LATEST HEADLINES👉

Your Ad Spot

Jan 2, 2023

MJUE MWAFRIKA ANAYEKISIWA KUWA MREFU ZAIDI DUNIANI

 

TH

Niliposikia fununu za mshindani mpya wa mwanaume mrefu zaidi duniani kaskazini mwa Ghana, niliamua kujua kama ni kweli. Tatizo pekee? Kumpima.

Hospitali ya eneo la kaskazini mwa Ghana ilimwambia Sulemana Abdul Samed mwenye umri wa miaka 29 wakati wa uchunguzi wake wa hivi majuzi kwamba alikuwa amefikia urefu wa 9 ft 6in (2.89m).

Hii ingemfanya kuwa mtu mrefu zaidi duniani, lakini kulikuwa na  changamoto - kliniki ya vijijini haikuweza kuwa na uhakika wa urefu wake kwa sababu haikuwa na zana sahihi za kupimia.

Alipogunduliwa na ugonjwa wa gigantism(Unaomfanya kua kwa kiasi kikubwa) miaka michache iliyopita, kijana huyo alikuwa akihudhuria miadi ya kila mwezi ili kukabiliana na matatizo ya kuishi kama jitu alipoombwa kusimama moja kwa moja dhidi ya fimbo ya kupimia.

Muuguzi aliyeshtuka alimwambia: "Umekua mrefu kuliko mizani."

Aliyejulikana zaidi na kila mtu kwa jina lake la utani Awuche, linalomaanisha "Twende" kwa Kihausa, alifurahishwa na tamasha aliyokuwa akisababisha.

Hakushangaa kusikia yeye ni mrefu zaidi, ikizingatiwa kuwa hajawahi kuacha kukua - lakini ilisababisha mshangao kwa wafanyikazi, ambao hawakuwa wamejiandaa kwa hali kama hiyo.

Muuguzi wa zamu akamwita mwenzake, ambaye naye alimwita mwingine kuomba msaada. Muda si muda kundi la wauguzi na wasaidizi wa afya walikusanyika ili kutatua kitendawili cha kuamua urefu wake.

Mmoja alipendekeza watafute nguzo na kuitumia kama nyongeza juu ya fimbo yao ili kupima urefu wake - na hivi ndivyo walivyofikia makadirio yao.

 

  'Bado anakua'

Nilipokutana na Awuche miezi michache iliyopita nilipokuwa nikisafiri kaskazini mwa Ghana, ambapo umaarufu wake ulikuwa umeenea katika nyanda za eneo hilo, sikuwa na kanda ya kunipimia ili kuthibitisha urefu wake.

Kwa hivyo ili kusuluhisha suala hilo - na nikiwa na mkanda wa kupimia futi 16 - nilirudi katika kijiji cha Gambaga wiki iliyopita.

TH

Mpango ulikuwa ni kumfanya aegemee ukuta, aweke alama kwenye utosi wa kichwa chake kisha atambue urefu wake kwa kutumia mkanda wa kupimia.

"Jinsi wanavyonipima, siwezi kusema kila kitu ni sawa," Awuche alikiri - akifurahishwa na mpango wangu wa kupata kipimo kamili.

Alionekana kuwa mrefu kuliko nyumba nyingi za jirani yake, lakini baada ya utafutaji mzuri tukapata jengo linalofaa na ukuta wa kutosha. 

Alivua viatu vyake – pati pati  kubwa zilizotengenezwa maalum kutoka kwa matairi ya gari na akapigilia misumari pamoja na mfanyakazi wa eneo hilo kwa kuwa ameshindwa kupata viatu vya kumtosha

Mmoja wa majirani zake alipanda juu ya stuli ya  mbao ili kufikia urefu wa Awuche ili aweze kuweka alama kwenye ukuta kwa kipande cha makaa.

Baada ya kuthibitisha mstari, tulinyoosha utepe wa kupimia kwa uthabiti kutoka kwa mstari uliowekwa alama hadi chini huku Awuche akitazama kwa hamu.










"Awuche, tepi ya kupimia inasoma 7ft 4in," nilisema.

Akiwa na  tabasamu lake lisilo na kifani, alijibu: "Wow, kwa hivyo inamaanisha nini?"

"Kweli, mtu mrefu zaidi aliye hai ana urefu wa futi 8 na inchi 2.8, ana urefu wa futi moja kuliko wewe."

Nilikuwa nikimrejelea Sultan Kösen mwenye umri wa miaka 40, ambaye anaishi Uturuki na anashikilia Rekodi ya Dunia ya Guinness .

"Bado ninakua mrefu. Nani anajua, labda siku moja naweza kufikia urefu huo pia," Awuche alisema - bila kukerwa hata kidogo na tofauti ya takwimu aliyopewa na hospitali.

Ulimi unaokua

Ongezeko hili la urefu lilianza kuonekana alipokuwa na umri wa miaka 22 na akiishi katika mji mkuu, Accra.

Awuche alikuwa amehamia huko kujaribu bahati yake katika jiji, ambapo mmoja wa ndugu zake aliishi, baada ya kumaliza shule ya upili.

Alikuwa akifanya kazi kwenye bucha, akiweka akiba ya  pesa za kusoma katika shule ya udereva.

Lakini aliamka asubuhi moja akiwa amechanganyikiwa: "Niligundua ulimi wangu ulikuwa umepanuka mdomoni mwangu kiasi kwamba sikuweza kupumua [vizuri]," anasimulia.

Alitembelea duka la dawa la mahali hapo kupata dawa, hata hivyo siku kadhaa baadaye aligundua kuwa kila sehemu nyingine ya mwili wake ilikuwa imeanza kuongezeka ukubwa.

Wakati familia na marafiki kutoka kijijini kwake walipotembelea jiji hilo, wote walisema juu ya kasi ya ukuaji wake na ilikuwa wakati huu aligundua kuwa polepole alikuwa akigeuka kuwa jitu.

Alianza kuwa juu ya kila mtu - na alitafuta msaada wa matibabu kwani ukuaji ulileta shida zingine.

Amebaki na mgongo uliopinda isivyo kawaida, mojawapo ya dalili kuu za hali yake, ugonjwa wa Marfan, ugonjwa wa maumbile unaoathiri tishu-unganishi za mwili.

Inasababisha miguu mirefu isiyo ya kawaida.

Matatizo makubwa zaidi yanahusisha kasoro za moyo.

Madaktari wanasema anahitaji kufanyiwa upasuaji katika ubongo wake ili kuzuia ukuaji huo.



Lakini bima ya afya ya umma ya Ghana haiwezi kulipia hili, ikigharamia  tu matibabu ya kimsingiKwa kila ziara ya hospitali lazima bado ataongeza takriban $50 (£40).

Matatizo yake ya kiafya hatimaye yalimlazimu kurejea kijijini kwao miaka sita iliyopita na kuachana na ndoto zake za kuwa dereva.

"Nilikuwa napanga kwenda shule ya udereva, lakini hata ninaporudisha kiti nyuma, siwezi kushikilia usukani... siwezi kunyoosha mguu wangu kwa sababu goti langu litagonga gurudumu."

Sasa anaishi na kaka yake - na anajikimu kimaisha kwa  biashara ndogo ya kuuza masalio ya simu za rununu .

Urefu wake pia umepunguza maisha yake ya kijamii.

"Nilikuwa nikicheza soka kama vijana wengine wote, nilikuwa mwanariadha lakini sasa siwezi hata kutembea umbali mfupi," alieleza.

 

Mtu Mashuhuri

Lakini Awuche haruhusu matatizo yake yamwangushe. Amejawa uchangamfu  huku umbo lake jembamba likipita katika njia zenye vumbi za kijijini - akitabasamu huku watu wakimuita.

Yeye ni  mtu Mashuhuri wa hapa

Kundi la wazee walioketi karibu na banda wanasemezena naye, watoto wanampungia mkono, baadhi ya wanawake wanakuja kwa ajili ya kumkumbatia na kushiriki naye utani.

Baadhi ya watu wanataka kupiga naye picha za selfie - hata watu wasiowajua wanakuja kuuliza kama yeye ndiye jitu waliloona kwenye mitandao ya kijamii.

"Kwa kawaida nitasema: 'Ndiyo njoo karibu' - tunasimama na kupiga picha nzuri," Awuche anasema.

Anaishukuru sana familia yake kwa msaada wao, akisema kwamba hajui  ndugu zake wengine, wakiwemo kaka  zake watatu, ambao wanaonyesha dalili zozote za kuwa na hali yake.

"Hakuna hata mmoja wao ni mrefu, mimi ndiye mtu mrefu zaidi."

Angependa kuola na kupata watoto siku moja lakini anataka kwanza kuelekeza nguvu zake katika kutatua afya yake.

Kipaumbele chake cha kwanza ni kujaribu kutafuta pesa kwa upasuaji wa plastiki ili kukabiliana na malalamiko makubwa ya ngozi kwenye mguu mmoja, kifundo cha mguu unaosababishwa na ukuaji wa ziada wa kiungo.

Lakini akitazama vidole vyake vilivyofungwa bandeji, Awuche anakataa kukatishwa tamaa na hali yake mbaya.

"Hivyo ndivyo Mwenyezi Mungu alivyonichagulia, niko sawa. Sina tatizo na jinsi Mungu alivyoniumba."

No comments:

Post a Comment

MAONI (COMMENTS)👇

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages