LATEST HEADLINES👉

Your Ad Spot

Oct 19, 2020

RAIS DK. MAGUFULI AMKABIDHI NYUMBA MZEE MWINYI, AKAGUA UJENZI WA NYUMBA YA KIKWETE NA KWENDA KUMSALIMIA MAMA ANNA MKAPA, LEO

Ikulu, Dar es Salaam

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli leo tarehe 18 Oktoba, 2020 amemkabidhi nyumba mpya ya kuishi Rais Mstaafu wa Awamu ya Pili, Mhe. Dkt. Ali Hassan Mwinyi iliyopo Masaki Jijini Dar es Salaam.


Nyumba hiyo imejengwa na Serikali ya Tanzania na kisha kukabidhiwa kwa Mhe. Rais Mstaafu Mwinyi kwa mujibu wa sheria ya mafao ya viongozi wa kisiasa namba 3 ya mwaka 1999 na marekebisho yake ya mwaka 2005 ambayo inaelekeza kuwa Marais wanapostaafu wanastahili kujengewa nyumba na Serikali.


Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Dkt. Laurian Ndumbaro amesema ujenzi wa nyumba ya Rais Mstaafu Mwinyi ulioanza mwaka 2005 ulisimama kwa muda mrefu na baadaye mwaka 2018 uliendelea chini ya Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) kupitia Shirika lake la Suma JKT kwa ushirikiano na Wakala wa Majengo Tanzania (TBA) hadi ulipokamilika.


Akizungumza baada ya kukabidhiwa nyumba hiyo, Rais Mstaafu Mwinyi amemshukuru Mhe. Rais Magufuli kwa kutoa msukumo mkubwa wa kukamilishwa kwa nyumba hiyo na pia ameishukuru Suma JKT na TBA kwa kujenga kwa ubora wa hali ya juu.


Mhe. Rais Magufuli amempongeza Rais Mstaafu Mwinyi kwa kupata nyumba hiyo, na amemtakia heri na maisha mema katika makazi yake hayo mapya. Pia ameipongeza Suma JKT na TBA kwa kukamilisha ujenzi wa nyumba hiyo.


Wakati huo huo, Mhe. Rais Magufuli amekagua jengo la nyumba ya Rais Mstaafu wa Awamu ya Nne, Mhe. Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete inayojengwa katika eneo la Kawe Jijini Dar es Salaam.


Ujenzi wa nyumba hiyo ulianza mwaka 2018 chini ya TBA na Mhe. Rais Magufuli ameiagiza TBA kuhakikisha ujenzi wa nyumba, uzio na mandhali yake unakamilika ifikapo tarehe 30 Januari, 2021.


Aidha, Mhe. Rais Magufuli ameiagiza Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) kujenga barabara ya lami yenye urefu wa meta 800 itakayounganisha nyumba hiyo na barabara ya lami iliyokaribu nayo.

Rais Mstaafu Kikwete amemshukuru Mhe. Rais Magufuli kwa ujenzi wa nyumba hiyo ambayo amesema anatarajia ndipo ataishi maisha yake yote.


Mapema leo asubuhi, Mhe. Rais Magufuli akiwa na Mkewe Mama Janeth Magufuli wamekwenda kumsalimu Mjane wa Rais Mstaafu wa Awamu ya Tatu, Mama Anna Mkapa nyumbani kwake Masaki Jijini Dar es Salaam.

PICHA: 👇


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt John Pombe Magufuli akimkabidhi mfano wa funguo Rais wa Awamu ya Pili Alhaj Ali Hassan Mwinyi na mkewe Mama Sitti Mwinyi katika hafla ndogo ya kumkabidhi
nyumba hiyo ambayo serikali imemjengea Mzee Mwinyi kwa mujibu wa sheria eneo la  Masaki jijini Dar es salaam leo Jumapili Oktoba 18, 2020. Kulia ni Mama Janet Magufuli.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt John Pombe Magufuli akiwa na Rais wa Awamu ya Pili Alhaj Ali Hassan Mwinyi wakati  akimkabidhi nyumba ambayo serikali imemjengea Mzee Mwinyi kwa mujibu wa sheria eneo la  Masaki jijini Dar es salaam leo Jumapili Oktoba 18, 2020

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt John Pombe Magufuli na Rais wa Awamu ya Pili Alhaj Ali Hassan Mwinyi wakishirikiana kukata utepe wakati wa kumkabidhi nyumba ambayo serikali imemjengea Mzee Mwinyi kwa mujibu wa sheria eneo la  Masaki jijini Dar es salaam leo Jumapili Oktoba 18, 2020

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt John Pombe Magufuli akimsikiliza Rais wa Awamu ya Pili Alhaj Ali Hassan Mwinyi akishukuru baada ya  kumkabidhi nyumba ambayo serikali imemjengea Mzee Mwinyi kwa mujibu wa sheria eneo la  Masaki jijini Dar es salaam leo Jumapili Oktoba 18, 2020
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt John Pombe Magufuli akiwa na Mkewe Mama Janeth Magufuli wakiwa katika picha ya pamoja na Rais wa Awamu ya Pili Alhaj Ali Hassan Mwinyi na mkewe Mama Sitti
Mwinyi na Mkuu wa Mkoa wa Dar es salaam Mhe Abubakar Kunenge na Vijana wajenzi wa JKT wakati wa hafla ndogo ya kumkabidhi nyumba Mzee Mwinyi ambayo serikali imemjengea kwa mujibu wa sheria eneo la  Masaki jijini
Dar es salaam leo Jumapili Oktoba 18, 2020
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt John Pombe Magufuli akiwa na Rais Mstaafu wa Awamu ya nne Dkt Jakaya Mrisho Kikwete alipotembelea na kukagua maendeleo ya ujenzi wa nyumba ambayo Dkt. Kikwete anajengewa na Serikali kwa mujibu wa Sheria eneo la Kawe Beach jijini Dar es salaam leo Jumapili Oktoba 18, 2020
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt John Pombe Magufuli akimsikiliza Rais Mstaafu wa Awamu ya nne Dkt Jakaya Mrisho Kikwete aliyekuwa akizungumza alipotembelea na kukagua maendeleo ya ujenzi wa nyumba ambayo Dkt. Kikwete anajengewa na Serikali kwa mujibu wa Sheria eneo la Kawe Beach jijini Dar es salaam leo Jumapili Oktoba 18, 2020
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt John Pombe Magufuli akiongea huku akisikilizwa kwa makini na Rais Mstaafu wa Awamu ya nne Dkt Jakaya Mrisho Kikwete alipotembelea na kukagua maendeleo ya ujenzi wa nyumba ambayo Dkt. Kikwete anajengewa na Serikali kwa mujibu wa Sheria eneo la Kawe Beach jijini Dar es salaam leo Jumapili Oktoba 18, 2020
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt John Pombe Magufuli akielezwa jambo na Rais Mstaafu wa Awamu ya nne Dkt Jakaya Mrisho Kikwete alipotembelea na kukagua maendeleo ya ujenzi wa nyumba ambayo Dkt. Kikwete anajengewa na Serikali kwa mujibu wa Sheria eneo la Kawe Beach jijini Dar es salaam leo Jumapili Oktoba 18, 2020
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt John Pombe Magufuli akiagana na Rais Mstaafu wa Awamu ya nne Dkt Jakaya Mrisho Kikwete alipotembelea na kukagua maendeleo ya ujenzi wa nyumba ambayo Dkt. Kikwete anajengewa na Serikali kwa mujibu wa Sheria eneo la Kawe Beach jijini Dar es salaam leo Jumapili Oktoba 18, 2020



Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt John Pombe Magufuli akimuaga Mama Anna Mkapa,
Mjane wa Rais ya Awamu ya Tatu Marehemu Benjamin William Mkapa, baada ya kuzungumza naye  alipokwenda kumjulia hali nyumbani kwake Masaki jijini Dar es salaam leo Jumapili Oktoba 18, 2020

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt John Pombe Magufuli na Mkewe Mama Janeth Magufuli wakizungumza  na Mama Anna Mkapa, Mjane wa Rais ya Awamu ya Tatu Marehemu Benjamin William Mkapa, na
walipokwenda kumjulia hali nyumbani kwake Masaki jijini Dar es salaam leo Jumapili Oktoba 18, 2020. PICHA ZOTE NA IKULU

No comments:

Post a Comment

MAONI (COMMENTS)👇

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages