LATEST HEADLINES👉

Your Ad Spot

Jul 21, 2024

MJUMBE WA KAMATI KUU PINDA AWATAKA WAGOMBEA CCM KUJIEPUSHA NA VINENO VYA UCHOCHEZI

Na Munir Shemweta, Mlele

Mjumbe wa Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Taifa ya Chama cha Mapinduzi (CCM), Waziri Mkuu mstaafu Mizengo Pinda, amewataka wanachama CCM wanaotaka kugombea nafasi yoyote kujiepusha na maneno ya uchochezi yanayoweza kuharibu mahusiano baina yao.

 

Pinda amesema hayo  akizungumza na viongozi mbalimbali wa CCM wakiwemo madiwani, viongozi wa Kata na Wazee katika Halmashauri ya Mpimbwe wilaya ya Mlele mkoa wa Katavi, jana, Julai 20, 2024.

 

Amesema, yeyote anayetaka kugombea nafasi ya uongozi ni vizuri akawa mwangalifu na maneno ya uchochezi aliyoyaeleza kuwa, wakati mwingine yanaweza kumletea tabu wakati haipo.

 

"Chonde chonde sana usije ukaingia kwenye ugonjwa, unakaa unakuzungusha kichwa kwa sababu kuna mtu kaja kukuambia eeh kuma mtu fulani anakusema vibaya, sasa hujathibitisha unaanza kutembea nayo na wewe, usiende hivyo kwenye siasa hatuendi hivyo" amesema Mizengo Pinda

 

Amewataka wanapopelekewa maneno kuyapokea na kutulia huku wakijaribu kuyachunguza ili kuona ukweli au uongo kwa kile wanachoambiwa na kuweka wazi kuwa, wengi huponzwa na maneno ambapo amesisitiza, wana CCM kujaribu kupunguza maneno ya uchochezi yatakayosababisha kukwaruzana pasipo sababu ya msingi.

 

Kwa upande wake mbunge wa jimbo la Kavuu ambaye ni Naibu Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Geophrey Pinda ameeleza kuwa, hali ya kiasiasa ndani ya jimbo lake iko shwari na amekuwa akifanya vikao vya mara kwa mara kwa wananchi wa rika zote kupitia kata za jimbo hilo.

 

Hata hivyo, Mbunge huyo ameweka wazi kuwa, wakati mwingine kwa namna moja ama nyingine amashindwa kumfikia kila mwananchi kwenye jimbo hilo kutokana na idadi kubwa ya wakazi wake aliyoieleza kwamba imekuwa ikiongezeka siku hadi siku.

 

Amebainisha kuwa, kupitia wizara yake ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi wako mbioni  kuweka mipango ya  matumizi bora ya ardhi kwa kila kijiji ila  wanachi wapate hati milki za ardhi na kuweza kuzitumia kwa matumizi mbalimbali ikiwemo kuchukulia mikopo benki. 

Waziri Mkuu Mstaafu na Mjumbe wa Kamati Kuu ya Chama cha Mapinduzi Taifa Mhe. Mizengo Pinda akisalimiana na Mbunge wa jimbo la Kavuu katika halmashauri ya Mpimbwe mkoa wa Katavi Mhe. Geophrey Pinda alipokwenda kuzungumza na viongozi mbalimbali wa CCM jimboni humo tarehe 20 Julai 2024


Washiriki wakisimama kumlaki Waziri Mkuu Mstaafu na Mjumbe wa Kamati Kuu ya Chama cha Mapinduzi Taifa Mhe. Mizengo Pinda.

Washiriki wakiwa wamekiti tayari kumsikiliza Waziri Mkuu Mstaafu na Mjumbe wa Kamati Kuu ya Chama cha Mapinduzi Taifa Mhe. Mizengo Pinda.


Waziri Mkuu Mstaafu na Mjumbe wa Kamati Kuu ya Chama cha Mapinduzi Taifa Mhe. Mizengo Pinda akizungunza katika mkutano huo.


Mbunge wa Jimbo la Kavuu na Naibu Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Geophrey Pinda akizungumza wakati wa mkutano huo.


No comments:

Post a Comment

MAONI (COMMENTS)👇

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages