LATEST HEADLINES👉

Your Ad Spot

Jan 4, 2021

DUWASA YAFUFUA KISIMA CHA MWAKA 1989 CHENYE UWEZO WA KUTOA LITA 192,000 ZA MAJI KWA SIKU



Naibu Katibu MkuuWizara ya Maji, Nadhifa Kemikimba akiangalia kibanda kilichotumika kuweka mota ya kupampu maji katika kisima cha maji kilichojengwa mwaka 1989, eneo la Nzuguni, Dodoma. Kulia ni Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Duwasa, Joseph Aron.


Kemikambi akionja maji ya kisima hicho aada ya kufufuliwa na Duwasa eneo la Nzuguni Dodoma.



Kemikambi akizungumza na baadhi ya watumishi wa Duwasa.



Na Richard Mwaikenda, CCM Blog, Dodoma.

MAMLAKA ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira Mji wa Dodoma (DUWASA), imefufua kisima cha maji kilichojengwa mwaka 1989 eneo la Nzuguni, jijini Dodoma.


Akielezea kuhusu kisima hicho mbele ya Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Maji, Nadhifa Kemikimba, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Duwasa, Joseph Aron alisema kuwa matokeo ya majaribio ya kisima hicho, yameonesha  kitakuwa kina uwezo wa kutoa lita 8000 kwa saa na kwa siku lita 192,000.


Aron, alisema kuwa Duwasa imeamua kufufua visima vya zamani 11 vilivyotelekezwa na kukosa usimamizi mzuri, ili kuongeza kiwango cha upatikanaji wa maji katika jiji la Dodoma kupunguza adha ya upungufu wa maji wanayopata wakazi wa jiji hilo ambalo  kila siku idadi ya watu inaongezeka.


Aidha, Aron alimweleza Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Maji, Kemikimba kuwa maji ya visima vilivyochimbwa na kufufuliwa yataingizwa kwenye mabomba makubwa kwa ajili ya kusambazwa kirahisi katika makazi ya jiji hilo.


 Baada ya Naibu Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Nadhifa Kemikimba kufika katika eneo hilo alishangaa kuona maji ya kisima hicho yakitoka kwa wingi, huku yakimwagika kutoka kwenye ndoo walizokinga, ambapo aliwaambia maafisa wa Duwasa kuwaita wakazi wa eneo hilo kwenda kuteka maji hayo, lakini alijibiwa kuwa waliruhusiwa kuyateka na wote wana maji ya kutosha majumbani.


Kemikimba baada ya kuelezwa na wataalamu wa Duwasa kuwa kisima hicho kilichokuwa kwenye majaribio, maji yake wameyapima na kujiridhisha kuwa yana ubora na yako salama kwa matumizi ya watu, aliamua kuteka kwa kutumia kiganja na kuyaonja.


Pia, alikagua kibanda cha mota na pumpu ambapo pia aliona jiwe la msingi la linaloonesha kisima hicho kilizinduliwa mwaka 1989 na alaliyekuwa Mkuu wa Wilaya Dodoma wakati huo.


Kemikimba akizungumza na wanahabari, watumishi wa Duwasa na baadhi ya wakazi wa Nzuguni waliokuwepo eneo hilo, alisema ameridhishwa na ubunifu wa Menejimenti ya Duwasa wa kufufua visima vya maji vilivyojengwa zamani vilivyotelekezwa na kukosa usimamizi mzuri.


“Nimefurahi sana kwa jitihada zenu, huo ni ubunifu mzuri, tangu mwanzo nimesema kabisa, changamoto huleta maarifa, na hayo mliyofanya ni maarifa, kufufua visima vya zamani vilivyokosa usimamizi, na endapo visima vyote vikifufuliwa  itasaidia kupunguza adha ya upungufu wa maji katika jiji la Dodoma,” alisema Katibu Mkuu Kemikimba.


Licha ya pongezi hizo, Kemikimba aliitaka Duwasa kuongeza kasi ya kukamilisha ufufuaji na uchimbaji wa visima hivyo kwa muda uliopangwa ili wananchi wa Dodoma wapate nafuu na kuondokana na adha wanayopata ya upungufu wa maji.


Baadhi ya wakazi wa Nzuguni waliozungmza na mwandishi wa habari hii, hawakusita kuonesha furaha yao na kwa nyakati tofauti kila mmoja alieleza kuwa kufufuliwa kwa kisima hicho utakuwa ni ukombozi kwao, kwani sasa wataondokana na adha ya kuhangaika kutafuta maji.


 Doris Sumisumi, aliishukuru serikali kwa kuwakumbuka kufufua kisima hicho kitakachowa saidia kupata kirahisi maji safi na salama.


Kabla ya kukagua kisima hicho na kujiridhisha, Kemikimba awali katika ziara yake alikagua uchimbaji  wa kisima kipya eneo la Ihumwa ambapo aliwapa siku tatu kumaliza kuchimba, alikagua ujenzi wa tanki kubwa la kuhifadhia maji eneo la Bwigiri ambapo pia alikwenda Hospitali ya Uhuru Chamwino kuangalia eneo patakapotandazwa bomba litakalokuwa linatoa maji tanki la Bwigiri kusambaza katika hospitali hiyo.

No comments:

Post a Comment

MAONI (COMMENTS)👇

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages