LATEST HEADLINES👉

Your Ad Spot

May 29, 2024

Dk Samia anaposubiriwa kumaliza mizozo Afrika

 

Dk Samia anaposubiriwa kumaliza mizozo Afrika

 

Ibrahim Bakari, Official CCM Blog

Mwaka 1961 baada ya Tanganyika kupata uhuru, Rais wa kwanza wa Tanganyika huru, Mwalimu Julius Nyerere aliwahi kusema, Tanzania haiwezi kuwa huru mpaka Afrika yote iwe huru.

Huyo alikuwa hayati Baba wa Taifa. Aliangalia mbali kwamba Watanzania hawawezi kujidai, hawawezi kula matunda ya uhuru kwa raha zao ilhali nyumba ya jirani  mitutu inalia kila kukicha.

Hakuishia kwenye matamshi ya jukwaani, alivaa viatu akaingia uwanjani.

Kutokana na shauku yake kutaka kuona Afrika inakuwa huru, aliteuliwa kuwa Mwenyekiti wa Kamati ya Ukombozi Kusini mwa Afrika.

Wakati huo lengo kuu ni kuhakikisha  mataifa ya Afrika yanapata uhuru ikiwemo;  Angola, Afrika Kusini, Zimbabwe, Namibia, Msumbiji na mengine yanakuwa huru kutoka mikononi mwa walowezi wachache.

Mapambano yakatimia. Afrika imekuwa huru.

Pamoja na hayo, ndani ya Afrika kumekuwa  na chokochoko za makundi ya waasi ambayo hadi leo yanaisumbua Afrika.

Itakumbukwa kulikuwa na watu kama; Jonas Savimbi ambaye aliuawa Februari 22, 2002 na vikosi vya Serikali ya Angola.

Kwa Savimbi, ilikuwa kila kukicha mitutu inasikika, lakini sasa Angola iko vizuri tofauti na wakati huo.

Mfano mwingine ni Taifa la Msumbiji likiongozwa na Chama cha Frelimo, lakini bado ilisumbuliwa na Waasi wa Renamo walioongozwa na Alphonso Dhlakama ambaye naye alifariki Mei 4, 2018.

Kufariki ama kuuawa kwa viongozi wa waasi, kwa njia moja na nyingine imesaidia angalau kutuliza mfululizo wa milio ya risasi na mabomu.

Hawa na wengine, ni mifano ya wavuruga  amani ya Afrika kwa uchu wa madaraka. Wengi wa waasi waliishia kuuawa.

Pamoja na hayo, waasi katika baadhi ya mataifa ya Afrika, bado ni tatizo, mfano mzuri inaonekana nchini Nigeria, makundi ya Boko Haram, nchini DR Congo makundi ya M23 yanavyoendelea kusumbua.

Tatizo lingine ambalo bado linasumbua Afrika ni mapinduzi ya kijeshi, ambayo mara zote hufanyika kwa kuondoa utawala halali na jeshi kuchukua madaraka kwa sababu mbalimbali na baadaye kukosekana amani na utulivu kutokana na mapinduzi hayo.

Kwa sasa, Baraza la Amani na Usalama la Umoja wa Afrika, AU lina kazi moja ya kumaliza mizozo ya mataifa kama ilivyo DR Congo uliodumu kwa zaidi ya nusu karne sasa, ambayo imesababisha hadi uingiliaji kati wa majeshi ya kigeni.

Itakumbukwa, Aprili 19, 2024, ujumbe wa amani wa Umoja wa Mataifa katika DR Congo (MONUSCO) ulikabidhi kambi ya Bunyakiri kwa majeshi ya Serikali (FARDC).

Kaimu kamanda wa kikosi cha MONUSCO, Meja Jenerali Khar Diouf, amesema hatua hiyo ni nzuri kwani na ni mwanzo mzuri wa kudhoofisha nguvu za M23 na tayari Baraza la Amani na Usalama chini ya Mwenyekiti wake; Rais Samia Suluhu wa Tanzania, limesema halitaki kusikia milio ya mitutu ikitamalaki.

Bunyakiri ni kambi ya pili ambayo MONUSCO iliikomboa nchini humo, baada ya kujiondoa, kwa wanajeshi wa uasi waliokuwa wamekaa katika kituo cha Kamanyola hadi Februari 28, 2000 walipoondoka katika jimbo hilo la mashariki mwa DRC la Kivu Kusini.

Makabidhiano haya mawili ya kambi, kipekee  yanaashiria kuanza kwa operesheni ambayo italazimu kuondoka kwa walinda amani wote wa UN wapatao 13,500, kabla ya Desemba 31, 2024. Wote hao chini ya Umoja wa Mataifa waliokuwepo nchini humo tangu mwaka 1999.

Mataifa mengine yenye mizozo ya kisiasa ni pamoja na yale ya pembe ya Afrika, ikiwemo Somalia ambayo hata hivyo inaelezwa mizozo imemalizwa na baraza hilo.

Aidha mpaka sasa, inaelezwa mizozo imetatuliwa katika mataifa ya Comoro, Sudan, Somalia na Ethiopia pamoja na baadhi ya mataifa ya Afrika Magharibi ikiwemo Mali.

Akizungumza katika maadhimisho ya Baraza hilo tangu lianzishwe Mei 25, 2004, Mwenyekiti wake, Dk. Samia amesema Baraza  limekuwa na nafasi muhimu katika kukuza amani, usalama na utulivu wa Afrika.

Amesema Tanzania itahakikisha Baraza la Amani na Usalama wa Afrika, unakuwa madhubuti ili kufikia malengo yaliyokusudiwa katika kutoa hamasa ya  kulinda amani na kuhakikisha ustawi wa watu.

Dk. Samia amesema ni muhimu kwa baraza kuwashirikisha vijana na wanawake katika kuimarisha na kuleta maendeleo ya kiusalama ili kuleta mabadiliko chanya pamoja na maendeleo kijamii na kiuchumi.

Amesema jitihada za pamoja ni muhimu katika kuimarisha usalama, hivyo ni muhimu kwa wanachama na baraza ambao ni mataifa ya Afrika  kwa ujumla kuongeza ushirikiano na wadau wa makundi mbalimbali.

“Leo ni miaka 20 tangu kuanzishwa kwa Baraza hili lina jukumu la kuzuia, kudhibiti na kutatua migogoro katika bara letu la Afrika hivyo niwapongeze viongozi wote kwa hatua tuliyofikia,” amesema na kuzipongeza nchi wanachama wapya waliojiunga na baraza hilo kuanzia Aprili, mwaka huu.

Dk Samia amewaahidi ushirikiano katika mambo yote ambapo nchi wanachama wa AU 53 kati ya 55 zimeridhia itifaki ya uanzishwaji wa baraza hilo ambalo bado linaendelea na jitihada za kutokomeza mitutu Afrika.

Mbali na mitutu, kubwa ni kuimarisha mifumo ya utambuzi wa migogoro, kuzuia masula ya ugaidi na kuimarisha demokrasia na utawala bora.

Dk. Samia amesema baraza la Amani na usalama Afrika limetembelea na kufanya ziara katika nchi ambazo zina migogoro na kuelewa vyema changamoto za nchi hizo, hivyo limeonesha mshikamano na wahusika wa migogoro kwa nia ya kuzuia na kuitokomeza kabisa.

 

Akizungumzia mafanikio Rais Dk. Samia ameainisha mafanikio ya baraza kuwa ni kuanzishwa kwa majadiliano baada ya vita, kukabiliana na migogoro na ugaidi, kujidhatiti kusimamia misingi ya haki za binadamu na ushirikiano wa taasisi.

Amesema ili kuimarisha amani na usalama Afrika, baraza linapaswa kuongeza uwezo wa kuzuia migogoro kwa kutumia nyenzo zilizopo, kuzuia migogoro isiwe endelevu kupitia mifumo ya utambuzi wa mapema, kuwepo kwa majadiliano na kuimarisha michakato ya maridhiano.

“Ipo mifumo ambayo haitumiki vizuri hivyo ni muhimu kuimarisha amani kutumia jeshi la Afrika, utekelezaji madhubuti wa nyenzo hii itasaidia kudhibiti mitutu,” amesema.

Ameainisha baadhi ya changamoto zinazoikabili baraza hilo kuwa ni uhitaji wa haraka wa kufanya tathmini ya uhuru kwa bara hilo, mabadiliko yasiyozingatia Katiba kwa sababu hayavumiliki.

Kwa hali hiyo, ni busara za Mwenyekiti zinasubiriwa kumaliza mizozo ndani ya Afrika kupitia vikao maalumu.

Kimsingi, kuundwa kwa baraza hilo, ni wazi Waafrika wanataka kumaliza matatizo yao kwa maana ya kwamba matatizo ya Afrika yatamalizwa na Waafrika wenyewe.


No comments:

Post a Comment

MAONI (COMMENTS)👇

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages