Katibu wa CWT Wilaya ya Igunga mkoani Tabora, Saphia Maziku |
Chama cha Walimu (CWT) Wilaya ya Igunga Mkoani Tabora, kimesema juhudi za Rais wa awamu ya sita wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, zinatoa muelekeo chanya wa ukuaji wa sekta ya elimu nchini.
Hayo yameelezwa na Katibu wa CWT Wilayani Igunga ,Sophia Maziku, alipozungumza na mwandishi wetu ofisini kwake mjini Igunga mapema leo.
Maziku amesema kuwa, uwekezaji mkubwa unaofanywa na serikali ya awamu ya sita katika sekta ya Elimu nchini unaleta tija na ufanisi kwenye ukuaji wa sekta hiyo muhimu kwa maendeleo ya Taifa.
"Kwa niaba ya Walimu wilayani Igunga kwanza tunampongeza sana Rais Samia Suluhu Hassan kwa jinsi ambavyo Serikali yake inavyotatua changamoto za elimu kwa kujenga madarasa, nyumba za Walimu sambamba na kuboresha maslahi ya walimu kote nchini." alisema Maziku.
Aliongeza kusema kuwa, Hatua ya Serikali kulipa malimbikizo ya madeni ya Walimu, kupandisha madaraja pamoja na kuanza kuorejesha utaratibu wa nyongeza ya mishahara kila mwaka imeongeza ari na mori ya Walimu kufanya kazi kwa juhudi na maarifa.
" Ahadi ya Rais Dkt Samia siku ya maadhimisho ya siku ya wafanyakazi duniani Mei Mosi, ya kwamba wafanyakazi kote nchini mambo yao yatakuwa moto kuanzia bajeti ya 2023/2024 itakayo anza kutekelezwa mwezi Julai mwaka huu imewapa tabasamu wafanyakazi wote hususani walimu wa wilaya ya Igunga," alisema Maziku.
Katika hatua nyingine CWT wilayani Igunga imeahidi kuwa bega kwa bega na Rais Samia ambapo wamesema kuwa watamuunga mkono kwa hali na mali ili aweze kumaliza vipindi vyake viwili vya Uongozi.
"CWT Igunga tunamuhakikishia Rais Samia kuwa tupo naye bega kwa bega, tutapambana kumsaidia kwa lolote huku tukiendelea kubaki kuwa wafuasi watiifu kwa serikali yake." alisema Maziku.
No comments:
Post a Comment
MAONI (COMMENTS)👇