LATEST HEADLINES👉

Your Ad Spot

Jan 12, 2023

SHAKA: CCM INAJIVUNIA MABADILIKO YALIYOFIKIWA KATIKA MIAKA 59 YA MAPINDUZI AMBAYO YAMEWAFANYA WANANCHI KUJIAMINI NA KUJITEGEMEA KIMAENDELEO

Na Mwandishi  Maalum, Z'bar.

Chama Cha Mapinduzi (CCM) kinajivunia mabadiliko makubwa yaliyofikiwa Zanzibar katika kipindi cha miaka 59 ya Mapinduzi Matukufu ambayo yamewafanya Wananchi kujiamini na kujiitegemea kimaendeleo.


Hayo yamesemwa leo mjini Zanzibar na Katibu wa Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC), Itikadi na Uenezi Shaka Hamdu Shaka katika mahojiano maalum, kuhusu Mapinduzi hayo yaliyofanyika Januari 12, 1964.


"Zanzibar imepiga hatua kubwa sana na CCM inatoa pongezi za dhati kwa kazi kubwa iliyokwishafanywa na inayoendelea kufanywa na Serikali ya awamu ya nane chini ya Rais Dk. Hussein Ali Mwinyi, ikiendelea  kuunga mkono juhudi za kukomesha ukandamizaji wa haki , ubaguzi, dhulma na  manyanyaso.


 Katika kipindi cha miaka 59 ya Mapinduzi matukufu licha ya kuleta ukombozi kamili lakini  pia yamewafanya  wananachi kuwa na fikra huru  na kujitawala" alisema Shaka na kuongeza;


"Kabla ya mapinduzi lipo tabaka lilokandamiza, kubagua na kuwapuuza wengine huku wananachi wakikosa haki za msingi na kutotumia fursa za kiuchumi sawa na utu wao  kutothaminiwa, na kupuuzwa.


Mapinduzi ya mwaka 1964 ni ushahidi kuwa Zanzibar ilikuwa na watu waliokoseshwa elimu bora, kutomiliki uchumi, ardhi, kukosa makaazi bora na kunyimwa huduma za jamii".


Alisema, Serikali zote (Serikali ya Mapinduzi Zanzibar na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania) zimetimiza wajibu wa kusimamia maendeleo. Rais Dk. Samia Suluhu Hassan na Rais Dk. Mwinyi baada ya miaka 59 wametafsiri mapinduzi ya ukombozi kuwa Mapinduzi ya kiuchumi. Maendeleo  yanayoonekana  sasa hayakuwepo miaka 200 ya utawala wa kikoloni,


Alisema, kazi kubwa iliyofanywa na Chama cha ASP ilikuwa kuhakikisha utawala wa ukandamizaji, uonevu na ubaguzi wa huduma za jamii unakomeshwa katika visiwa vya Unguja na Pemba kwa sera ya mapinduzi ya ukombozi na kazi iliyobaki ni kujenga uchumi na maendeleo.


"Ni vyema kwa watendaji  waliopewa dhamana katika Serikali na taasisi za umma kuhakikisha  wanatimiza wajibu wao kwa kumsaidia Rais Dk. Mwinyi ili akamilikshe kazi ya kutekeleza mapinduzi ya kiuchumi na kuongeza Kasi ya kuleta maendeleo. 


Kazi ya kumwondoa mkoloni aliyetawala kwa ubaguzi na ukandamizaji imemalizika. Kazi iliyobaki ni kuongoza kwa haki, umoja na maendeleo. Kukumbuka madhila yaliyokuwepo kabla ya mapinduzi kunatupa ari ya kufikia mabadiliko tuanayoyataka,"  alisema Shaka.


Alisema, baada  ya kufanikisha mapinduzi ya mwaka 1964 na utawala kushikwa na ASP, Rais wa kwanza wa Zanzibar hayati Mzee Abeid Amani Karume alianza utekelezaji  wa sera za maendeleo ikiwemo kutolewa bure kwa huduma za msingi.


"Elimu imetolewa bure, maji  safi na matibabu, serikali ikaweka viwango vya mishahara minono kwa mujibu wa ajira ya kila mfanyakazi, yamejengwa makaazi ya kisasa na sasa kazi hiyo inaendelezwa na  serikali ya Rais Dk. Mwinyi.


"Ni waombe watanzania wenzangu hasa vijana kutobabaishwa na porojo za baadhi ya wapinga maendeleo na mapinduzi matukufu ya 1964 ambao wamekuwa wapotoshaji wa ukweli kwa kudai serikali za CCM hazijafanya lolote tangu mwaka 1964 wakati asiliamia 98 ya maendeleo yaliyofanyika nchini yamepatikana katika utawala wa Chama Cha Mapinduzi" alihitimisha Shaka mahojiano hayo.

Katibu wa Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) Shaka Hamdu Shaka, akizungumza katika Studio za Wasafi TV mjini Zanzibar, leo.

No comments:

Post a Comment

MAONI (COMMENTS)👇

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages