LATEST HEADLINES👉

Your Ad Spot

Dec 14, 2020

AIRTEL TANZANIA NA TRC WAINGIA UBIA, SASA WASAFIRI WA TRENI WATAWEZA KULIPA NAULI KUPITIA AIRTEL MONEY

Dar es Salaam, Jumatatu, Disemba 14, 2020 

Kampuni ya simu za mkononi ya Airtel Tanzania imetangaza ushirikiano mpya na Shirika la Reli Tanzania kupitia huduma yake ya Airtel Money ambapo kuanzia sasa, wateja wao wataweza kununua tiketi za kusafiri wa treni kupitia akaunti zao za Airtel Money.


Kwa sasa, usafiri wa treni umekuwa ni mkombozi mkubwa kwa watanzania baada ya serikali ya awamu ya tano inayoongozwa na Rais, Dk. John Magufuli, kufanya kazi kubwa ya kuimarisha sekta ya miundombinu ya reli nchini kwa kukarabati reli ya kanda kaskazini (Tanga, Moshi, Arusha) na huduma hii inaanzia Dar es Salaam -Arusha.


Akizungumza jijini Dar es Salaam wakati wa kutangaza ushirikiano huo mpya, kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa Airtel Tanzania Mkurugenzi wa mawasiliano wa Airtel Beatrice Singano amesema kuwa Airtel Money imekuwa tayari kukaribisha ushirikiano wowote ambao unaongeza tija kwa wateja wake.


“Airtel Money Tunajisikia fahari sana kuingia katika ushirikiano mwingine na shirika letu la taifa la Reli Tanzania. Ubia huu utaongeza tija katika utoaji huduma zetu na hivyo kuwanufaisha wateja wetu wote.  Wateja wa TRC kwa sasa wataweza kulipia tiketi zao kupitia huduma yetu ya Airtel Money kwa uhuru kabisa. Naomba nitumie fursa hii kutoa rai kwa wateja wa Airtel kutumia huduma yetu ya Airtel Money ili kuokoa muda na kufanya malipo kwa njia rahisi na salama.


Tunaelewa ya kuwa hiki kipindi cha msimu wa sikukuu wateja wetu husafiri sana kwa ajili ya kwenda kukutana na familia, ndugu jamaa na marafiki kwa ajili ya kusherehekea sikukuu za Krismas na Mwaka Mpya. 

Ushirikiano huu utawapa unafuu kwani kwa sasa watakuwa na uhuru wa kulipia tiketi za usafiri wakiwa mahali popote pale bila kutembelea ofisi za TRC", alisema Singano  na kufafanua kuwa Mteja atakakiwa kupiga *150*60# kisha kwenda namba 5 Lipabili namba 5 tena Malipo ya Serikali kisha mteja ataingiza namba ya kumbukumbu aliyopata toka kwenye tovuti ya TRC na kufanya malipo papo hapo atahakikishiwa safari yake.


“Airtel Money kwa sasa imeunganishwa mtandao wa huduma kwa wateja wa Shirika la Reli Tanzania,kwa kuingia kwa tovuti ya TRC ambayo ni www.trc.co.tz, ili kukata tiketi kwa njia ya mtandao, ambapo kwa muunganiko huo  wateja wa Airtel Money wanaweza kulipia tiketi zao za TRC moja kwa moja kupitia akaunti za Airtel Money kwani ni njia salama, haraka na nafuu.

 

Airtel Tunaimani  ya kwamba kwa kupitia Airtel Money, tumeweza kuwarahisishia wasafiri kutotumia muda mwingi kutembelea ofisi za TRC kwa ajili ya kulipia tiketi zao, lakini kwa sasa ukiwa na Airtel Money, unauhakika kuwa siti yako imehifadhiwa kwa ajili yako", Singano aliongeza.


Akizungumza katika hafla hiyo, Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Reli Tanzania (RTC) Masanja Kadogosa alisema TRC daima inaendeleza ubunifu katika kutoa huduma bora, haraka na salama kwa wateja wetu wote kwa kuwa tunatambua umuhimu wa huduma zetu kwa jamii na ni usafiri wa gharama nafuu kuliko usafiri wowote .


Alisema ubia huo wa TRC na Airtel Tanzania utasaidia kuboresha zaidi utoaji huduma kwa wateja wanaotumia mtandao wakati wakulipia tiketi zao kwani ni rahisi kwenye kutumia na vile vile unaweza kujihudumia ukiwa popote na hivyo kuwahakikishia wateja huduma za uhakika na haraka za usafirishaji.


“Airtel Money ni moja ya njia rahisi na salama kwenye kufanya malipo kwa njia ya mtandao. Kwa kuwa sasa imeunganisha kwenye mtandao wetu wa malipo, wateja wetu watakuwa na uhuru wa kuchagua zaidi inapokuja suala la kulipia tiketi za usafirishaji”. Aliongezea ili kupata huduma hii wateja wanatakiwa kuingia kwa tovuti ya TRC, ambayo ni www.trc.co.tz, fungua kata tiketi kwa njia ya mtandao, unapoingia hapo utajaza kutokana ma maelekezo unapewa", alisema.


"Naendelea kuwasihi wateja wetu tukate tiketi kwa njia ya mtandao ambayo ni rahisi zaidi popote ulipo, maana ni inakupunguzia gharama na muda, huduma za usafiri  wa reli kwa njia kaskazini kutoka Dar es Salaam  kwenda Arusha ni siku ya Jumatatu, Jumatano na ijumaa, muda wa safari kuanzia sa 8:30 mchana na inafika Arusha sa 3:00 Asubuhi, na kutoka Arusha ni Siku ya Jumanne, Alhamisi na Jumamòsi, muda ni sa 8:30 mchana na kufika Daresalaam sa 3:00 Asubuhi, alisema Kadogosa.

Mkurugenzi wa Mawasiliano Airtel Tanzania Beatrice Singano akizungumza jijini Dar es Salaam mwishoni mwa wiki, kutangaza ushirikiano wa Mtandao huo wa simu za mkononi na Shirika la Reli Tanzania (TRC) ambapo sasa wateja wa mtandao huo wateweza kulipa nauli za usafiri wa treni kupitia Airtel Money. Kulia ni Mkurugenzi Mtendaji wa TRC Masanja Kadogosa.

Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Reli Tanzania (TRC) Masanja Kadogosa, akizungumza jijini Dar es Salaam mwishoni mwa wiki, kutangaza ushirikiano wa Shirika hilo na Airtel Tanzania, ambapo sasa wateja wa TRC wateweza kulipa nauli za usafiri wa treni kupitia Airtel Money. Kushoto ni Mkurugenzi Mtendaji wa Mawasiliano Airtel Tanzania Beatrice Singano.

No comments:

Post a Comment

MAONI (COMMENTS)👇

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages