LATEST HEADLINES👉

Your Ad Spot

Oct 11, 2020

MGOMBEA UBUNGE CCM AAHIDI KUIMARISHA SEKTA YA MAWASILIANO ILEMELA

 

………………………………………………………………………………….
Mgombea Ubunge kupitia Chama Cha Cha Mapinduzi kwa Jimbo la Ilemela Mhe Dkt Angeline Mabula ameahidi kuboresha na kuiimarisha sekta ya mawasiliano ndani ya Jimbo hilo kwa kuhakikisha anafungua njia za barabara  zilizokuwa hazipitiki na  minara ya simu inajengwa maeneo yote yenye changamoto za kimtandao.

Hayo ameyasema wakati akihutubia wananchi wa Kata ya Sangabuye katika viwanja vya shule ya msingi Isesabudaga ikiwa ni muendelezo wa mikutano yake ya kampeni kuwaomba wananchi wa Jimbo hilo wamchague ili kuendelea na utekelezaji wa shughuli za kimaendeleo.

Amesema kuwa kupitia ofisi yake ameshafungua barabara za enzi ya mkoloni ambazo zilizokuwa zimesahaulika na hazipiti ndani ya kata hiyo ya Sangabuye na kuongeza kuwa kiasi Cha shilingi milioni 100 zimetumika kujenga mnara wa kampuni ya Vodacom katika eneo la shule ya msingi Isesabudaga huku shule hiyo ikipata kiasi Cha shilingi laki mbili na elfu hamsini kila mwezi kama Kodi ya pango  ya eneo lao lilitumika kwaajili ya ujenzi wa mnara huo.

‘.. Wakati tunaomba ridhaa yenu mtuchague kwa kura nyingi kipindi kilichopita natambua kulikuwa na changamoto ya mawasiliano, Barabara zilikuwa hazipitiki na hata simu zilikuwa changamoto ..’ Alisema
Aidha Dkt Mabula akaongeza kuwa upo mpango wa ujenzi wa minara ya mawasiliano kutoka kampuni za Airtel na Vodacom katika kata za Bugogwa, Ilemela na Buswelu ili kumalizia kabisa changamoto za kukosekana kwa mtandao sanjari na kuahidi kuimalizia mitaa 56 yenye changamoto ya umeme Kati ya mitaa 171 ya Jimbo hilo katika kipindi kijacho.

Kwa upande wake meneja kampeni wa CCM kwa Jimbo la Ilemela Ndugu Kazungu Safari Idebe akasema kuwa katika kata hiyo imejengwa shule ya kidato Cha tano na Sita Sangabuye sekondari na kwa mwaka huu mpya wa fedha imetengwa fedha kiasi Cha shilingi milioni 72 kukamilisha ujenzi wa Bweni la wasichana wa shule hiyo ili kukwepa changamoto ya muingiliano na Jamii Jambo linalochangia tatizo la  mimba kwa wanafunzi.

 Aliwaomba wananchi hao kumpa tena Kura nyingi Rais Mhe John Magufuli Kama shukran kwa kuwaondolea wazazi na walezi kero ya uchangiaji wa gharama kubwa za elimu kwa kuja na mpango wa Elimu Bure Jambo lililochangia baadhi ya watoto hasa wa kipato Cha chini kushindwa kumudu gharama na matokeo yake kushindwa kusoma. 

Kwa upande wake mwenyekiti wa CCM wilaya ya Ilemela Ndugu Nelson Mesha akawataka wananchi hao kutochanganya wagombea kwa kuhakikisha wanapigia Kura wagombea wa CCM pekee kwa nafasi zote za Urais, Ubunge na Udiwani ili suala la maendeleo liwe rahisi kutekelezeka wakati mgombea wa udiwani wa kata ya Sangabuye Ndugu Renatus Mulunga Bahebe akiahidi kushirikiana nao tena katika kuhakikisha wanamalizia kutatua kero na changamoto zilizobaki baada ya kumchagua kwa kipindi kingine.

No comments:

Post a Comment

MAONI (COMMENTS)👇

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages