Mbunge wa Jimbo la Malinyi, Mhe. Dkt. Mecktridis Mdaku amewataka viongozi wa Chama cha Mapinduzi (CCM)
kutanguliza maslahi ya wananchi wa Jimbo la Malinyi kwa kuwasikiliza changamoto zao, na kuweka mikakati ya kuitatua, kuwapa nafasi ya kutoa maoni juu ya mipango mikakati ya kuboresha hali za uchumi wa kila mmoja kwa pamoja.
Amesisitiza kuwa uimara wa Chama hautokani na idadi ya wanachama pekee bali unajengwa na Viongozi wanaowajibika kwa wanachama wanaoshiriki kikamilifu katika shughuli zote za maendeleo.
Kauli hiyo ameitoa wakati mikutano mikuu ya Chama katika Kata za Malinyi na Biro, ambapo pamoja na kujadili mikakati ya kuimarisha chama, Viongozi walipanga hatua za kuongeza ushiriki wa wananchi katika shughuli za maendeleo na kuinua uchumi wa jamii.
Mhe. Dkt. Mdaku amesema wakati umefika kwa kila kiongozi wa CCM kuhakikisha chama kinaendelea kuwa hai kuanzia ngazi ya shina hadi Wilaya, kwa kuhamasisha ujenzi wa ofisi za chama katika Kata, kufanya vikao kwa mujibu wa Katiba na Kanuni za CCM, pamoja na kuimarisha mshikamano miongoni mwa Viongozi na wanachama.
Amesisitiza kuwa wanachama wanapaswa kushiriki kikamilifu katika shughuli za chama badala ya kubaki wanachama wa majina pekee, akieleza kuwa uhai wa chama ndio msingi wa utekelezaji wa Ilani ya CCM na maendeleo ya wananchi.
Mbunge amewakumbusha viongozi kutambua kuwa wao ni daraja kati ya wananchi na Serikali, hivyo wana wajibu wa kupokea, kufuatilia na kushughulikia kero za wananchi, kwa kushirikiana na Mamlaka husika.
Amesema hatua hiyo itaendelea kuimarisha imani ya wananchi kwa CCM na kuongeza kasi ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo katika Jimbo la Malinyi.
Akihitimisha ziara yake katika Kata za Malinyi na Biro, Mhe. Dkt. Mdaku aliwahimiza Viongozi na wanachama kuendelea kutekeleza maazimio ya chama kwa vitendo, kudumisha mshikamano na kutumia fursa zilizopo kuinua uchumi wa wananchi, huku wajumbe wakiahidi kuyafanyia kazi maelekezo yote yaliyotolewa kwa maslahi ya chama na maendeleo.
No comments:
Post a Comment
Tupia Comments👇