Mwenyekiti wa Jumuiya ya wazazi Taifa Ndg. Fadhili Maganya amewaasa viongozi wa chama cha mapinduzi (CCM) ngazi za Wilaya pamoja na Mkoa wa Pwani kuhakikisha kwamba wanalivalia njuga suala la kero ya migogogoro ya ardhi sambamba na kusikiliza changamoto mbali mbali zinazowakabili wananchi na kuzitafutia ufumbuzi.
Kauli hiyo ameitoa wakati wa ziara yake ya kikazi yenye lengo la kuweza kukijenga chama pamoja na kuangalia uhai wake pamoja na kuimarisha jumuiya zake, na kuangalia mwenendo mzima wa utekelezaji wa ilani na kukagua na kutembelea baadhi ya miradi mbali mbali ya maendeleo.
Mwenyekiti huyo amebainisha kuwa katika ziara hiyo pia imelenga kukutana na viongozi mbali mbali wa serikali na kupokea taarifa zao zinazohusiana na suala zima la utekelezaji wa kazi zao ambazo wanazifanya katika maeneo yao kwenye nyanja mbali mbali za kimaendeleo.
"Nimeanza ziara yangu ya kikazi katika Wilaya ya Kibaha na lengo kubwa na kwamba ziara hii ni ya kikazi na lengo lake kubwa ni kuangalia uhai wa chama jinsi iliovyo, pamoja na jumuiya zake ikiwa sambamba na kuweza kuangalia na kutembelea miradi mbali mbali ya kimaendeleo na kuzungumza na wanachama," amebainisha Mwenyekiti huyo.
Pia Mwenyekiti huyo amewasihi wanachama na viongozi kuhakikisha kwamba wanaachana kabisa na tabia ya kuwasikiliza baadhi ya wanaharakati ambao wamekuwa wakibeza mambo mbali mbali ambayo yanatekelzwa na serikali ya awamu ya sita na badala yake wajikite zaidi katika kumuunga mkono Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi ambazo anazifanya.
Pia amewahimiza madiwani na viongozi wengine kuhakikisha wanaweka misingi imara ya kusimamia utoaji wa fursa za mikopo ya asilimia 10 ambayo inatolewa na halmashauri kwa lengo la kuwasaidia wajasiriamali waweze kujikwamua kiuchumi na kuondokana na umasikini .
Aidha Mwenyekiti huyo hakusita kumpongeza kwa dhati Mkuu wa Mkoa wa Pwani kwa kuweza kuchapa kazi kwa bidii pamoja na kuendelea kutekeleza ilani kwa vitendo katika suala zima la kusimamia fedha ambazo zimekwenda kutekeleza miradi mbali mbali ya maendeleo pamoja na mkurugenzi mtendaji wa HalmashaurI ya Manispaa ya Kibaha Dkt. Rogers Shemwelekwa.
Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa Pwani AlhajI Abubakari Kunenge akitoa salama zake amesema kwamba Mkoa wa Pwani imeweza kuendelea kutekeleza miradi mbali mbali ya maendeleo ikiwemo sekta ya elimu, afya, umeme, miundombinu ya barabara pamoja na ujenzi wa viwanda.
Naye Mjumbe wa halmashauri kuu ya chama cha mapinduzi (CCM) Taifa Hamoud Jumaa amesema kwamba lengo lake kubwa ni kuendelea kushirikiana bega kwa bega katika kuhakikisha chama cha serikali kinaendelea kuwa na mahusiano mazuri ikiwemo sambamba na kutekeleza ilani ya chama.
Mwenyekiti wa Jumuiya ya wazazi Mkoa wa Pwani Jackson Kituka amebainisha kuwa ni jukumu la wanachama kuendelea na kuweza kushikamana katika kukijenga chama ikiwa sambamba na kuiimarisha zaidi kwa vitendo jumuiya zake zote.
Mwenyekiti wa chama cha mapinduzi(CCM) Wilaya ya Kibaha mjini Mwalimu Mwajuma Nyamka amempongeza kwa dhati Mwenyekiti huyo kwa kuamua kufanya ziara ambayo itaweza kuleta uhai wa chama pamoja na kuimarisha jumuiya zake ikiwa pamoja na kutembelea miradi mbali mbali ya maendeleo.
Mbunge wa Jimbo la Kibaha mjini Silvestry Koka amempongeza Mwenyekiti wa jumuiya ya wazazi Taifa kwa kutekeleza ilani ya chama kwa vitendo ikiwa sambamba na kuweza kuona umuhimu wa kufanya ziara yake ya kikazi ambayo itaweza kuleta matokeo chanya katika suala zima la kukiimarisha chama pamoja na jumuiya zake kwa pamoja.
Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wazazi Taifa ameanza ziara yake rasmi ya kikazi katika Mkoa wa Pwani ambapo ameanza katika Wilaya ya Kibaha ambapo ameweza kutembelea baadhi ya miradi ya maendeleo katika Zahanati ya Kilimahewa iliyopo kata ya Tangini, Kituo cha afya mlandizi pamoja na kutembelea mradi wa ujenzi wa stendi ya mabasi Mlandizi.
No comments:
Post a Comment
Tupia Comments👇