Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,Dkt. Samia Suluhu Hassan kupitia Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia imetoa shilingi 48,469,498,473/= kwa Chuo cha Uhasibu Arusha (IAA) kupitia Mradi wa Elimu ya Juu kwa Mageuzi ya Kiuchumi (HEET),kwa ajili ya kuboresha utekelezaji wa majukumu yake ya msingi ya kutoa mafunzo, kufanya tafiti na kutoa ushauri wa kitaalam.
Kiasi hicho cha fedha kimetangazwa na Mkuu wa Chuo cha Uhasibu Arusha (IAA), Prof. Eliamani Sedoyeka, alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari kuhusu miradi ya maendeleo na fursa kwa vijana leo Februari 20, 2026, katika ukumbi wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mtumba jijini Dodoma.
Ametaja maeneo ya kipaumbele ya utekelezaji wa mradi huo kuwa ni; ujenzi na uboreshaji wa miundombinu, kufanya mapitio ya mitaala kuendana na mahitaji ya soko la ajira, kuimarisha uhusiano na sekta binafsi, kuimarisha matumizi ya teknolojia na kuimarisha miundombinu ya TEHAMA na kuwajengea uwezo wafanyakazi.
Aidha, Prof. Sedoyeka ameelezea moja ya mafanikio ya chuo hicho kuwa ni uatamizi wa zaidi ya vijana 8600 kati yao vijana 1520 wakibuni mawazo mbalimbali ya biashara na kufanikiwa kuanzisha biashara zaidi ya 50 ambapo katika hizo kampuni 12 zilisajiliwa.
"Makampuni yaliyoanzishwa na kusajiliwa yamejikita katika maeneo ya biashara,ubunifu katika teknolojia, sanaa, uhifadhi,uhifadhi wa mazingira na maeneo mengine ambayo yametoa nafasi kwa wanafunzi wetu kujiajiri wenyewe na kuajiri vijana wenzao," amesema Prof. Sedoyeka.
Mkuu wa Chuo cha Uhasibu Arusha(IAA), Prof. Eliamani Sedoyeka, akizungumza na waandishi wa habari katika mkutano huo.
Wanahabari wakiwa katika mkutano huo.
Prof. Sedoyeka akitoka ukumbini baada ya kumaliza mkutano huku akisindikizwa na Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Habari MAELEZO, Kelvin Kinje aliyeuongoza mkutano huo.
No comments:
Post a Comment
Tupia Comments👇