LATEST HEADLINES👉

Your Ad Spot

May 21, 2022

MFAHAMU GANGISA LUTENI KANALI MSTAAFU ALIYEFANYAKAZI NA IDD AMIN WA UGANDA KWA MIAKA MITATU




Tanzania haitamsahau Dikteta Idd Amini Dada aliyeitawala Uganda kwa mabavu kisha kuvamia Tanzania mwaka 1978 ambapo Tanzania iliingia vitani  na kufanikiwa kumng’oa mvamizi huyo mwaka 1979.

Luteni Kanali Mstaafu Daniel Gangisa ambaye hivi sasa ana umri wa miaka 96 anaishi Chandarua Manispaa ya Songea mkoani Ruvuma anasema Idd Amin anamfahamu vizuri kwa sababu  walisoma na kufanyakazi pamoja kwa miaka mitatu Nakuru nchini Kenya.

Gangisa alizawaliwa mwaka 1927 katika eneo la Ruhuwiko mjini Songea ambapo alijiunga na jeshi la wakoloni mwaka 1947 ambapo mwaka 1953 alikwenda chuo cha Jeshi Nakuru Nchini Kenya ili kupata mafunzo Zaidi ya kijeshi ambako alikutana na Dikteta Idi Amini.

“Nimesoma na Idd Amini miaka mitatu kuanzia 1953 hadi 1955 alikuwa rafiki yangu sana,tulikuwa tunalala chumba kimoja bwenini, baada ya kumaliza kozi  mimi na Amini tulipata alama za juu hivyo chuo kilitupa makataba wa kuwa walimu tulifanya kazi  sote tukiwa na cheo cha Sajenti kwa miaka mitatu’’,anasema Luteni Kanali Mstaafu Gangisa.

Hata hivyo Gangisa anasema licha ya Amini katika kipindi hicho kuonekana kuwa ni kijana mtulivu na ambaye hakuwa mgomvi sana isipokuwa alikuwa mpiganaji wa ngumi na kwamba Amin alimwomba Gangisa amfundishe ngumi,lakini alikataa.

Gangisa anasema kwa muda alioishi na Idd Amin aligundua dosari kubwa aliyokuwa nayo tangu kipindi hicho Dikteta Idd Amin alipenda sana vyeo hivyo hata aliposikia amepindua nchi hakushangaa kwa sababu alimfahamu.

Luteni Kanali Mstaafu Gangisa anasema baada ya kumaliza mkataba wa kufundisha Nakuru alirudi Nyeri nchini Kenya kambi yake ya Jeshi kuendelea na Vita ya Maumau kisha alikwenda kwenye vita nchini Mauritius na Idd Amin alirudi kwao Uganda ambapo mara ya mwisho kuonana na Idd Amin anasema ilikuwa mwaka 1960 nchini Kenya.

Anasema mwaka 1964 alishiriki katika kuunda  JWTZ Jeshi jipya lenye heshima nchini Tanzania na kwamba yeye ni miongoni mwa maafisa waliunda JWTZ ambapo yeye ni Ofisa wa 50 wakati huo akiwa na cheo cha Luteni Kanali.

Kwa mujibu wa Luteni Kanali Mstaafu huyo,Hayati Baba wa Taifa Mwl. Julius Nyerere wakati anaanza harakati za uhuru na kuunda chama cha TANU yeye alikuwa na Idd Amini Nakuru Kenya.

“Idd Amini ndiye aliyenipa taarifa kwamba wewe Mswahili  nyumbani kwako kuna bwana ameanzisha Chama cha kupigania uhuru,alinitisha kwamba Maumau itaamia kwenu,nikamwambia Mungu yupo,alikuwa anaongea Kiswahili kizuri,alikuwa rafiki yangu mkubwa sana’’,alisisitiza Gangisa.

Gangisa aliacha kazi ya JWTZ mwaka 1978,lakini baada ya kusikia Idd Amini amepindua nchi ya Uganda na kuvamia sehemu ya Kaskazini ya Tanzania aliamua kurudi jeshini kupambana na rafiki yake Idd Amin.

“Nilisema kama amevamia nchi yetu narudi jeshini,tulipambana naye,nilifika hadi kijijini kwake,Kampala pale alinusurika kuuawa, akatorokea njia ya Kenya,tuliwaomba Kenya wafunge mpaka walikataa hivyo Idd Amin akanusurika akatoroka ukiwa ndiyo mwisho wa Vita ya Uganda’’alisema.

Luteni Kanali Mstaafu Gangisa pia anasema alishirikiana na Samora Machel wa Msumbiji wakati wa harakati za kupigania Uhuru wa Msumbiji ambapo mara kadhaa amelala kwenye mashimo na Samora Machel.

Anasema Samora Machel mara baada ya Uhuru alifika Songea mwaka 1975 wakati anazungumza na wananchi alimshukuru Luteni Kanali Gangisa akisema alishiriki naye kwa kutoa silaha na walilala wote kwenye mashimo na kula mihogo ya watu wakati wa mapambano ya wareno.

Gangisa anatoa rai kwa serikali kuwakumbuka wastaafu waliolitumikia Taifa kwa uzalendo mkubwa ili kumalizia  kwa furaha maisha yaliobaki hapa duniani.

Imeandikwa na Albano Midelo

Kitengo cha Mawasiliano Serikalini Mkoa wa Ruvuma

Mei 21,2022

No comments:

Post a Comment

MAONI (COMMENTS)👇

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages