LATEST HEADLINES👉

Your Ad Spot

Dec 15, 2020

RAIS DK. MWINYI AKUTANA NA KUFANYA MAZUNGUMZO NA WAZIRI WA ULINZI NA JKT, IKULU MJINI ZANZIBAR, LEO

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Hussein Ali Mwinyi akisalimiana na Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa Elia Kuandikwa, wakati alipofika Ikulu Jijini Zanzibar leo kwa ajili ya kujitambulisha pamoja na kumpa pongezi kwa Ushindi alioupata katika Uchaguzi Mkuu uliopita mwaka huu.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi,Dkt.Hussein Ali Mwinyi (kulia) akimsikilza Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Mhe.Mhandisi Elias John Kuandikwa wakati walipokuwa na mazungumzo alipofika Ikulu jijini Zanzibar leo Desemba 15,2020 kwa ajili ya kujitambulisha pamoja na kumpa pongezi kwa ushindi alioupata katika Uchaguzi Mkuu uliopita mwaka huu.[Picha na Ikulu].

Rais Dkt. Hussein Mwinyi ameyasema hayo leo Ikulu jijini Zanzibar wakati alipofanya mazungumzo na Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa,Mhandisi Elias John Kuandikwa aliyefika Ikulu kwa ajili ya kujitambulisha na kumsalimia Rais ambapo pia, Waziri huyo alifuatana na Katibu Mkuu wa wizara hiyo, Faraji Mnyepe.

Katika mazungumzo hayo, Rais Dkt. Hussein Mwinyi ameeleza jinsi alivyofarajika na uteuzi wa Waziri huyo kutokana na uwezo wake mkubwa wa uongozi na kuahidi kumpa ushirkiano mkubwa ili iwe ni chachu katika utekelezaji wa kazi zake ndani ya wizara hiyo.

Rais Dkt. Hussein amesema kuwa, kwa vile wizara hiyo ni ya Muungano ana matumaini makubwa kwamba ataendelea kuwa karibu na Waziri huyo katika kuhakikisha anatekeleza vyema majukumu yake sambamba na kuhakikisha Brigedi za Zanzibar zinaendelea kuimarika zaidi.

Nae Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Mhandisi Elias John Kuandikwa ametumia fursa hiyo kumpongeza Rais Dkt. Hussein Mwinyi kwa kuchaguliwa kwa kishindo na wananchi wa Zanzibar katika Uchaguzi Mkuu uliofanyika Oktoba mwaka huu wa 2020.

Waziri Kuandikwa ameeleza matumaini yake pamoja na yale ya wananchi wa Zanzibar na Watanzania wote kwa jumla kwamba Rais Dkt. Hussein Mwinyi atawaletea maendeleo makubwa Wazanzibari hasa kutokana na kasi yake kubwa aliyoanza nayo ya utendaji wake wa kazi kwa azma ya kuwaletea wananchi maendeleo.

Aidha, Waziri Kuandikwa amempongeza Rais Dkt. Hussein Mwinyi kwa kazi nzuri aliyoifanya wakati akiwa Waziri katika Wizara hiyo jambo ambalo limempa wepesi na faraja katika uongozi wake na kuahidi kufuata nyayo zake ili kufikia malengo yaliokusudiwa.

Pamoja na hayo, Waziri Kuandikwa amemuahidi Rais Dkt. Hussein Mwinyi kwamba atahakikisha anatumia nafasi yake kuja mara kwa mara Zanzibar katika kutekeleza majukumu yake ya kikazi hasa ikizingatiwa kwamba Wizara yake ni ya Muungano.

Sambamba na hayo, Waziri Kuandikwa ameahidi kuendelea kujifunza kutoka kwa Rais Dk. Mwinyi kutokana na mafanikio makubwa yaliopatikana kutokana na uongozi wake akiwa katika Wizara hiyo huku akiahidi kufanya kazi zake kwa ustadi mkubwa zaidi.

Rais Dk. Hussein Mwinyi kabla ya kuchaguliwa kuwa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi alikuwa Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa kwa muda wa kipindi cha miaka kumi na moja.

No comments:

Post a Comment

MAONI (COMMENTS)👇

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages