Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira na Mahusiano Deus Sangu amesema mahusiano mema, mazungumzo ya kujenga na mshikamano wa kitaifa ni nguzo muhimu katika kuimarisha demokrasia, amani na maendeleo endelevu nchini.
Akifungua Warsha ya Viongozi wa Vyama vya Siasa na Wajumbe wa Baraza la Vyama vya Siasa leo Juni 17, 2026, mjini Morogoro, Waziri Sangu alisema Serikali itaendelea kushirikiana na wadau wote wa kisiasa kwa kuzingatia misingi ya kuheshimiana, ushirikishwaji na kutanguliza maslahi ya Taifa.
Alisema viongozi wa vyama vya siasa wanapaswa kuwa mstari wa mbele kuhamasisha mazungumzo yenye kujenga, kudumisha amani na kuimarisha mshikamano wa kitaifa badala ya kuhimiza migogoro.
“Mahusiano mema ndiyo msingi wa amani, umoja na maendeleo ya Taifa. Tunaposhirikiana kwa heshima na maelewano bila kujali tofauti zetu za kiitikadi, tunajenga Taifa imara lenye mshikamano,” alisema Waziri Sangu.
Aidha, aliwataka viongozi hao kushirikiana na Serikali katika utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 itakayoanza kutekelezwa Julai Mosi, 2026, akieleza kuwa mafanikio ya dira hiyo yanategemea ushirikiano wa wadau wote wa maendeleo bila kujali tofauti za kisiasa.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Baraza la Vyama vya Siasa nchini, Juma Ali Khatibu alisema uwepo wa vyama vya siasa unatoa mchango mkubwa katika kuimarisha mahusiano na mshikamano ndani ya jamii.
Pia alimpongeza Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kumteua Dkt. Eveline Munisi wa Chama cha NCCR-Mageuzi kuwa Mbunge na Naibu Waziri katika Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira na Mahusiano, akisema hatua hiyo ni ishara ya kuendelea kuimarika kwa ushirikiano na maridhiano ya kisiasa nchini.
Vyama vya Siasa vilivyoshiriki ni CCM, CUF,UMD, NCCR-Mageuzi, NLD, UPDP, NRA,ADA TADEA, TLP,UDP,MAKINI, SAU,AAFP, CCK, ADC,CHAUMA na ACT Wazalendo.



No comments:
Post a Comment
Tupia Comments👇