LATEST HEADLINES👉

Your Ad Spot

Nov 5, 2020

DK. JOHN MAGUFULI AAPISHWA KUWA RAIS JIJINI DODOMA



JAJI Mkuu wa Tanzania Mhe Profesa Ibrahim Hamis Juma 
akimuapisha Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. John Pombe Magufuli leo 5/11/2020, katika uwanja wa Jamuhuri Jijini Dodoma, baada ya kushinda uchaguzi Mkuu wa Tanzania uliofanyika mwaka huu Oktoba 28,2020.(Picha na Ikulu)

Ikulu, Dodoma

Mhe. Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, leo tarehe 05 Novemba, 2020 ameapishwa kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kipindi cha pili cha miaka 5 baada ya kipindi cha kwanza cha miaka mitano kumalizika.

Mhe. Dkt. Magufuli ameapishwa kushika wadhifa huo baada ya kushinda katika uchaguzi mkuu uliofanyika tarehe 28 Oktoba, 2020 ambapo alipata jumla ya kura 12,516,252 sawa na asilimia 84.4 ya kura zote zilizopigwa kwa wagombea 15 waliokuwa wanawania kiti cha Urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Mhe. Dkt. Magufuli ameapishwa pamoja na Mhe. Samia Suluhu Hassan ambaye ameapishwa kuwa Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Sherehe za kiapo hicho zimefanyika kwa mara ya kwanza katika uwanja wa Jamhuri Jijini Dodoma ambako ni Makao Makuu ya Tanzania na zimehudhuriwa na viongozi mbalimbali wakiwemo Wakuu wa Nchi na Serikali, Makamu wa Rais, Mawaziri Wakuu, Marais Wastaafu, Makamu wa Rais Wastaafu, Mawaziri Wakuu Wastaafu, Mawaziri, Mabalozi, Wawakilishi wa Mashirika ya Kimataifa na Jumuiya za Kikanda, viongozi wakuu wa vyombo vya Ulinzi na Usalama, viongozi wa Dini, viongozi wa vyama vya siasa kikiwemo chama tawala nchini Tanzania (Chama Cha Mapinduzi – CCM) na viongozi wa sekta binafsi.

Viongozi Wakuu wa Nchi waliohudhuria sherehe hizo ni Rais wa Jamhuri ya Uganda, Mhe. Yoweri Kaguta Museveni, Rais wa Umoja wa Visiwa vya Komoro Mhe. Azali Assoumani, Rais wa Jamhuri ya Zimbabwe Mhe. Emerson Mnangagwa na pia Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Botswana Mhe. Slumber Tsogwane ambaye amemwakilisha Rais wa nchi hiyo Mhe. Mokgweetsi Masisi, Waziri Mkuu wa Msumbiji Mhe. Carlos Agostinho Rosario ambaye amemwakilisha Rais wa Msumbiji Mhe. Filipe Nyusi na Naibu Waziri Mkuu wa Qatar Sultan bin Saad Al Muraikhi aliyemwakilisha Mtawala wa Qatar Sheikh Tamim bin Hamad Al-Than.

Aidha, Marais na Wakuu wa Nchi na Serikali wa Kenya, Afrika Kusini, DRC, Malawi, Misri, Zambia, Kuwait, Namibia, Rwanda, Umoja wa Ulaya na Ethiopia wamewakilishwa naWaheshimiwa Mawaziri na Mabalozi wa nchi hizo.

Akizungumza baada ya kuapishwa kwake, Mhe. Rais Magufuli amewashukuru viongozi wote waliohudhuria sherehe za kuapishwa kwake wakiwemo Mabalozi wanaoziwakilisha nchi mbalimbali hapa nchini na amewahakikishia kuwa Tanzania itaendeleza ushirikiano na uhusiano mzuri uliopo kati yake na nchi hizo.

Mhe. Rais Magufuli amevishukuru vyombo vya ulinzi na usalama pamoja na wananchi wote wa Tanzania kwa kuhakikisha mchakato wa uchaguzi mkuu unafanyika na kukamilika kwa amani na utulivu, jambo ambalo limeendelea kudhihirisha kuwa Tanzania sio tu kisiwa cha amani bali pia ni kitovu cha demokrasia.

Mhe. Rais Magufuli amesema uchaguzi umekwisha na kwamba jukumu lililo mbele ya Watanzania ni kuchapa kazi na kuleta maendeleo. Hivyo ameahidi kutekeleza Ilani ya Uchaguzi Mkuu ya CCM ya mwaka 2020/25 huku akitilia mkazo katika ujenzi wa miradi ya maendeleo, kutunza rasilimali za Taifa, kuzalisha ajira, kushughulikia kero za wananchi na kuzidisha mapambano dhidi ya rushwa.

Amekishukuru chama chake cha CCM kwa kufanya kampeni nzuri zilizowezesha kupata ushindi mkubwa katika uchaguzi mkuu wa Rais, Wabunge na Madiwani ambao sasa wanakwenda kubeba jukumu la kuwahudumia wananchi wa Tanzania kama walivyoahidi.

Katika sherehe hizo Wakuu wa Nchi wamepata nafasi ya kutoa salamu ambapo Mhe. Rais Museveni pamoja na kumpongeza Mhe. Rais Magufuli kwa kuchaguliwa na kuapishwa kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania amewataka Watanzania hasa vijana kurejea madhumuni ya uhuru uliopiganiwa na waasisi akiwemo Hayati Mwl. Julius Kambarage Nyerere huku akiwataka kujiepusha kuwa vibaraka wa mabeberu na kufanya kazi ili kujitegemea na kujenga ustawi wa jamii.

Kwa upande wake, Mhe. Rais Mnangagwa wa Zimbabwe ameishukuru Tanzania ambayo amesema Zimbabwe inaiona kama Baba na Mama huku akitambua juhudi za kuanzia Hayati Mwl. Nyerere hadi Mhe. Rais Magufuli ambao wamekuwa mstari wa mbele kuipigania Zimbabwe bila kuchoka.

 

Gerson Msigwa

Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais, IKULU

Chamwino                                            

05 Novemba, 2020

No comments:

Post a Comment

MAONI (COMMENTS)👇

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages