Rais Cyril Ramaphosa wa Afrika Kusini ametangaza sababu zilizomfanya aitishe kikao maalumu cha Bunge akisisitiza kuwa, mgogoro wa kuteswa na kunyanyaswa kupindukia wanawake nchini humo ndiko kulimlazimisha aitishe kikao hicho.
Alisema: Nimeitisha kikao hiki maalumu cha pamoja na Bunge kwa sababu nchi yetu hivi sasa imefunikwa na kiwingu kizito na cheusi cha ukandamizaji na mashambulizi makubwa dhidi ya wanawake. Rais huyo wa Afrika Kusini ameongeza kuwa, nchi yake ni moja ya nchi zisizo salama kabisa kwa wanawake duniani na kuongeza kuwa, kiwango cha ukandamizaji na unyanyasaji wa wanawake nchini Afrika Kusini ikilinganishwa na nchi nyingine duniani tunaweza kusema ni cha mazingira yanayowakumbwa wanawake wakati wa vita.
Rais Ramaphosa ameongeza kuwa, mwaka jana pekee wanawake 2,700 na zaidi ya watoto 1,000 waliuliwa katika matukio ya kutumia mabavu nchini Afrika Kusini. Amesema, kila siku jeshi la polisi la nchi hiyo linapokea zaidi ya kesi 100 za kunajisiwa wanawake nchini humo. Amesisitiza kuwa, kesi hizo hazijumuishi nyingine nyingi zaidi ambazo haziripotiwi kwa jeshi la polisi.
Takwimu zilizotolewa na idara ya takwimu ya Afrika Kusini (Statistics South Africa) zinaonesha kuwa, mmoja kati ya kila wanawake watano wenye umri wa zaidi ya miaka 18 nchini Afrika Kusini ameshawahi kunyanyaswa na kupigwa na mpenzi wake.
Hivi sasa serikali ya Afrika Kusini imeamua kuanzisha mpango mpya wa dharura utakaoanza kufanya kazi katika kipindi cha miezi sita ijayo ili kukabiliana na hali hiyo mbaya. Rais Ramaphosa aidha amesema, serikali yake imeamua kuanzisha kampeni kubwa ndani ya vyombo vya habari kwa ajili ya jamii mbalimbali, maeneo ya umma, maeneo ya kazi, vyuoni na mashuleni kama njia ya kupunguza kiwango kikubwa mno cha unyanyasaji na ukatili dhidi ya wananchi nchini Afrika Kusini.
No comments:
Post a Comment
ANDIKA MAONI (COMMENTS) HAPO👇