LATEST HEADLINES👉

Your Ad Spot

Nov 10, 2020

DK. MAGUFULI KUWALIPA DENI KWA KUFANYA KAZI USIKU NA MCHANA

👈Na Joe Nakajumo

 "NILETEENI huyu……nileteeni hawa na mimi naomba  kura   zenu", hii ni kauli iliyotolewa na mgombea urais kwa tiketi  ya Chama  cha Mapinduzi (CCM) Dk. John Magufuli  katika mikutano yake yote ya kampeni ya uchaguzi mkuu wa Rais, wabunge na madiwani uliofanyika hivi karibuni.

Kauli mbiu hiyo imesaidia pamoja na mikakati mingine ya kampeni za uwazi za CCM kuwawezesha Dk. Magufuli, wagombea ubunge na madiwani wa CCM kuibuka washindi kwa kupata kura nyingi katika uchaguzi uliomalizika.

Dk. Magufli alitangazwa Oktoba 30, 2020 na Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) kuwa mshindi kwa kupata kura 12,516,252 sawa na asilimia 84.4.

Alipogombea mara ya kwanza Urais mwaka 2015 alipata zaidi ya kura milioni nane zikiwa ni sawa na asilimia 58.

Uchaguzi wa mwaka huu ambao ni wa sita chini ya mfumo wa vyama vingi ulifanyika Oktoba 28, mwaka huu ambapo kampeni zilianza Agosti 26 na kumalizika Oktoba 27.

Katika kipindi cha zaidi ya miezi miwili, wagombea urais, ubunge na madiwani walikuwa katika kampeni za kunadi sera za vyama vyao mbele ya wananchi ili kuomba wachaguliwe na kuongoza nchi kwa kipindi cha miaka mitano yaani 2020 hadi 2025.


WANACCM WAPOKEZANA KIJITI CHA URAIS

Tanzania iliingia kwenye mfumo wa vyama vingi 1992 na uchaguzi wa kwanza chini ya mfumo huo ulifanyika 1995 Wana CCM wamekuwa wakipokezana kijiti cha mbio za kuwania Urais na kushinda.

Mshindi wa kwanza kiti cha Rais kwa tiketi ya CCM alikuwa hayati Benjamin Mkapa.

Tangu wakati huo kwa mfululizo CCM imeshinda kiti cha Urais ambapo hayati Mkapa aliyefariki Julai mwaka huu alitetea kiti chake, mwaka 2005 ulipofanyika uchaguzi na Dk.Jakaya Kikwete alishinda kuwa Rais miaka 10 kuanzia 2005 hadi mwaka 2015.

Baada ya Rais Kikwete kuondoka, Dk.Magufuli alipokea kijiti na kushinda uchaguzi wa mwaka huo Oktoba 2015.

Mwaka huu matokeo yaliyotangazwa  yanamwezesha kumalizia kipindi cha pili cha miaka mitano  hadi 2025.

Mgombea wa CCM, Dk. Magufuli ambaye ni Mwenyekiti wa CCM ,alikuwa ni miongoni mwa wagombea kutoka vyama 15 walioshiriki kuwania nafasi ya Urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Tofauti na wagombea wenzake 14 wakiwemo wanawake wawili, Dk. Magufuli ambaye kwa mara ya kwanza alishinda Urais mwaka 2015,alipitishwa na Mkutano Mkuu wa Chama kugombea urais kwa kipindi kingine cha miaka mitano.

Katika mikutano yake ya kujinadi kwa Watanzania akiomba ridhaa yao ili wamchague kumalizia ngwe ya pili ya miaka mitano ijayo, Dk. Magufuli alikuwa akisisitiza sana umoja, mshikamano na kudumisha amani.


USHINDI  NA UKAMILISHAJI WA MIRADI.

Suala lingine alilokuwa akiwaeleza wananchi ni mafanikio ya utendaji wa serikali yake katika kipindi cha miaka mitano aliyomaliza.

Aliwatajia wananchi mafanikio yaliyopatikana katika sekta zote za jamii zikiwemo afya,maji,miundombinu na elimu.

Aidha alikuwa akiwaeleza mambo ambayo serikali yake itatekeleza kwa mujibu wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM kwa kipindi cha miaka mitano ijayo iwapo Chama chake kitapata ridhaa ya wananchi kuongozi nchi.

Lakini pia alikuwa akiwakumbusha  wananchi jinsi serikali yake ilivyoibua na kuanza kutekeleza miradi mikubwa ya kimkakati na kuwaomba ridhaa wamchague ili aweze kukamilisha miradi aliyoianzisha maana hakuna uhakika wa miradi hiyo kukamilishwa endapo hatachaguliwa.

Miradi hiyo ni ujenzi wa reli ya kisasa itakayotumia umeme kutoka Dar es Salaam hadi Mwanza na Kigoma.

Awamu ya kwanza ya mradi wa reli ya kisasa ’STANDARD GAUGE RAILWAY SGR kutoka Dar es Salaam hadi Morogoro unakaribia kukamilika kwani umefikia asilimia 95.

Treni ya umeme itakayosafiri katika reli hiyo itakuwa na kasi ya kilomita 160 kwa saa.

Dk.Magufuli alitaja miradi mingine inayotekelezwa ni ujenzi wa bwawa la Nyerere kufua umeme katika mto Rufiji ambapo litakapokamilika mwaka 2022 litazalisha umeme wa kilovoti 2,115.

Pia mara tu baada  ya serikali yake kuingia madarakani  mwaka 2015,ilishanunua ndege mpya 11, na tayari ndege nane zinafanya kazi serikali ikiwa imezikodisha ndege hizo kwa  Shirika la Ndege la Tanzania (ATCL).

Mgombea wa CCM anasema Ilani ya Uchaguzi wa CCM yenye kurasa 303 ina kipengele cha ununuzi wa ndege nyingine mpya tano moja ikiwa ya mizigo.

AING’ARISHA DODOMA NA IKULU YA CHAMWINO

Uamuzi mwingine wa kihistoria ambao Dk. Magufuli aliuchukua mara baada ya kuingia madarakani ni serikali yote kuhamia makuu Dodoma.

Hatua hii aliichukua baada ya kipindi cha zaidi ya miaka 40 tangu serikali ya awamu ya kwanza iliyoongozwa na hayati Baba wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere, kuamua makao makuu ya serikali yahamia Dodoma kutoka Dar es Salaam.

 Uamuzi wa kuhamia Dodoma ulipitishwa na Mkutano Mkuu wa TANU Oktoba, mwaka 1973.

Hivi sasa serikali nzima ipo Dodoma Rais Dk.Magufuli ameenda mbele zaidi kwa kupanua eneo la Ikulu Chamwino kwa kuongeza majengo mapya na kuweka bustani ya wanyamapori ndani ya eneo hilo lenye ukubwa wa  ekari 8,473 ambalo limezungushiwa ukuta wa kilomita 27.

Ikulu ya Dar es Salaam na barabara zake ina eneo la kilomita 41.8. Dodoma mji wa serikali upo eneo la Itumba ambako kuna wizara zote.

 

ALIWABEBA WAGOMBEA WA CCM

Kwenye mikutano ya kampeni, Dk. Magufuli alikuwa na kazi ya ziada na katika majimbo mengine  kazi ya kuwaombea wabunge na madiwani kura ilikuwa ngumu kutokana na fununu alizokuwa nazo kwamba mgombea aliyepitishwa na Chama hakubaliki na hivyo kusababisha wasiwasi wa Chama kushinda katika jimbo husika.

Lakini kwa ujasiri mkubwa alizisawazisha kasoro hizo mbele ya halaiki ya wananchi waliohudhuria mikutano yake.

Mtindo wake wa kuwaombea kura wagombea   ubunge na udiwani umesaidia sana kuiwezesha CCM kupata ushindi wa kishindo na wa kihistoria katika uchaguzi mkuu wa mwaka huu wa 2020.

Alikuwa anawasimamisha wabunge mmoja mmoja kuomba kura na madiwani wote wa jimbo husika walisimama katika msitari mmoja mbele ya umati wa watu na kuwaombea kura.

‘Nileteeni huyu…… kwa maana mbunge na nileteeni hawa kwa maana ya madiwani Na alimalizia kwa kuwaomba wananchi kwamba ‘na mimi naomba kura,wangapi watanipigia, aliwauliza wananchi nao waliitika kwa umoja wao wakisema ‘umepita baba, umepata baba’.

Jambo lingine ambalo alilifanya kwa wagombea udiwani wa CCM ni yeye kuwaapisha mbele ya wananchi kwa kuwataka warudie maneno aliyokuwa akiyatamka kwa mfano’,nitajitahidi kusikiliza kero za wananchi na kutafuta namna ya kuzitatua,sitaomba rushwa.’

‘Mkinichanganyia kazi yangu itakuwa mgumu,lakini mkiniletea hawa wa CCM, ni rahisi kuwadhibiti kwa sababu mimi ndio Mwenyekiti wao,madiwani ndio wanaosimamia shughuli za Halmashauri na halmashauri inapokea fedha nyingi kutoka serikali kuu,

kwa hiyo hawa wana majukumu makubwa ya kusimamia miradi ya maendeleo katika maeneo yao,’ aliwaeleza  wananchi katika mikutano yake.


ATALIPA DENI KWA KUCHAPA USIKU NA MCHANA

Hatimaye Dk. Magufuli aliyezindua  kampeni kwa Chama chake cha Mapinduzi  Agosti 29 mkoani Dodoma na alihitimisha  hapo hapo Dodoma Oktoba 27 kwa kuzungumza na wazee mjini Dodoma.

Kutokana na wananchi wengi kujitokeza kwa wingi katika mikutano yake ya kampeni, Dk. Magufuli alikuwa akiwaeleza wazi kwamba alikuwa na deni kwao.

Siku ya Novemba Mosi,2020,katika ukumbi wa  Tume UCHAGUZI HOUSE Dodoma alipokabidhiwa cheti cha ushindi na Tume ya Taifa ya Uchaguzi, Rais Mteule Dk. Magufuli katika hotuba yake fupi ya kuwashukuru wananchi  alisema;’kwangu mimi nina deni kubwa sana kwa  Watanzania kwa imani yao na mimi nitatimiza kwa kufanya kazi usiku na mchana.’

Katika uchaguzi mkuu wa mwaka huu wa 2020  wananchi 12,516,252 wamemkubali Dk. Magufuli na kumpa ridhaa ya kuongoza kipindi kingine cha miaka mitano ambacho ni cha mwisho kwake kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Wagombea wengine wa Urais walikuwa Tundu Lissuwa Chadema aliyepata kura 1,933,271,Bernard Membe wa ACT Wazalendokura 81,129,Profesa Mahona Lucas wa  NRA kura 80,787, Ibrahim Lipumba CUF kura 72,885,

John Shibuda wa ADA TADEA kura 33,086 Mutamwega Mugahywa wa SAU 14,922,Cecilia Mmanga Demokrasia Makini kura 14,556,Maganja Jeremiah NCCR Mageuzi kura 19,969,.

Philipo Fumbo wa DP kura 8,283,Queen Sendiga  ADC kura 7,627,Twalib Kadege wa UPDP kura 6,194,Hashim Rungwe wa CHAUMA kura 32,878 na Mazrui Khalfan Mohamed wa UMD kura 3,721 na Seif Maalim Seif wa AAFP kura 4,635. 

#Mwandishi wa Makala hii anapatikana kwenye simu namba 0784291434 email nakajumoj@gmail.com

No comments:

Post a Comment

MAONI (COMMENTS)👇

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages