Chuo Kikuu cha Afya na Sayansi Shirikishi Muhimbili (MUHAS), kupitia Shule ya Tiba ya Meno, juzi Mei 29, 2026, kiliwakaribisha wajumbe kutoka Chama cha Madaktari wa Meno Tanzania (TDA) pamoja na Shirikisho la Madaktari wa Meno Duniani ( World Dental Federation) katika juhudi za kuimarisha ushirikiano katika elimu ya tiba ya meno na maendeleo ya taaluma hiyo.
Ziara hiyo iliwakutanisha wataalamu wa tiba ya meno, wahadhiri, pamoja na wanafunzi kwa ajili ya kujadili fursa za ushirikiano katika mafunzo, utafiti, na kujengeana uwezo ndani ya sekta ya afya ya meno.
Akizungumza wakati wa mkutano huo, Mkuu wa Shule ya Tiba ya Meno MUHAS, Dkt. Ferdinand Machibya, alimkaribisha Rais wa Shirikisho la Madaktari wa Meno Duniani (FDI), Prof. Nikolai Sharkov, chuoni hapo. Alieleza kuwa ziara hiyo inaonesha kuongezeka kwa ushirikiano kati ya MUHAS na washirika wa kimataifa katika kuendeleza elimu ya tiba ya meno na huduma za afya.
Dkt. Machibya alisema kuwa MUHAS inaendelea kuwa na mchango mkubwa katika kuzalisha wataalamu wenye ujuzi kupitia ufundishaji, utafiti, pamoja na huduma za ushauri wa kitaalamu. Aliongeza kuwa Shule ya Tiba ya Meno imekuwa ikivutia wanafunzi wa shahada za uzamili na wataalamu kutoka nchi mbalimbali wanaojiunga na chuo hicho kwa ajili ya mafunzo maalum na kozi fupi za afya.
Katika ziara hiyo, Prof. Nikolai Sharkov aliipongeza Shule ya Tiba ya Meno ya MUHAS kwa mchango wake katika sayansi ya afya ya kinywa na meno, na kuisifu shule hiyo kwa kuwa Kituo Bora cha Umahiri katika Sayansi ya Afya ya Kinywa na Meno Afrika Mashariki.
Kwa upande wake, Prof. Sharkov pia aliipongeza MUHAS pamoja na Chama cha Madaktari wa Meno Tanzania kwa mchango wao katika kuimarisha huduma za afya ya meno na kuzalisha wataalamu wenye sifa nchini Tanzania.
Aidha, aliwahimiza wanafunzi wa tiba ya meno kuendelea kuwa makini katika masomo yao na kukuza taaluma zao ili waweze kuchangia ipasavyo katika mustakabali wa huduma za afya ya kinywa na meno.
Tukio hilo lilifanyika katika Shule ya Tiba ya Meno MUHAS na kuhudhuriwa na viongozi wa Chama cha Madaktari wa Meno Tanzania, madaktari wa meno wa kanda mbalimbali, wahadhiri wa MUHAS, pamoja na wanafunzi.

No comments:
Post a Comment
Tupia Comments👇