Waziri anayeshughulikia masuala ya kimataifa katika Wizara ya Mambo ya Nje Ya Uganda amesema kwamba nchi yake itachunguza suala la kumpa hifadhi Omar al-Bashir, rais wa Sudan aliyeng'olewa madarakani na ambaye anasakwa na Mahakama ya Kimataifa ya Jinai ICC.
Waziri Henry Oryem Okello ameashiria mchango wa al-Bashir katika mchakato wa mapatano ya amani ya Sudan Kusini a kusisitiza kwamba nchi yake itachunguza suala la kumpa Bashir hifadhi katika ngazi za juu zaidi za uongozi wa nchi hiyo. Huku akisema kuwa Uganda inafuatilia kwa karibu matukio ya Sudan, Waziri Okello amewataka viongozi wapya wa kijeshi wa nchi hiyo kuheshimu matakwa ya Wasudan kwa kukabidhi madaraka kwa serikali ya kiraia.
Kufuatia ghasia za miezi kadhaa iliyopita, Alkhamisi iliyopita jeshi la Sudan lilimpindua Rais Omar al-Bashir na kutwaa madaraka ya nchi hiyo. Mgogoro wa Sudan ulianza tarehe 19 Disemba mwaka uliopita ambapo wananchi waliingia mitaani na kuanza kufanya maaandamano ya kila siku kulalamikia ughali wa maisha na hali mbaya ya uchumi pamoja na ongezeko kubwa la bei ya bidhaa na hasa mkate na mafuta. Mgogoro huo ulichukua mkondo mpya wa kisiasa, kiuchumi na kiusalama baada ya jeshi kuingilia kati na kuanza kuwakandamiza waandamanaji. Vyama vya siasa navyo viliamua kuzidisha mashinikizo kwa kufuatilia matakwa ya wananchi likiwemo suala zima la kutaka wapewe uhuru zaidi wa kisiasa. Maandamano ya aina hiyo ambayo yalitaka Omar al-Bashir aondolewe madarakani yalikuwa hayajawahi kushuhudiwa nchini Sudan katika miongo mitatu ya hivi karibuni.
No comments:
Post a Comment
MAONI (COMMENTS)👇