Magomeni, Dar es Salaam
Katibu wa Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) Shaka Hamdu Shaka ni miongoni mwa mamia ya waombolezaji ambao wameshiriki shughuli ya mazishi ya Msanii msanii maarufu wa filamu nchini Bi Chuma Suleiman au Bi Hindu, iliyofanyika leo Jumapili, Julai 10, 2022 Jijini Dar es Salaam.
Katika shughuli hiyo ya mazishi iliyoanzia nyumbani kwa Bi Hindu Mtaa wa Butiama, Magomeni na maziko kufanyika katika makaburi ya Mwinyi Mkuu, Magomeni, yamehudhuriwa pia na Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo Mohamed Mchengerwa na viongozi wengine mbalimbali, Ndugu, jamaa, marafiki, wanamichezo na wasanii wa tasnia mbali mbali nchini.
”Chama cha Mapinduzi kitamkumbuka Bi Chuma kwa mchango wake mkubwa katika kutetea utaifa wetu kwa kudumisha utamaduni, mila, silka na desturi zetu hasa katika kuelimisha, kuhamasisha, kuburudisha na kulea rika zote kupitia semi, tungo na ujumbe maridhiwa katika nyakati tofauti” ni baadhi ya maneno aliyosema Shaka wakati akitoa salam za pole kwa niaba ya CCM kwenye mazishi hayo.
Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo Mohamed Mchengerwa pia ni miongoni mwa viongozi waliopata nafasi ya kutoa salamu za pole aliwasilisha salamu za Serikali ambapo alitoa salam za pole kwa Rais na Mwenyekiti wa CCM Samia Suluhu Hassan.
Mchengerwa amesema, Rais amemwelezea Bi. Hindu kuwa ni msanii aliyetoa mchango mkubwa katika tasnia ya Sanaa hapa nchini.
"Bi Hindu ametoa elimu ya sanaa kwa wasanii wengi sana, Serikali inatambua mchango wake. Mheshimiwa Rais Samia amepokea msiba huu kwa mshituko mkubwa". akasema Mchengerwa na kuongeza kuwa Bi Hindu amefariki wakati Serikali inafanya mapinduzi makubwa katika sekta za Sanaa.
Bi Hindu alifariki dunia jana, Jumamosi Julai 9, 2022 baada ya kuugua kwa muda mrefu.
No comments:
Post a Comment
MAONI (COMMENTS)👇