LATEST HEADLINES👉

Your Ad Spot

Aug 20, 2018

KATIBU MKUU CCM ATOA ONYO KWA WATAKAO HUJUMU MALI ZA CHAMA

NA IS-HAKA OMAR, ZANZIBAR.
KATIBU Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Tanzania Dk.Bashiru Ally amesema Chama hicho kinadhibiti mianya ya ubadhilifu wa rasilimali fedha na mali zake ili kijitegemee kiuchumi.

 Alisema endapo rasilimali hizo zitatumika vizuri na kuanzishwa kwa miradi mingine mikubwa ya uzalishaji wa kipato katika ngazi mbali mbali za chama na jumuiya kwa  kuwanufaisha  wanachama wote badala ya watu wachache.

Kauli hiyo aliitoa jana katika mwendelezo wa ziara yake kisiwani Pemba wakati akizungumza na viongozi na wanachama wa Chama cha Mapinduzi wa Mikoa Miwili katika ukumbi wa Fidel Castro uliopo, Mkoa wa Kusini Pemba.

Dk.Bashiru alieleza kuwa lengo la kusimamia dhana ya ukuaji wa uchumi ndani ya chama kupitia vyanzo vyake vya mali na fedha ni kukiondosha chama katika mazoea ya kutegemea ufadhili wa watu wenye fedha wanaokuwa na malengo ya kujinufaisha wenyewe kisiasa.

Pia aliyataja malengo mengine kuwa ni uimarishaji wa maslahi ya watumishi wa CCM na jumuiya zake kwani bado maslahi yao ni ya kiwango cha chini ambayo hayaendani na hadhi ya taasisi yenyewe.

“ Kwa miaka mingi chama chetu kimeondoka katika misingi ya kujitegemea na badala yake kujitokeza kwa watu wenye fedha kukichangia chama wakati wa uchaguzi na mazoezi mengine ya kitaasisi, sasa katika mageuzi haya ya kimuundo tuna dhamira ya chama chetu kukiondosha uko na tukaweza kutumia mali zetu wenyewe kujiendesha kitaasisi.” Alifafanua Dk.Bashiru.

Alieleza kuwa malengo hayo yakifanikiwa utakuwa ni ushindi mkubwa kwa wanachama wa CCM wote kwani tabia za rushwa na makundi ya kusaka nafasi za uongozi kwa kutumia fedha yatakuwa yamedhibitiwa.

Aliwataka viongozi wote wa taasisi hiyo kuunga mkono malengo hayo kwa kuhakikisha wanapunguza matumizi holela ya fedha na badala yake waanzishe miradi itakayowasaidia kujiendesha ili kulinda heshima na hadhi ya CCM mbele ya jamii.

Pamoja na hayo alizitaka jumuiya zote hasa ya umoja wa vijana (UVCCM) kuhakikisha wanakuwa wabunifu kwa kutumia rasilimia walizonazo kwa kuanzisha miradi mikubwa ya kilimo, uvuvi na viwanda vidogo vidogo ili vijana wajiajiri wenyewe.

Katibu Mkuu huyo Dk.Bashiru aliweka wazi msimamo wa Chama Cha Mapinduzi kuwa wale wote waliohusika na kutapeli na kujimilikisha mali za taasisi hiyo kinyume na utaratibu wote watachukuliwa hatua za kisheria.

Naye Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar Dk.Abdulla Juma Mabodi alisema wanachama wote wana haki ya kuunga mkono mambo mema yanayotekelezwa na taasisi hiyo kwa nia ya kuongeza ufanisi.

Alisema wakati wa vyama vya ukombozi vya ASP na TANU viongozi wa wakati huo walifanikiwa kupanga mambo ya maendeleo yaliyodumu kwa muda mrefu kutokana na umoja na mshikamano waliokuwa nao hasa katika masuala ya kuvijenga kimaendeleo vyama vyao.

Dk. Mabodi alieleza kuwa suala la uzalendo katika kusimamia maslahi ya kitaifa ni jambo muhimu hasa kwa viongozi wanaoaminiwa na kupewa dhamana za kuongoza jamii.

Akizungumzia ushindi wa CCM visiwani Zanzibar mwaka 2020 alisema mpaka sasa Zanzibar hakuna upinzani bali kuna vikundi vidogo vidogo vya watu wanaojivisha joho la upinzani wakati wao ni madalali wa kisiasa waliofilisika kifikra.

Naibu Katibu Mkuu huyo alisema CCM itashinda kisayansi kutokana na serikali zake kutekeleza mahitaji ya wananchi wa mijini na vijijini kupitia utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya mwaka 2015/2020.

No comments:

Post a Comment

ANDIKA MAONI (COMMENTS) HAPO👇

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages