Baruapepe elfu tatu zilizotumwa kwa siri kwa aliyekuwa waziri wa mambo ya nje wa Marekani zimefichua namna Ufaransa ilivyohusika katika mauaji ya kiongozi wa zamani wa Libya Muammar Gaddafi.
Toleo la Jumapili la gazeti la Ra'yul-Yaum limeandika kuwa, kufichuliwa yaliyomo kwenye baruapepe hizo elfu tatu za siri kumeonyesha kuwa hamu ambayo Ufaransa ilikuwa nayo ya kulinda na kuendeleza ubeberu wake wa kifedha barani Afrika na kupata hisa kubwa zaidi katika uzalishaji wa mafuta ya Libya iliifanya nchi hiyo ilitumie shirika la kijeshi la NATO kama wenzo wa kumpindua Gaddafi.
Baruapepe hizo zilitumwa mwezi Aprili mwaka 2011 kwa waziri wa mambo ya nje wa Marekani wakati huo Hillary Clinton.
Ndani ya baruapepe hizo yalitajwa malengo matano ya aliyekuwa rais wa Ufaransa wakati huo Nicolas Sarkozy ya kuishambulia kijeshi Libya, ambayo ni: Kupata mafuta ya Libya, kuhakikisha Ufaransa inaendelea kuwa na satua na ushawishi katika eneo, kuimarisha nafasi ya Sarkozy mwenyewe, kutilia mkazo nguvu za kijeshi za Ufaransa na kuzuia taathira na ushawishi wa Gaddafi magharibi mwa Afrika.
Muammar Gadafi aliuawa mwaka 2011 kufuatia uvamizi wa madola ya Magharibi yakiongozwa na Marekani nchini Libya kupitia shirika la kijeshi la NATO.
Tangu wakati huo hadi sasa nchi hiyo inaendelea kushuhudia machafuko na mapigano na kuvurugika amani na uthabiti wa kisiasa.../
No comments:
Post a Comment
MAONI (COMMENTS)👇