serikali iliyofanyika, Ikulu Chamwino, jijini Dodoma leo. Picha na Othman Michuzi.

Na Said Mwishehe, Michuzi Globu ya jamii 

MSAJILI wa Hazina Athumani Mbuttuka amesema kwa sasa wanajivunia kuongeza kiwango cha makusanyo ya mapato yasiyo ya kodi kutoka katika kampuni, taasisi, na mashirika ya umma yanayotokana na gawio, michango ya asilimia 15, na mapato ya Taasisi na Mashirika ya Umma, marejesho ya mtaji uliozidi, na ziada ya mwisho wa mwaka.

Mafanikio hayo yametokana na utekelezaji wa maagizo ya Rais Dk.John Magufuli aliyoyatoa mwaka 2018 wakati wa mashirika, taasisi na kampuni mbalimbali zikitoa gawio kwa Serikali. 
Mbuttuka amesema hayo leo Ikulu ya Chamwino Mjini Dodoma wakati wa Taasisi, Mashirika na Kampuni mbalimbali zikabidhi gawio kwa Serikali ambapo hundi hizo zimepokelewa na Rais Dk.Magufuli.

Amefafanua kuwa hundi ambazo zimepokelewa zinajumuisha Mapato ya Mwaka wa Fedha unaoishia Juni 31 mwaka 2019 na kwamba katika kipindi cha miaka mitano, makusanyo ya mapato kutokana na uwekezaji kwenye mashirika ya umma na kampuni ambazo Serikali ina hisa yameongezeka  kufikia Sh.trilioni 1.05 mwaka 2018/19 kutoka Sh.bilioni 161.04 mwaka 2014/15, ikiwa ni ongezeko la asilimia 552.
Ameongeza katika makusanyo hayo, Sh. bilioni 683.23 ya makusanyo yote kwa mwaka ulioishia Juni 30, 2019 yalipitia katika Akaunti ya Msajili wa Hazina na Sh.bilioni 370.59 ziliwasilishwa moja kwa moja kwenye Mfuko Mkuu wa Serikali kutoka Michango ya Mamlaka ya Bandari Tanzania, Bodi ya Michezo ya Kubashiri, Mamlaka ya Anga Tanzania; na Shirika la Maendeleo ya Mafuta na Petroli Tanzania.

Amesema kuwa mapato hayo yanatokana na gawio, michango ya asilimia 15 na huduma za jamii. ongezeko hili la mapato limechangiwa na maelekezo yako thabiti kwa Mashirika na Taasisi za Umma katika kuimarisha makusanyo na kupunguza matumizi yasiyo na tija; ukusanyaji wa maduhuli kwa mfumo wa kieletroniki [GePG],
Aidha, Udhibiti wa Matumizi; na kuongeza usimamizi wa Mashirika ya Umma na Makampuni yanayomilikiwa kwa hisa chache na Serikali. Masuala mengine ni ufuatiliaji wa kina na mapitio ya mikataba ya wanahisa, mikataba ya kimenejimenti na mikataba ya misaada ya utaalamu katika makampuni yanayomilikiwa kwa hisa chache na Serikali.

Pia, ufuatiliaji wa matumizi kwa Mashirika na Taasisi za Umma, mapitio ya sera za gawio, kutoa miongozo kwa bodi za wakurugenzi, kupitia mipango-mkakati na mipango ya biashara, na kuingia mikataba ya utendaji na Bodi za Wakurugenzi za Mashirika ya Umma.

Amesema kuwa ulipaji wa gawio umeimarika zaidi kwenye mashirika ambayo Serikali inamiliki hisa zaidi ya asilimia 50 ambapo rejesho la mtaji limeendelea kukua kutoka asilimia 1.5 mwaka 2014/15 hadi asilimia 7.21 mwaka 2018/19 ikilinganishwa na kampuni zinazomiliki hisa chini ya asilimia 50, ambapo rejesho la mtaji limeongezeka kutoka asilimia 5.3 mwaka 2014/15 hadi asilimia 6.64 mwaka 2018/19. Hali hii inaonesha ufanisi katika Mashirika ya Umma una imarika.

"Idadi ya Kampuni na Mashirika yanayotoa gawio na kuchangia katika Mfuko Mkuu wa Serikali ni ndogo ikilinganishwa na idadi iliyopo na ukubwa wa sekta. Kampuni na Mashirika 40 kati ya 81 yaliyopaswa kutoa gawio yameshindwa kutokana na kujiendesha kwa hasara au kuwa na mtaji mdogo,"amesema.

Amebainisha kazi ya kurekebisha Mashirika na Makampuni wanayoyasimamia inaendelea. Hadi kufikia mwezi Juni 2019, mashirika 15 yaliunganishwa na kuwa mashirika 6 na shirika moja lilitenganishwa na kuwa mashirika mawili.
Ameongeza lengo kubwa la kuunganisha au kutenganisha mashirika hayo ni kuipunguzia Serikali gharama na kuongeza ufanisi katika utoaji wa huduma kwa wananchi.

Wakati huo huo, amesema kwamba Ofisi ya Msajili wa Hazina, Wizara ya Fedha na Mipango pamoja na ESRF inaendelea kufanya tathmini ya kina kwa mashirika yote ya biashara kwa lengo la kubaini hatua stahiki za kuchukua ili kuboresha utendaji wake kwa ujumla.

Pia amesema Wizara ya Fedha na Ofisi ya Msajili wa Hazina (OMH) zinaratibu zoezi la uhakiki wa mali za umma nchi nzima ambapo mpaka kufikia Juni 30, 2019 idadi ya mali 531 zilikuwa zimetambuliwa na kurejeshwa kwenye mikoa 10 iliyopitiwa.

Amesema kati ya mali zilizorejeshwa kuna majengo (337), viwanja (140), mashamba (10), maghala (41) na mali zingine (3). Aidha, katika mali zilizobainika kuna kampuni mbili Songwe Water Company Limited na Liquid Storage Company Ltd ambazo Serikali inamiliki kwa asilimia 100 na 40 mtawalia na zoezi hili bado linaendelea.
Vilevile, hadi kufikia tarehe 30 Juni, 2019 OMH ilikuwa imerejesha viwanda 31 vilivyothibitika kutofanya kazi na taratibu za kisheria zinaendelea katika hatua mbalimbali.

Amesema wazi kuwa Ofisi ya Msajili wa Hazina inakabiliwa na changamoto ambazo zikipata ufumbuzi inaweza kuboresha zaidi ukusanyaji wa mapato. Kuhusu changamoto amesema kuwa mojawapo ni mfumo hafifu wa TEHAMA wa utoaji taarifa na ufuatiliaji, changamoto za Sheria ya Msajili wa Hazina, ongezeko la mahitaji ya watumishi wenye utaalamu na uzoefu wa kazi, na kukosekana kwa Mfuko wa Fedha za Uwekezaji.

No comments:

Post a Comment

MAONI (COMMENTS)👇

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages