LATEST HEADLINES👉

Your Ad Spot

Jun 30, 2021

UWT DAR ES SALAAM KUKAMILISHA UJENZI WA NYUMBA ZA WATUMISHI WAKE NOVEMBA 2021, UJENZI KUGHARIMU KIASI CHA SH. BILIONI 1.3


Na Bashir Nkoromo, CCM Blog
Jumuiya ya Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT) ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Dar es Salaam, imepanga kukamilisha ujenzi wa nyumba kwa ajili ya Watumishi wake Novemba mwaka huu.

Katibu wa Jumuiya hiyo mkoa wa Dar es Salaam, Grace Haule amesema nyumba hizo zitakuwa 6, moja katika ngazi ya mkoa na nyingine moja moja katika kila wilaya zote katika mkoa huo.

Amesema ujenzi wa nyumba hizo utagharimu kiasi cha Sh. Bilioni 1.3, na tayari wamo katika  harakati za kukusanya fedha kwa ajili ya ujenzi, nguvu kubwa ikiwa kwenye kuchangishana Wanawake wenyewe katika vikao mbalimbali wanavyofanya kila Wilaya.

Grace amesema hayo, jana wakati wa mkutano wa Ziara ya Mwenyekiti wa UWT mkoa wa Dar es Salaam, Florence Masunga na Kamati ya Utekelezaji na Viongozi wa ngazi mbalimbali wa UWT na (CCM),  Wilaya ya Ubungo, uliofanyika katika Ukumbi wa Victory Geneses, Temboni wilayani humo.

"Tumeamua tuanze kuchangishana wenyewe kwenye mikutano ya ziara zetu, baadaye ndiyo tutashirikisha wadau wengine kutuchangia pale tutakapokuwa tumepelewa", amesema Grace.

Akizungumza na Wanachama, Watendaji na Viongozi wa UWT na CCM kwenye kikao hicho, Mwenyekiti wa UWT mkoa wa Dar es Salaam Florence Masunga, aliuelezea kwa kina mpango wa ujenzi wa nyumba hizo, akisema zitakuwa zenye hadhi ya kisasa na stahili bora kwa kuishi mtumishi wa Jumuiya hiyo.

Florence aliwataka Wanachama wa Jumuiya hiyo, kupambana katika uchangiaji fedha za ujenzi wa nyumba hizo ili kuudhihirishia umma kwamba Wanawake wanaweza na wakiwa na jambo lao haikwami.

Alisema, pamoja na lengo kuu la ziara zake katika wilaya zote kuwa ni kuhamasisha uchagiaji wa ujenzi wa nyumba hizo, lakini pia ni kuwahamasisha Wanawake kuzitumia fursa za mikopo zilizopo ili kuinua vipato vyao, familia zao na taifa kwa jumla.

"Katika hili natambua kuwa changomo kubwa iliyopo ni Wanawake wengi kutokuwa na maarifa ya kutosha kuhusu namna ya kuipata mikopo yenyewe na hata namna ya kuiendesha ili itoe tija kwa wake wanaokuwa wameipata.

Kwa hiyo, hivi karibuni nitafanya ziara zibgine katika wilya zote, kwa ajili ya kutoa semina kuhusu maarifa ya upatijanaji mikopo na namna ya kuziendeleza fedha za mikopo hiyo", amesema Florence.

Ziara ya jana Ubungo ilikuwa ni mwendelezo wa ziara kama hiyo ambazo ameshazifanya katika wilaya kadhaa, ikiwemo Temeke na Ilala, na kwa mujibu wa Mwenyekiti huyo, ziara hizo zitafanyika katika Wilaya zote.

Mwenyekiti wa UWT mkoa wa Dar es Salaam Florence Masunga akionesha mfano wa nyumba ambazo UWT itazijenga kwa ajili ya Watumishi wake, wakati wa mkutano wake
wa ziara yake na Kamati ya Utekelezaji na Viongozi wa ngazi mbalimbali wa UWT na (CCM),  Wilaya ya Ubungo, uliofanyika katika Ukumbi wa Victory Geneses, Temboni wilayani humo, jana. Kushoto ni Katibu wa UWT mkoa huo Grace Haule (Picha na Bashir Nkoromo)

No comments:

Post a Comment

ANDIKA MAONI (COMMENTS) HAPO👇

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages