LATEST HEADLINES👉

Your Ad Spot

Mar 29, 2019

MAHAKAMA KUU YAMKUTA NA HATIA NASSARI, YATUPILIA MBALI KESI ALIYOTAKA AREJESHEWE UBUNGE


Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dodoma, leo tarehe 29 Machi, 2019 imetoa Uamuzi wa kuifuta kesi Na. 22 ya Mwaka 2019 iliyofunguliwa na Joshua Nassari aliyekuwa Mbunge wa jimbo la Arumeru Mashariki kutaka arejeshewe Ubunge wake na imemuamuru alipe gharama za kesi hiyo.

Katika Shauri hilo Joshua Nassari alimshtaki Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwa madai kuwa Spika ametoa uamuzi wa kumvua ubunge wake isivyo halali.

Uamuzi wa Mahakama wa kuifuta kesi hiyo umefikiwa baada ya Serikali kupitia Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali kuweka Mapingamizi ya Kisheria kutokana na kesi hiyo kukiuka misingi ya kisheria hivyo Wakili Mkuu aliomba kesi hiyo itupiliwe mbali na Nassari alipe gharama za kesi.

Misingi iliyozingatiwa na Mahakama kutupilia mbali kesi hiyo ni:

• Haikuwa sahihi kumshtaki Mheshimiwa Spika kwa kuwa hakumvua Nassari ubunge wake bali aliijulisha Tume ya Uchaguzi kuwa nafasi ya Mbunge wa Jimbo la Arumeru Mashariki ipo wazi kutokana na kitendo cha Joshua Nassari kushindwa kuhudhuria vikao vya Bunge vitatu mfululizo bila kuomba wala kupewa ruhusa ya maandishi ya Spika.

• Hati ya Kiapo cha Joshua Nassari kilichowasilishwa Mahakamani kilikuwa na dosari za kisheria kutokana na kiapo hicho kushuhudiwa na Wakili aliyekuwa anamuwakilisha Mahakamani jambo ambalo ni kinyume na sheria inayisimamia usimamizi wa viapo.

 • Joshua Nassari hakuwasilisha mahakamani uamuzi wowote anaoulalamikia kwamba umetolewa na Mheshimiwa Spika bali aliambatisha Taarifa kwa Umma iliyotolewa na KItengo cha Mawasiliano na uhusiano wa kimataifa - Bunge iliyofahamisha Umma kuwa Mheshimiwa Spika amemtaarifu mwenyekiti wa Tume kuwa

 “Ubunge wa Joshua Nassari umekoma kutokana na kushindwa kuhudhuria mikutano ya Bunge.”

Vile vile mahakama imeeleza kuwa, iwapo Joshua Nassari anaamini kuwa Spika ametoa uamuzi dhidi yake basi anayo fursa ya kukata rufaa dhidi ya uamuzi anaoulalamikia kwa mujibu wa kanuni ya 5(4) ya Kanuni za Kudumu za Bunge, 2016 kwa kuwasilisha malalamiko hayo kwa Katibu wa Bunge ili yafanyiwe kazi na Kamati ya Kanuni.

Baada ya kusikiliza Hoja za pande zote, Mahakama imeyakubali Mapingamizi yote ya Mawakili wa Serikali na kuamua kutupilia mbali kesi iliyofunguliwa na Joshua Nassari na kumtaka alipep gharama za kesi. Imetolewa na: Kitengo cha Mawasiliano na Uhusiano wa Kimataifa

No comments:

Post a Comment

MAONI (COMMENTS)👇

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages