RAIS Samia Suluhu Hassan ametoa maelekezo kwa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo na Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) kuwalea vizuri na kuwapa fursa, waandishi wa habari za mitandaoni na blogs ili waweze kufanya kazi zao vizuri.
Hayo yameelezwa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, na Msemaji Mkuu wa Serikali, Bw. Gerson Msigwa, alipokuwa akifunga kikao cha pamoja cha wanachama wa Mtandao wa Mabloga Tanzania (TBN) na Jukwaa la Mitandao Tanzania (JUMIKITA) kilichoandaliwa na Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) jijini Dar Es Salaam Desemba 18,2025
"Mheshimiwa Rais amewapongeza sana na anatambua kazi zenu nzuri. Ni maelekezo yake kwamba sisi Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo kupitia Idara ya Habari MAELEZO na Wizara ya Mawasiliano na Teknolojia ya Habari kupitia TCRA. Kuna maelekezo kutoka kwa Rais Samia Suluhu Hassani kwamba waandishi wa habari wa mitandaoni na blogs walelewe vizuri, wapewe fursa Ili wafanye kazi zao vizuri."
"Hayo kwetu ni maelekezo na kwa utaratibu wa kiserikali ni kama jeshini ukishapewa maelekezo hakuna mjadala kinachofuata ni utekelezaji, kwa hiyo tupo hapa na mzee Jabiri tunatekeleza maagizo ya Mheshimiwa Rais,"amesema Msigwa huku akipigiwa makofi.
Msigwa amesema mwelekeo huo unaendana na falsafa ya Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, ambayo inalenga kushirikiana na wadau mbalimbali kwa manufaa ya taifa.
Aliitaja Tanzania Bloggers Network (TBN) na Jukwaa la Mitandao Tanzania (JUMIKITA) kuwa ni wadau wakubwa wa serikali katika tasnia ya habari, akisisitiza kuwa mchango wao ni muhimu katika kusambaza taarifa na kujenga mawasiliano kati ya serikali na wananchi.
“Serikali imewaamini waandishi wa mitandaoni, sasa nanyi muendelee kuonesha imani kwa serikali. Ushirikiano wetu umeendelea kuimarika na changamoto zinazojitokeza tunazitatua kwa pamoja,” amesema Msigwa.


No comments:
Post a Comment
Tupia Comments👇