LATEST HEADLINES👉

Your Ad Spot

Dec 29, 2023

TET YAANDAA MAFUNZO KUWAJENGEA UWEZO WAWEZESHAJI WA WALIMU SHULE BINAFSI KATIKA UTEKELEZAJI MITAALA ILIYOBORESHWA

Official CCM Blog, Dar es Salaam
TAASISI ya Elimu Tanzania (TET) imeandaa mafunzo ya kuwajengea uwezo wawezeshaji wa walimu wa shule binafsi katika kutekeleza mitaala iliyoboreshwa, mafunzo ambayo yatafanyika kwa siku mbili katika Ukumbi wa Shule ya Msingi ya Bernard Bendel, Kola B, mkoani Morogoro, kuanzia Januari 2, 2023.

Utoaji mafunzo hayo ni miongoni mwa maazimio ya kikao kati ya TET na viongozi wa taasisi zinazosimamia shule zisizo za serikali (ambrela organisation) kilichofanyika katika Ukumbi wa TET Jijini Dar es Salaam, leo Disemba 29, 2023, kikiongozwa na Kamishna wa Elimu, Wizara ya Elimu Sayansi na Teknolojia Dk. Lyabwene Mtahabwa ambaye alishiriki kwa njia ya mtandao.

Baada ya mjadala mpana wa mambo mbalimbali kikao hicho kiliazimia kuwa kila taasisi itoe inayosimamia shule binafsi itoe walimu kumi (10) watakaopata mafunzo kuhusu utekelezaji wa mtaala ulioboreshwa wa mwaka 2023.

"Walimu hawa watakuwa ni sehemu ya wawezeshaji kwa walimu wengine katika shule zilizochini ya taasisi hizo. TET inatarajia kutoa mafunzo kabilishi kwa walimu hao tarehe 2–3 Januari 2024 katika ukumbi wa Shule ya Msingi ya Bernard Bendel, Kola B, Morogoro".

Ninaandika barua hii, kukuomba kuteua washiriki kumi (10) watakaowezeshwa namna ya utekelezaji wa mtaala ulioboreshwa na uendeshaji wa Mafunzo Endelevu ya Walimu Kazini (MEWAKA) ikiwemo mfumo wa ujifunzaji kimtandao (Learning Management System)", ameeleza Mkurugenzi Mkuu wa TET Dk. Aneth Komba katika barua kwa Viongozi wakuu wa Taasisi hizo zinazosimamia shule binafsi.

Dk. Aneth ameeleza kuwa kila mshiriki katika mafunzo hayo anatakiwa kwenda na kishikwambi au kompyuta atakayotumia wakati wa mafunzo na kueleza kuwa TET itagharimia wawezeshaji, ukumbi na chakula wakati wa mafunzo kwa washiriki wote lakini gharama za malazi na usafiri itakuwa ni jukumu la taasisi zinazomiliki shule.

Taasisi zilizopewa mwaliko kuandaa walimu watakaoshirii mafunzo hayo ni Jumuiya ya Wazazi Tanzania (CCM), Baraza Kuu la Waislamu Tanzania (BAKWATA), Tume ya Kikristo ya Huduma za Jamii Tanzania (CSSC) na Tanzania Association of Private Investors (TAPIE).

Nyingine ni Baraza la Sunnah Tanzania (BASUTA), Mtandao wa Elimu Tanzania (TENMET), Tanzania Association of Women Owners of Schools & Colleges (TAWOSCO) Tanzania School Empowerment and Service Organization (TASESO) na Shirikisho la Wamiliki na Mameneja wa Shule na Vyuo Visivyo vya Serikali (TAMONGSCO).

No comments:

Post a Comment

MAONI (COMMENTS)👇

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages