KATIBU wa Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) ya CCM, Itikadi na Uenezi Shaka Hamdu Shaka amefanya ziara ya kukagua miradi mbalimbali ya maendeleo visiwani Pemba huku akitumia nafasi hiyo kueleza Chama hicho kitaendelea kuwalinda na kutambua mchango wa wabunge,madiwani na wawakilishi ambao wako mstari wa mbele kutekeleza miradi ya maendeleo.
Shaka akiwa katika ziara hiyo iliyoanza Julai 14, 2022 visiwani humo amepata nafasi ya kukagua miradi ya ujenzi wa madarasa na kisima cha maji safi na salama katika Jimbo la Gando, miradi ambayo imewapunguzia adha wananchi ikiwemo ya kufuata maji umbali mrefu.
Akiwa katika mkutano wa hadhara ulioandaliwa na Mbunge wa Jimbo hilo Salim Mussa Omar na Mwakilishi wa Jimbo hilo Mariam Thani Juma na kufanyika kwenye Uwanja wa Mpira Kizimbami Shaka amesema utekelezaji wa miradi ya maendeleo unaofanyika katika jimbo hilo na maeneo mengine yanayoongozwa na wabunge na madiwani wa CCM.
“Utekelezaji wa miradi unaofanywa na viongozi wa CCM unalenga kutekeleza ahadi na kutatua changamoto za wananchi katika huduma za jamii ikiwemo afya, elimu na maji.Niwahakikishie wabunge,madiwani na wawakilishi wanaotokana na CCM kwamba Chama kitaendelea kuwalinda dhidi ya yeyote anayetaka kuwavuruga na kusababisha washindwe kutekeleza majukumu yao.
“Wabunge,madiwani na Wawakilishi wanapaswa kuachwa watekeleze Ilani ya Uchaguzi ya CCM na kwamba mwanachama yeyote mwenye malengo ya kuomba uongozi asubiri wakati mwafaka unaoruhusiwa kisheria,”amesema Shaka .
Maelezo hayo ya Shaka yalitokana na Mbunge na Mwakilishi wa Jimbo la Gando kutoa kilio chao mbele ya mkutano huo kuna baadhi ya wanachama wa Chama chao wamekuwa wakiwashika mashati na hivyo kuchelewesha utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi Mkuu pamoja na miradi ya maendeleo,hivyo kutoa ombi kwa Chama kuangalia namna ya kukomesha hali hiyo.
Awali kabla ya kuhudhuria mkutano huo mapema asubuhi aada ya kuwasili kisiwani Pemba , Shaka alizuru kaburi la aliyekuwa Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika Serikali ya Awamu ya Tatu marehemu Dk. Omari Ali Juma, wilayani Chakechake.
Shaka baadae alikwenda kwenye kaburi la aliyekuwa Makamu wa Kwanza wa Rais Zanzibar marehemu Maalim Seif Sharif Hamad lililopo Kijiji cha Mnyali, Mtambwe wilaya ya Were Mkoa wa Kaskazini Pemba.
Akiwa katika makaburi hayo Shaka ametumia nafasi hiyo kueleza mchango wa viongozi hao ambao enzi za uhai wao wamelitumikia Taifa kwa uadilifu mkubwa na kutekeleza majukumu yao kwa uadilifu na uzalendo mkubwa.
Aidha amesema wakati Watanzania wakiwa wametimiza miaka 30 ya mfumo wa vyama vingi vya siasa mchango wa Dk .Omari Ali Juma pamoja na Maalim Seif hautasahaulika kwani walijitoa kwa kiwango kikubwa kuufanikinisha mfumo huo
No comments:
Post a Comment
MAONI (COMMENTS)👇