LATEST HEADLINES👉

Your Ad Spot

Oct 11, 2020

MAJALIWA: BIMA YA AFYA KWA WATANZANIA WOTE INAKUJA

Mjumbe wa Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya CCM Majaliwa Kassim Majaliwa

Na Mwandishi Maalum, Tanga

MJUMBE wa Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Taifa ya Chama cha Mapinduzi (CCM), Kassim Majaliwa amesema Serikali inayoongozwa na CCM imedhamiria kuimarisha mfumo wa utoaji huduma za afya kwa wananchi kwa kuboresha mifumo ya bima ya Afya nchini ikiwemo Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) na Mfuko wa Afya ya Jamii (CHF) ili kufikia lengo lake la kuwa na bima ya afya kwa wananchi wote.


Serikali inachukua ahatua hizo ikiwa ni utekelezaji wa Ilani ya CCM ya Uchaguzi ya mwaka 2020-2025, ambayo inaielekeza kwamba katika kipindi cha miaka mitano ijayo Serikali iendelee kutoa kipaumbele katika sekta ya afya kwa kuwa sekta hiyo inagusa maisha ya Watanzania na ustawi wa Taifa, huku lengo likiwa ni kuhakikisha wananchi wanakuwa na afya  bora ili waweze kushiriki katika shughulli za ujenzi wa Taifa na kuboresha maisha yao.


Majaliwa alitoa kauli hiyo jana, Jumamosi, Oktoba 10, 2020 alipozungumza na wananchi kwa nyakati tofauti katika mikutano ya kampeni ya kuiombea kura CCM, hususan za mgombea urais kwa tiketi ya CCM Rais Dk. John Magufuli, mgombea ubunge jimbo la Korogwe Vijijini, Timotheo Mzava na wagombea udiwani kwa tiketi ya CCM, ambapo aliwaomba wananchi hao wawachague wagombea wa CCM ili waweze kushirikiana kuwaletea maendeleo.

 

Alisema awali Serikali ilianzisha Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) ambao ulihusisha watumishi wa umma na baada ya kupata mafanikio ilianzisha Mfuko wa Afya ya Jamii (CHF) ambapo wananchi wanajipangia kiasi cha kuchangia katika maeneo na kuwawezesha kupata huduma za afya pamoja na familia zao.

 

“Awali mfuko huu wa CHF uliwezesha wananchi kutibiwa ndani ya wilaya zao tu ambapo kwa sasa umeboreshwa na kuwawezesha kutibiwa ndani ya mikoa yao, baada ya kupata mafanikio makubwa katika uendeshaji wa mifuko kwa sasa Serikali inaandaa utaratibu wa kutoa huduma za afya kwa Watanzania wote na tayari kazi imeanza kwa muswada kusomwa kwa mara ya kwanza bungeni.”


Majaliwa alisema changamoto ya upatikanaji wa huduma za afya katika Halmashauri ya Wilaya ya Korogwe mkoani Tanga kuwa historia baada ya Serikali kutoa sh. Bilioni 1.8 kwa ajili ya ujenzi wa Hospitali ya Wilaya Makuyuni, ambapo tayari ujenzi wa majengo sita umekamilika na jengo moja linamaliziwa.

 

Pia, Serikali imetoa sh. Milioni 598.6 kwa ajili ya ujenzi wa kituo cha Afya Mkumbara na sh. Milioni 200 kimetolewa kwa ajili ya ujenzi wa kituo kingine cha afya cha Kerenge, ambapo ujenzi wa vituo hivyo tayari umekamilika na taratibu za ununuzi wa vifaa tiba unaendelea kufanyika.

 

Kuhusu utekelezaji wa miradi ya elimu katika wilaya hiyo, Majaliwa alisema, Serikali imetoa Sh. Bilioni 3.188 kwa shule 138 za msingi kwa ajili ya ukarabati, utawala, michezo, mitihani na posho kwa Maofisa Elimu Kata na Walimu Wakuu huku Sh. bilioni 2.50 zimetolewa kwa shule 28 za sekondari kwa ajili ya fidia ya ada, chakula kwa shule za bweni na posho ya madaraka kwa Wakuu wa Shule.

 

“Sh. Bilioni 1.410 zimetolewa kwa ajili ya ukamilishaji wa miundombinu ya madarasa, vyoo na ofisi kwa shule 58 ikiwemo ujenzi wa madarasa ya shule za msingi za Mruazi, Gereza, Kwamzindawa, Bombo Majimoto ,Mswaha, Lewa na Mkumbara na shilingi bilioni 1.568 zimetolewa kwa ajili ya ujenzi wa miundombinu ya madarasa, vyoo na maabara kwa shule za sekondari za Madago, Mkalamo, Mashindei, Mkomazi, Buiko, Patema, Kwagunda, Mazinde Day, Hale, Mnyuzi na Bungu.” Alisema Majaliwa.

No comments:

Post a Comment

MAONI (COMMENTS)👇

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages