LATEST HEADLINES👉

Your Ad Spot

Aug 18, 2022

NAIBU WAZIRI WA MADINI ATATUA CHANGAMOTO UZALISHAJI GRAPHITE RUANGWA



 

*Atoa ahadi kwa Lindi Jumbo Ltd kuwakutanisha na mabenki

*Aweka msisitizo kushiriki Sensa ya Watu na Makazi

Na Mwandishi wetu,Lindi

NAIBU Waziri wa Madini Dkt. Steven Kiruswa ameahidi kuikutanisha Kampuni ya Lindi Jumbo Limited inayotarajiwa kuanza uchimbaji wa madini ya Kinywe (Graphite) hivi karibuni na taasisi za fedha kwa lengo la kupatiwa mkopo ili ianze uzalishaji wa madini hayo kwa wakati.

Dkt. Kiruswa ametoa ahadi hiyo baada ya kutembelea eneo la kijiji cha Matambarale panapo jengwa mgodi wa uchimbaji madini hayo katika wilaya ya Ruangwa mkoani Lindi.

Dkt. Kiruswa amesema, Wizara ya Madini imeingia mkataba na mabenki mbalimbali kwa lengo la kutoa mikopo kwa wachimbaji na wafanyabiashara ya madini ambapo ameahidi kuikutanisha Kampuni hiyo na mabenki.

"Mhe. Rais wetu Mama Samia Suluhu Hassan ametuagiza sisi Wizara ya Madini kuwalea na kuwaongoza wachimbaji wa madini ili muweze kufanya shughuli zenu kwa tija, hivyo wiki hii nitazungumza na mabenki ili waone jinsi gani wataweza kuwapatia mkopo muanze uzalishaji wa madini haya muhimu,"  amesema Dkt. Kiruswa.

Aidha, Dkt. Kiruswa amesema kuwa, Wizara ya Madini imefungamana na sekta nyingine ambapo ameahidi kukutana na Wizara ya Maji, Nishati na Miundombinu kwa lengo la kutafuta suluhisho la upatikanaji wa maji, umeme na barabara katika maeneo yanayotarajiwa kuanza uzalishaji wa madini ya Kinywe (Graphite).

Pamoja na mambo mengine, Dkt. Kiruswa amesema lengo la ziara yake hiyo ni kutaka kujua maendeleo ya Sekta ya Madini katika mkoa wa Lindi na kujua changamoto zinazoikabili sekta hiyo mkoani humo.

Pia, Dkt. Kiruswa ametembelea eneo linalotarajiwa kujengwa mgodi wa kuchimba madini ya Kinywe na kiwanda cha betri cha Uranex kilichopo wilayani Ruangwa ambapo amekagua ujenzi wa nyumba 59 zinazojengwa kwa ajili ya makazi ya waliopisha eneo la mradi huo ambapo ameonesha kuto ridhika na ujenzi huo. 

Awali, Dkt. Kiruswa alikutana na Mkuu wa Wilaya ya Ruangwa Hassan Ngoma pamoja na Kamati ya Ulinzi na Usalama ya wilaya hiyo kwa lengo la kupata taarifa za shughuli za uchimbaji madini katika mkoa huo.

Aidha, Dkt. Kiruswa ametumia fursa hiyo  kuwasisitiza wachimbaji wa madini kote nchini kuhakikisha wanatoa ushirikiano kwa Makarani wa Sensa ili kufanikisha zoezi la kuhesabiwa kwa ajili ya maendeleo ya Sekta ya Madini na Taifa kwa ujumla.

Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Ruangwa Hassan Ngoma amempongeza Dkt. Kiruswa kwa kufanya ziara yake mkoani humo ambapo amesema ana uhakika changamoto zinazo ikabili Sekta ya Madini mkoani humo zitapatiwa suluhisho.

Naye, Meneja Uhusiano wa Lindi Jumbo Limited Paul Shauri  amesema, mgodi huo ukianza uzalishaji  utazalisha zaidi ya tani 39,000 za graphite  kwa mwaka ambapo maisha ya mgodi yanatarajiwa kuwa miaka 24 na una hifadhi ya zaidi ya tani milioni 300 za graphite zenye ubora wa hali ya juu .

No comments:

Post a Comment

ANDIKA MAONI (COMMENTS) HAPO👇

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages