Naibu Kamanda Mkuu wa Jeshi la Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu ya Iran (SEPAH) amesema kuwa, uamuzi wa Marekani wa kuliweka Jeshi la Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu katika orodha ya makundi yake ya kigaidi ni wa kipumbavu na usio kuwa na maana.
Brigedia Jenerali Hussein Salami alisema hayo jana Jumamosi katika radiamali yake kwa hatua ya kiuhasama iliyochukuliwa Jumatatu iliyopita na Rais Donald Trump wa Marekani, ya kuliweka Jeshi la Iran la Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu katika orodha yake ya makundi ya kigaidi.
Amesema ni kichekesho kwa Marekani kuchukua hatua kama hiyo ya kijinga, katika hali ambayo yenyewe ni muungaji mkono mkubwa wa ugaidi, sambamba na kuunga mkono ukandamizaji na utesaji, licha ya kujipiga kifua na kudai kuwa ndiye mtetezi wa demokrasia duniani.
Naibu Kamanda Mkuu wa Jeshi la IRGC amesema kuwa, Jamhuri ya Kiislamu imeonyesha kuwa ina uwezo na nguvu za kuushinda ustikabari wa kimataifa katika nyuga mbalimbali na ndiposa Marekani inekerwa na kutia kiwewe na ushawishi wa Iran kieneo na kimataifa.
Amesisitiza kwamba, tangazo hilo la Rais wa Marekani, Donald Trump dhidi ya SEPAH linaonyesha kukata tamaa na woga wa hali ya juu ilionao nchi hiyo katika kukabiliana kijeshi na Jamhuri ya Kiislamu ya Iran.
Uamuzi huo wa Trump umechukuliwa ikiwa ni katika kuendeleza uhasama dhidi ya Iran na ni mashinikizo dhidi ya vikosi ambavyo, kwa kupambana na makundi ya kigaidi, vimefelisha stratijia ya Washington katika eneo.
No comments:
Post a Comment
MAONI (COMMENTS)👇