LATEST HEADLINES👉

Your Ad Spot

Mar 29, 2020

SUMAYE AKABIDHIWA KADI YA UANACHAMA NA KATIBU MKUU WA CCM DKT BASHIRU ALLY

 Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Dkt. Bashiru Ally (aliyesimama) akizungumza jambo kabla ya hafla fupi ya kumkabidhi rasmi kadi ya uanachama wa chama hicho Waziri Muu Mstaafu ndugu Fredrick Sumaye leo Machi 29 jijini Dodom.
 Mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM ambaye pia ni Waziri Mkuu Mstaafu Mizengo Pinda (aliyesimama) akizungumza jambo katika hafla fupi ya kukabidhiwa rasmi kadi ya uanachama wa chama hicho Waziri Muu Mstaafu ndugu Fredrick Sumaye leo Machi 29 jijini Dodom. 
 Waziri Muu Mstaafu ndugu Fredrick Sumaye (kushoto) akizungumza jambo mara baada ya hafla fupi ya kukabidhiwa rasmi kadi ya uanachama wa chama Cha Mapinduzi na Katibu Mkuu wa Chama Dkt. Bashiru Ally

 Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Dkt. Bashiru Ally (kulia) akimkabidhi rasmi kadi ya uanachama wa chama hicho Waziri Muu Mstaafu ndugu Fredrick Sumaye leo Machi 29 jijini Dodom.

Na Sakina AbdulMasoud,Dodoma

KATIBU Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Dkt Bashiru Ally amemkabidhi rasmi kadi ya uanachama wa chama hicho Waziri Mkuu Mstaafu ndugu Fredrick Sumaye Machi 29 jijini Dodoma.

Awali Sumaye alikuwa mwanachama wa CCM kabla ya kuhamia Chama Cha Demokrasia na Maendeleo(CHADEMA) na baadae kuamua kurudi CCM.

Akikabidhi kadi hiyo Dkt Bashiru amesema Sumaye amekabidhiwa kadi Dodoma kwa sababu Chama hicho ni chama cha kitaifa na sio chama cha watu na hiyo ndio sababu CCM inaendelea kuongoza nchi kutokana na kuwa ni kimbilio la wanyonge.

“Mnaweza kujiuliza kwa nini akabidhiwe Dodoma badala ya Hanang,sababu ni kwamba hata kadi ya awali aliipatia tawi la makao makuu hapa Dodoma,na hii ya leo inatolewa na tawi la Mji Mpya hapa hapa Dodoma,”alisema Dkt Bashiru.

Hata hivyo amesema mara zote chama kinapopokea mwanachama mpya huwa kinafanya sherehe lakini mara hii wamesitisha kutokana na kufuata maelekezo ya serikali ya kuwa na tahadhari dhidi ya Virusi vya Corona (COVID 19).

“Ndani ya CCM leo ni siku muhimu sana,kila tunapopokea mwanachama huwa ni sherehe kubwa,lakini kutokana na tahadhari tunayoichukua kwa kufuata maelekezo ya serikali,tunasitisha sherehe hii lakini ipo siku tutafanya sherehe ya mapokezi haya,”alisema Dkt Bashiru.

Akizungumza baada ya kukabidhiwa kadi hiyo Sumaye amesema ameshukuru kurudi nyumbani na kuahidi kutoa ushirikiano kwa viongozi na wanachama wa chama hicho.

“Nakushukuru Katibu Mkuu ulinipokea Dar es salaam na leo umekuja kunikabidhi kadi Dodoma,nitoe shukrani kwa tawi la Mji Mpya maana wao wangenikataa tu wakasema alikwendaga kufanya nini huko hatumhitaji lakini wamenipokea bila hata ya kuumizwa maana mngeweza kunipa adhabu lakini hawajafanya hivyo,”

Amekumbushia kauli yake aliyowahi kuitoa wakati anaondoka CCM, “Naondoka CCM lakini sina chuki na CCM,sina chuki na aliyekuwa mwenyekiti wa chama wakati huo Dkt Jakaya Kikwete,na nilisema sina chuki na mgombea aliyeteuliwa kugombea urais Dkt John Magufuli,sasa unaweza kushangaa kama sikuwa na chuki kwa nini niliondoka sasa hiyo nitaieleza siku nyingine,”aliongeza Sumaye.

Kwa upande wake Mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM ambaye pia ni Waziri Mkuu Mstaafu Mizengo Pinda amesema amefurahi kwa kuwa wakati wanaondoka CCM alipata shida sana kwani aliishi nao kama kaka zake.

“Walipoondoka kaka zangu hawa tena kwa mara moja nilipata wakati mgumu,nilipata pigo kwak uwa nilizoea kwenda kumsalimia kaka yangu Sumaye kutokana na kwamba tulikuwa majirani pia,lakini kwa sasa hakuna kikwazo cha kwenda kwake kunong’ona,”alisema Pinda.

No comments:

Post a Comment

ANDIKA MAONI (COMMENTS) HAPO👇

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages