Na Dismas Lyassa.
Mbunge wa Jimbo la Kibaha Mjini, Mheshimiwa Silvestry Francis Koka (aliyevaa barakoa) ametembelea shule ya msingi Mkombozi iliyoko Mtaa wa Mkombozi, Kata Pangani kujionea maendeleo ya ujenzi wa shule hiyo.
Akiwa katika eneo hilo, Mheshimiwa Koka aliwapongeza
wananchi wa Mkombozi wa kushirikiana na Serikali katika kuhakikisha shule hiyo
inajengwa na kufikia hapo ilipofikia.
Shule hiyo ambayo inaendelea kujengwa imejengwa vyumba
viwili na jengo la ofisi, na tayari imefikia linta. Inasubiri fedha kutoka
halmashauri kwa ajili ya kuezeka na kumalizia ili wanafunzi waweze kuanza
kuitumia.
“Nimefurahishwa na ujio wa Mbunge na timu yake, wakiwamo
watumishi wa halmashauri, jambo hili limenipa hamasa sana,” anasema Anasi
Bwanari, Mwenyekiti wa Serikali ya Mtaa wa Mkombozi.
Mkombozi ni mtaa mpya ambao umeanzishwa baada ya kugawanywa
mtaa wa Kidimu, Kata ya Pangani, halmashauri ya Mji Kibaha. Mtaa huu hauna
shule, hivyo kusababisha wanafunzi wakiwamo wa darasa la kwanza kulazimika kutembea
masafa marefu kutafuta shule, kitendo ambacho kimekuwa kikisababisha baadhi yao
kushindwa kwenda shule inavyotakiwa hasa kunaponyesha mvua kubwa.
Mtaa huu una changamoto nyingi zikiwamo kutokuwa na huduma
za maji, badala yake wananchi wengi Zaidi wanategemea maji ya vidimbwi ambayo
sio salama kwa matumizi. Hali kadhalika mtaa unasumbuliwa na barabara mbovu,
kitendo kinachosababisha kupitika kwa shida hasa nyakati za mvua.
“Naiona dalili njema kutoka kwa Mbunge na Serikali kwa ujumla, naamini wataongeza nguvu katika kusaidia kuondoa kero zinazotusumbua. Kwa pamoja tutaweza,” anasema Bwanari akipongeza ujio wa mheshimiwa Mbunge na viongozi wa halmashauri katika mtaa wake.
No comments:
Post a Comment
MAONI (COMMENTS)👇