LATEST HEADLINES👉

Your Ad Spot

Feb 21, 2023

NJAA YAMUIBUA MTUHUMIWA WA MAUAJI YA MKE WA MWENYEKITI KAGERA.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kagera ACP William Mwampagale akizungumzia tukio la kukamatwa kwa mtuhumiwa wa mauaji.


Na Lydia Lugakila, Bukoba


Jeshi la Polisi Mkoa wa Kagera limefanikiwa kumkamata mtuhumiwa wa mauaji aliyetambulika kwa jina la Paschal Kaigwa Mariseli (21) mzaliwa wa Kijiji cha Katerero, Kata ya Kishogo, Wilaya ya Bukoba aliyekuwa akiishi na Mwenyekiti wa mtaa wa National Housing Kata Rwamishenye Manispaa ya Bukoba Mkoani Kagera.


Kijana huyo  amekuwa akitafutwa na Jeshi la Polisi Mkoani Kagera kwa kushirikiana na Wananchi ambao wamekuwa wakimsaka Kijana huyo kila chocho baada ya kutekeleza mauaji ya Bi Khadija Ismail (29) ambaye alikuwa ni Mke wa Mwenyekiti wa mtaa wa National Housing Kata Rwamishenye  mnamo Februari 13, 2023 majira ya saa 12 na nusu jioni kwa kumpiga na ubao kisha Kumbaka na  kutokomea kusiko julikana.


Akiongea na Waandishi wa Habari leo Februari 21, 2023 Kamanda wa Polisi Mkoani Kagera ACP William Mwampagale amesema mtuhumiwa huyo  kwa kipindi alichotoweka alikwenda kujficha vichakani na ndipo  Februari 19, 2023 majira ya saa 10 jioni aliamua kutoka mafichoni baada ya kuhisi njaa kali.


Kamanda amesema baada ya kuhisi hali hiyo aliamua kwenda kutafuta msaada wa chakula nyumbani kwa Shangazi yake katika mtaa wa Kashai  Manispaa ya Bukoba na baadae kukutana na watoto wa Shangazi yake ndipo Majirani wakamtambua na kisha kupiga Kelele na na kufanikiwa kumkamata.


Aidha Kamanda Mwampagale amewashukuru Wananchi wote Mkoani humo kuendelea kutoa ushirikiano Katika kuwafichua  wahalifu.


Hata hivyo ametoa onyo kwa wote wanaojihusisha na vitendo mbali mbali vya uhalifu ikiwemo mauaji, ubakaji na ukatili  kuacha mara moja.

No comments:

Post a Comment

MAONI (COMMENTS)👇

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages