LATEST HEADLINES👉

Your Ad Spot

Sep 14, 2024

KIHULLA: WMA TUTAONGEZA GAWIO KUTOKA BILIONI 4.3 HADI KUFIKIA BILIONI 7.7, SHERIA YETU INARANDANA NA QUR-AN NA BIBLIA

CCM's Official Blog, Dar es Salaam
WAKALA wa Vipimo Tanzania (WMA) imesema imejipanga kuongeza mchango wake katika Mfuko Mkuu wa Serikali  kutoka Sh, Bilioni 4.3 ilizochangia katika mwaka wa fedha wa 2022/2023 hadi kufikia gawio la Sh. Bilioni 7.7  mwaka huu wa fedha wa 2023/24.

Imesema, ikiwa kati ya taasisi 258 za Umma, Juni 11, 2024 ilipata tuzo kama taasisi bora inayochangia kwa wakati katika Mfuko Mkuu wa Serikali, ambapo katika mwaka wa fedha 2022/2023 taasisi hiyo ilitoa Gawio la Sh. Bilioni 4.3.

Hayo yalisemwa na Mtendaji Mkuu wa WMA Alban Kihulla, wakati akitoa wasilisho lake kuhusu mafanikio ya utekelezaji wa majukumu ya WMA katika kikaokazi baina yake na wahariri  na Waandishi wa habari, kilichoratibiwa na Ofisi ya Msajili wa Hazina kilichofanyika Septemba 11, 2024, jijini Dar es Salaam..

“Tunafanya hivi tukizingatia Ilani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) na sababu ni lazima tuangalie mipango ya maendeleo ya nchi iilivyo na hivyo WMA inao wajibu wa kuchangia kwa wakati ili kuiwezesha serikali kutekeleza mipango iliyojiwekea.” akasema Kihulla.

Akizungumzia majukumu ya WMA, Kihulla amesema inahusika sio tu na mizani za kupima uzito bali inahusika na Vipimo kwa ujumla wake na majukumu yake ni pamoja na kumlinda mlaji katika Sekta ya Biashara, Usalama, Mazingira na Afya kupitia matumizi ya vipimo sahihi.

Kihulla akasema,  WMA pia inao wajibu wa kusimamia na kutoa ushauri wa kitaalamu kwa wanaojihusisha na utengenezaji, uundaji, na uingizaji wa vipimo mbalimbali katika Biashara, Usalama, Mazingira na Afya ili kuwa kiungo kati ya taifa na taasisi za kikanda na Kimataifa katika masuala ya Vipimo (Legal Metrology).

Majukumu mengine ametaja kuwa ni kuhakikisha vifaa vyote vitumikavyo nchini kama standards za vipimo vinaulinganisho sahihi na ule wa Kimataifa, Kukagua na kuhakiki bidhaa zilizofungashwa (Net quantity & labeling) na kutoa elimu na ushauri wa kitaalamu kuhusu masuala ya vipimo kwa wadau.

Aidha Kihulla amesema WMA, Kihulla, yapo maeneo 17 ambayo sekta binafsi inaweza kushirikiana na WMA ili kuongeza tija katika sekta ya vipimo huku akitoa mwito kwa taasisi, asasi na mashirika binafsi kuimarisha ushirikiano na wakala hiyo katika masuala yanayohusu vipimo kwa nyanja za biashara, afya, usalama na mazingira.

Kihula akitaja baadhi ya maeneo hayo ya kivipimo kuwa ni ukaguzi na uhakiki wa mizani, uhakiki wa mitambo ya gesi, dira za maji zilizoko kwenye matumizi, mashine za michezo ya kubahatisha na lifti za majengo.

Kuhusu sheria inayoipa mamlaka WMA kutekeleza majukumu yake, Kihula alisema sheria hiyo ambayo msingi wake hasa ni vitabu vitakatifu vya dini, hususa vya Quran na Biblia, ni ya Usimamizi wa Vipimo Sura Namba 245 na 340 ya Mwaka 2002 ambayo inawatambua maafisa vipimo kama wakaguzi wanapotekeleza majukumu ya ukaguzi na uhakiki wa vipimo.

Alibainisha kuwa jukumu kubwa la WMA ni kuilinda jamii ili kuepukana na madhara yatokanayo na matokeo ya upimaji usio sahihi katika biashara ambapo WMA inawajibika kukagua sehemu za biashara kama vile maduka ya kuuzia bidhaa mbalimbali, viwanda, maduka ya vifaa vya ujenzi, vituo vya kujazia mafuta na sehemu nyinginezo.

“Tunasisitiza kila mara kwa wananchi kuwa, ukihisi kwamba umepimiwa visivyo sahihi katika sehemu uliyoenda kupata huduma, ni jukumu lako kutoa taarifa ili wataalamu wetu wakafanye uchunguzi eneo hilo,” alisema.

Mtendaji huyo mkuu aliongeza kuwa WMA inawajibika kuhakiki mzunguko mzima wa mafuta kuanzia yanapoingia nchini kupitia bandari, uhakiki wa matangi na maghala ya kuhifadhia mafuta na wakala hufanya shughuli hizo kupitia kitengo maalum cha bandari.

Sambamba na hayo, Kihulla alibainisha kwamba WMA ina mpango wa kuingia kwenye maeneo mapya ya uhakiki wa vipimo kama vile uhakiki wa gharama za vifurushi vya muda wa maongezi na mashine za michezo ya kubashiri.

Mpango mwingine, alisema ni kutoa elimu kwa wananchi na wadau wa vipimo kuhusiana na matakwa ya sheria ya vipimo, kuendelea kuboresha mifumo ya utendaji kazi pamoja na kuwajengea uwezo zaidi wataalamu wake ikiwa ni kuwapa mafunzo zaidi na ununuzi wa vifaa vya kisasa.

Mwenyekiti wa Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF), Deodatus Balile ameipongeza WMA kutokana na utendaji kazi wake na ameahidi ushirikiano wa vyombo vya habari na Wakala hiyo ili kuhakikisha elimu ya matumizi sahihi ya vipimo inawafikia wananchi kwa ukubwa wake.

“WMA mna nafasi ya kuufikia umma wa watanzania kwa kutumia vyombo vya habari kwenye kampeni hizi za kivipimo, elimu inahitajika sana, wananchi wanatakiwa kufahamu kwamba wanapaswa kuwa makini wanapokwenda kupata huduma mbalimbali, hii itachagiza maendeleo katika taifa letu” alisema.
Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Vipimo (WMA) Alban Kihulla, akitoa wasilisho lake kuhusu mafanikio ya utekelezaji wa majukumu ya WMA katika kikaokazi baina yake na wahariri  na Waandishi wa habari, kilichoratibiwa na Ofisi ya Msajili wa Hazina kilichofanyika Septemba 11, 2024, jijini Dar es Salaam.

No comments:

Post a Comment

MAONI (COMMENTS)👇

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages