Mkurugenzi wa Miradi ya Ustawi ya Umoja wa Mataifa nchini Yemen amesema kuwa, kila dakika 12 mtoto mmoja mwenye umri wa chini ya miaka mitano hufariki dunia huko Yemen.
Shirika la habari la FARS limemnukuu Achim Steiner akisema hayo jana Jumatano na kuongeza kuwa, takwimu hizo zinaonesha ni kiasi gani hali ya kibinadamu ni mbaya mno nchini Yemen kutokana na uvamizi wa muungano unaoongozwa na Saudi Arabia. Ameongeza kuwa, sehemu kubwa ya watoto wadogo wa Yemen wanafariki dunia kutokana na kukosa maji, chakula na madawa.
Kwa upande wake, Mark Lowcock, Naibu Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa katika masuala ya misaada ya kibinadamu alisema hivi karibuni kuwa, Yemen hivi sasa inakabiliwa na maafa mabaya zaidi ya kibinadamu kuliko wakati mwingine wowote katika historia yake yote.

Mwezi Machi 2015, Saudi Arabia kwa baraka kamili za mabeberu wa dunia hasa Marekani, Uingereza na Israel na kwa kushirikiana na baadhi ya nchi za Kiarabu hasa Umoja wa Falme za Kiarabu, iliunda muungano ulioanzisha uvamizi wa kikatili dhidi ya wananchi Waislamu wa Yemen. Uvamizi huo wa Saudia na wenzake huko Yemen umeshaua makumi ya maelfu ya watu na kuwafanya wakimbizi mamilioni ya wananchi wa nchi hiyo ya Kiarabu.
Uvamizi huo wa kikatili umezidi kuisababishia matatizo nchi maskini ya Yemen hasa upungufu mkubwa wa chakula, maji na madawa.
No comments:
Post a Comment
Tupia Comments👇