LATEST HEADLINES👉

Your Ad Spot

Feb 17, 2021

MALAWI YAIPONGEZA TANZANIA URATIBU WA TAASISI ZISIZO ZA KISERIKALI (NGO)

 

Katibu Mkuu Wizara ya Afya-Idara Kuu ya Maendeleo ya Jamii Dkt. John jingu akifafanua jambo kwa ujumbe wa Jamhuri ya Malawi uliofanya ziara kwa lengo la kujifunza jinsi Serikali ya Tanzania inavyoratibu Mashirika yasiyo ya Kiserikali. Kushoto ni Waziri wa Jinsia, Maendeleo ya Jamii na Ustawi wa Jamii wa nchini Malawi Mhe. Patricia Kaliati.

Msajili wa Mashirika Yasiyo ya Kiserikali nchini Vickness Mayao akieleza jinsi Serikali inavyoratibu mashirika hayo nchini kwa ujumbe wa Jamhuri ya Malawi uliofanya ziara kwa lengo la kujifunza jinsi Serikali ya Tanzania inavyoratibu Mashirika Yasiyo ya Kiserikali. Ujumbe huo umeongozwa na Waziri wa Jinsia, Maendeleo ya Jamii na Ustawi wa Jamii wa nchini Malawi Mhe. Patricia Kaliati.
 Baadhi ya wawakilishi wa Jamhuri ya Malawi waliofanya ziara kwa lengo la kujifunza jinsi Serikali ya Tanzania inavyoratibu Mashirika Yasiyo ya Kiserikali. Waziri wa Jinsia, Maendeleo ya Jamii na Ustawi wa Jamii wa nchini Malawi Mhe. Patricia Kaliati ameongoza ziara hiyo.

************************

Na Mwandishi wetu, Dodoma

Serikali ya Malawi imepongeza Tanzania kwa jitihada zake za kuwaletea maendeleo Wananchi wake ikiwa ni pamoja na Uratibu wa Mashirika Yasiyo ya Kiserikali ili kuhakikisha yanachangia katika maendeleo ya Taifa.

Pongezi hizo zimetolewa jijini Dodoma na Waziri wa Jinsia, Maendeleo na Ustawi wa Jamii wa Malawi, Patricia Kaliati katika ziara ya Mafunzo kuhusu hatua zinazochukuliwa na vyombo vya uratibu na uendeshaji wa Mashirika Yasiyo ya Kiserikali nchini Tanzania (NGOs) na hivyo kufanikiwa katika mpango wa kuwawezesha Wananchi wake.

“Katika Utawala wa Serikali hii, Tanzania imepiga hatua kubwa ya Maendeleo katika shughuli mbalimbali ikiwa ni pamoja na utaribu wa kazi za Mashirika Yasiyo ya Kiserikali. Nasi tumekuja kujifunza njia gani mnazitumia kuratibu mashirika hayo na hatimaye kuchangia katika maendeleo ya Watanzania,” alisema Waziri Kaliati.

Akizungumza kwa niaba ya Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Dkt. Dorothy Gwajima, Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Dkt. John Jingu amesema Serikali imekuwa ikifanya mazungumzo ya mara kwa mara na Wadau mbalimbali yakiwemo Mashirika Yasiyo ya Kiserikali ili kuhakikisha shughuli zinazofanyika zinakuwa na mchango mkubwa kwa Jamii na taifa kwa ujumla.

Amefafanua kuwa Sheria ya Mashirika Yasiyo ya Kiserikali imefanyiwa mabadiliko kadhaa ili kuhakikisha Serikali na NGOs zinajenga uelewa wa pamoja kuhakikisha shughuli za Serikali zinawafikia Wananchi kwa malengo yaliyokusudiwa yanafikiwa.

“Ili kufanikisha mipango inayohusika kati ya Serikali na NGOs kuna mabadiliko mbalimbali katika sheria ya Mashirika Yasiyo ya Kiserikali ili kuhakikisha kwamba kunakuwa na uelewa wa pamoja na kuondoa malalamiko yanayoweza kujitokeza,” alisema Dkt. Jingu.

Amefafanua kuwa siri ya mafanikio yaliyofikiwa ni kufanya ufuatiliaji kuhakikisha kwamba NGO zinafanya kazi kwa mujibu wa Usajili wake na maendeleo yaliyokusudiwa yanawafikia Wananchi katika maeneo yao.

Akiwasilisha mada kuhusu uratibu na wajibu wa NGOs kwa jamii, Mwenyekiti wa Bodi ya Uratibu wa Mashirika Yasiyo ya Kiserikali, Dkt. Richard Sambaiga amesema jukumu na uratibu linahitaji umakini mkubwa ili kulinda maslahi ya taifa badala ya maslahi binafsi.

Hata hivyo, amesema wakati mwingine wakati wa mazungumzo yanaweza kutokea malalamiko kuwa NGOs zinabanwa lakini ukweli ni kwamba Bodi ya Uratibu pamoja na Msajili wa Mashirika Yasiyo ya Kiserikali wanawajibika kuhakikisha kwamba maslahi ya Taifa yanalindwa.

“Lazima kuhakikisha kwamba kila upande unafanya kazi kulingana na malengo yake ambayo yamewekwa vinginevyo mara chache utasikia malalamiko kwamba mashirika yanaminywa” alifafanua Dkt. Sambaiga.

Awali akiwasilisha mada kuhusu sera na mfumo na uratibu wa NGOs Tanzania bara, Msajili wa Mashirika Yasiyo ya Kiserikali, Vickness Mayao amesema utaratibu uliopo ni kuhakikisha kwamba kuna uwazi na uwajibikaji katika uendeshaji na uratibu wa mashirika hayo

Amesema matumizi ya mfumo wa kidigitali wa mawasiliano umerahisisha utendaji na kupunguza gharama za uendeshaji kutokana na shughuli zote kufanyika kwa njia ya mtandao.

Akichangia mada katika kikao hicho, Mbunge wa Viti Maalum anayeshughulikia Mashirika Yasiyo ya Kiserikali, Neema Lugangira amesema Bunge limekuwa likifanya kazi kwa kushirikisha makundi mbalimbali ili kuweka uwakilishi sawia.

Hata hivyo, amesema kumekuwa na upotoshaji kwa baadhi ya mashirika kukwepa kuwasilisha taarifa zake na wakati mwingine kuwasilisha taarifa zisizo sahihi kwa maslahi binafsi.

Ziara ya Waziri wa Jinsia, Maendeleo na Ustawi wa Jamii wa Malawi inahusisha Ujumbe wa watu wanane akiwemo Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Roselyn makhumula, Wabunge kutoka kamati inayoratibu mashirika Yasiyo ya Kiserikali na Wawakilishi wa Bodi ya Uratibu wa NGOs nchini Malawi.

No comments:

Post a Comment

MAONI (COMMENTS)👇

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages