LATEST HEADLINES👉

Your Ad Spot

Nov 18, 2020

KANISA HALISI: WATALII WENGINE HUJA KUSHANGAA UTAKATIFU WA TAIFA LA TANZANIA, LAANDAA UZINDUZI WA KITABU 'UFAHAMU ULIOANZIA TANZANIA KWENDA MATAIFA YOTE', DESEMBA 6, 2020


Kiongozi Mkuu wa Kanisa Halisi la Mungu Baba, Baba wa Uzao, akizungumza na Waandishi wa habari, katika Kanisa hilo, Tegeta Kibo, Jijini Dar es Salaam, leo, kuhusu Kanisa hilo kufanya uzinduzi wa Kitabu 'Ufahamu ulioanzia Tanzania kwenda Mataifa mengine yote' utakaoyafnyika Desemba 6, mwaka huu, katika Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam. Wapili kulia ni Mama wa Uzao na kulia ni Katibu wa Kanisa hilo.

Mwaliko kwa watu wote

Habari Kamili👇

Na CCM Blog, Tegeta

Kiongozi wa Kanisa Halisi la Mungu Baba, Baba Wa Uzao, amesema Watalii kutoka mataifa ya nje wanapokuwa hapa nchini wengine huwa siyo kwa lengo la kuona vivutio vya utalii tu kama wanyama bali huja kushanga pia utakatifu wa Taifa la Tanzania kama ambavyo watu mashuhuri na wasio Mashuhuri walivyokuwa wakienda kwenye miji mitakatifu ya Yerusalemu, Madina na Meka kuhiji au kuabudu.


Hayo yamesemwa leo na Baba wa Uzao kwenye Kanisa hilo, Tegeta jijini Dar es Salaam, wakati akieleza maandalizi ya Kanisa hilo kuhusu uzinduzi wa kitabu 'Ufahamu ulioanzia Tanzania Kwenda Mataifa yote'  utakaofanyika Desemba 6, 2020, katika Uwanja wa  Uhuru jijini Dar es Salaam, kuanzia saa 8 mchana hadi saa 11 jioni.


Amesema kutokana na umuhimu viongozi wote wa Kitaifa na kijamii, wakiwemo Wabunge wote, viongozi wote wa dini na madhehebu pamoja na huduma binafsi wamealikwa na Kanisa hilo kufika kushuhudia uzinduzi huo akisema  sababu ya kualika kila mtu ni kwa kuwa sio suala la kidini au dhehebu, bali ni suala la Maendeleo ya Kitaifa na Mataifa.


Tafadhali, soma tarifa kamili kama ilivyotayarishwa na Baba Wa Uzao wa Kanisa Halisi la Mungu Baba, kuhusu yatakayokuwemo katika Kitabu hicho...

(CCM Blog tunakuomba uinasome huku ukizingatia kuwa ni maandiko ya kiimani, na kama imani inayozungumziwa itakuwa haikuhusu wewe soma tu mwanzo hadi mwisho, hutapata hasara). Hiyo hapo.👇 




UFUNGUO       

Lango la 26 Eluli, Vol.1(6 Desemba,2020), Kanisa Halisi la MUNGU BABA litakuwa na Uzinduzi wa Ufahamu ulioanzia Tanzania Kwenda Mataifa yote katika Uwanja wa Taifa/ Uhuru kuanzia saa 8 mchana hadi saa 11 jioni. Viongozi wote kitaifa na kijamii, wamealikwa kushuhudia uzinduzi wa ufahamu huo. Aidha, viongozi wote wa dini na madhehebu pamoja na huduma binafsi wamealikwa kushuhudia uzinduzi huo. Sababu ya kualika kila mtu ni kwa kuwa sio suala la kidini au dhehebu, bali ni suala la Maendeleo ya Kitaifa na Mataifa.

 

Ufahamu huu ulioanzia Tanzania kwenda Mataifa yote, unathibitishwa na Mafundisho yanayoanzia Mwaka 2017, ya Kanisa Halisi la MUNGU BABA, ambayo hupatikana Ng’ambo ya Mto Usiovukika (Ezekieli 47:5 na Ufunuo 22:18-19). Aidha, Mafundisho yanayohusu Shamba Jipya, lililoko Ng’ambo ya Korongo la 2 Wakorintho 4:6, mahali ambapo Waliotumwa wote hawakufika yanathibitisha. Pia, Mafundisho ya kuingia Mji wa Raha katika Isaya 14:3-7 na Ufunuo 21:10, ambapo hakuna aliyewahi kusema huo Mji wenye Mfumo Mpya wa maisha uko wapi hasa, yanathibitisha kwamba huu Ufahamu hautoki katika vyuo vya Theolojia, Falsafa na Saikolojia vilivyoanzia Mataifa ya Magharibi. Hivyo, tuna ujasiri wa kusema kuwa Ufahamu huu umeanzia Tanzania kwenda mataifa mengine yote.

 

Katika Mwanzo 15:16 Ibrahimu alipewa kuwa Baba wa Mataifa yote kwa vizazi vinne. Vizazi vya Ibrahimu viliongozwa na Musa (Kutoka 3:10); Eliya Mtishbi (1Wafalme 17:1); Yesu Kristo (Matendo 10:38); na Eliya Adamu wa Pili kutoka Tanzania (Isaya 41:2,4 na 1Wakorintho 15:44-59).

 

Majira ya Vizazi hivyo Vinne vya Ibrahimu ilifika ukomo wake Mwaka 2017, kwa kutumia kanuni ninayofafanua katika sentensi inayofuata. Ukichukua Miaka 3½ ya Musa (kuanzia pale alipopokea Torati hadi alipopiga Mwamba mara mbili), ukajumlisha Miaka 3½ ya Mtishibi, ukajumlisha Miaka 3½ ya Yesu na ukajumlisha Miaka 3½ ya Adamu wa Pili kutoka Tanzania unapata Miaka 14. Miaka hiyo 14 ukijumlisha na Mwaka 2003 Adamu wa Pili alipoonekana Nchini Tanzania katika Mji wa Kigoma, unafika Mwaka 2017.   Huo ndiyo Mwaka Nafsi ya Kwanza (Baba) kati ya zile Tatu za MUNGU (1Yohana 5:8), ilipokuja juu ya Nchi.

Hivyo, Ufahamu tunaosema umeanzia Tanzania kwenda Mataifa mengine, ni ule wa kuanzia 2017 baada ya ukomo wa Madhabahu ya Mwana. Huu ni Ufahamu aliokuja nao Nafsi ya Kwanza (Baba) kutuvusha Mto Usiovukika, kutuingiza Shamba Jipya na Mji wa Raha. Baadhi ya mambo yaliyoanzia Tanzania ndipo yakaenda kwingineko:

 

Ufahamu Kuhusu Hija ya Chanzo Halisi Umeanzia Tanzania

Katika Matendo 8:27-39, tunashuhudia jinsi watu Mashuhuri na wasio Mashuhuri, walivyokuwa wakienda Yerusalemu, Madina na Meka kuhiji au kuabudu. Wengine walienda kwa Magari, kwa Ndege na Meli pia.

 

Tulichokuwa tunafuata kule Yerusalemu, Madina na Meka ni Sauti iliyosikika kule. Sasa Sauti ya Moyo iko Tanzania. Watu wote Kaskazini, Kusini, Mashariki na Magharibi mwa Uumbaji wote wajue kuwa Hija ya Chanzo Halisi iko Tanzania, Mjini Kigoma. Hija haiko Mashariki ya Kati tena. Kama walivyokuwa wanaendesha Magari, Ndege na Meli kwenda Mashariki ya Kati, sasa waje Tanzania.



Majira na Nyakati Sahihi za MUNGU BABA Zimeanzia Tanzania

Katika Isaya 33:6, tunasoma kuwa ilikusudiwa tangu Chanzo kuwepo na Majira Imara, Majira ya Wokovu tele, Majira ya Kumcha MUNGU BABA, na ya Raha tele. Ukitoa zile alama mbili, unapata 336; ikiwa na maana ya Miezi 12 x siku 28=336 kwa Mwaka.  Dunia iliamua kuzidisha Mwezi na kuongeza Siku 3, Mwezi ukawa na Siku 29, 30 na 31.  Hivyo, badala ya Mwaka kuwa na Siku 336 wakasema Mwaka una Siku 365 ¼!

 

Hii ina maana kuwa Mwaka badala ya kuwa na Miezi 12, una Miezi 13.  Kuthibitisha hili, baadhi ya Mashirika Makubwa ya Ndani na Nje, wanalipa Wafanyakazi wao Mshahara wa Miezi 13, badala ya Miezi 12!  Zaidi ni kwamba mtu mwenye umri wa Miaka 12, kumbe ana Miaka 13. Mwenye Miaka 24, kumbe ana Miaka 26! Mwenye Miaka 36, kumbe ana Miaka 39. Mwenye Miaka 48, kumbe ana Miaka 54. Ambaye amefikisha Miaka 60, kumbe ana Umri wa Miaka 65, nakadhalika.


Hiyo Miaka ya ziada ilitengenezwa na dunia ili kuhifadhi ndani ya mtu: makunyanzi; magonjwa; shida; adha; matatizo; utumwa na kadhalika. Ufahamu huu umefahamika kupitia Majira ya Mkombozi Halisi aliyekuja Sayuni Halisi (Isaya 59:20) kwa walioacha maasi. Watu kutoka mataifa yote waje kupokea Ufahamu huo unaopatikana bure nchini Tanzania.


 Kilele cha Ibada ni BABA Siyo Mwana Imeanzia Tanzania

Katika Warumi 10:4, Kitabu kinasema kuwa Kilele cha Ibada ni Mwana. Ingawa Mwana mwenyewe alisema katika Yohana 14:28 kuwa BABA ni Mkuu kuliko Yeye. Aidha, katika Yohana 4:23, Mwana alisema saa ipo na inakuja ambapo Waabuduo Halisi, Watamwabudu MUNGU BABA, ambaye ndiye Aliyewaumba.  Katika Mataifa yote, Tanzania ndiyo walioanza kwenda kwa MUNGU BABA Moja kwa Moja bila kupitia kwa Mwana. Watu wa mataifa yote waje kupokea Ufahamu huo ulioanzia Tanzania.


 Ibada ni Uzalishaji Imeanzia Tanzania

Katika Mwanzo 1:28, wakati Adamu na mkewe walipokuwa bado wako Kitangani kwa MUNGU BABA (Isaya 49:16), kitu cha kwanza walichoambiwa ni kuzalisha. Aidha, wakati Adamu ameumbwa na anaonekana kwa macho (Mwanzo 2:7), kitu cha Kwanza alichoambiwa ni kulima na kutunza (kuzalisha). Kumbe hiyo ndiyo Ibada ambayo MUNGU BABA anaitaka.

 

Mitume na Manabii baada ya Kitabu cha Mwanzo kuisha, hawakutaka tena Ibada ni Uzalishaji. Waliiga kile alichokuwa anafanya Musa, alipokuwa anawavusha wana wa Israeli kutoka Misri kwenda Kaanani.  Kila mmoja alipenda Hema ya Kukutania, bila kujua kuwa ilimlazimu Musa kufanya hivyo kwa sababu ya mazingira ya Wana wa Israeli walipokuwa njiani kutoka Misri kwenda Kaanani. Kanisa Halisi la MUNGU BABA, tumerejea kule alikokuwa anataka MUNGU BABA, ikiwa na maana ya Ibada ni Uzalishaji.

 

Tunakuja Kanisani kushukuru na kutoa heshima kwa MUNGU BABA aliyetufanikisha kwenye Uzalishaji ambayo ndiyo Ibada.  Hatujengi Kanisa Ofisini kwa kuwa tukimhudumia vizuri mteja pale kazini, hiyo ndiyo Ibada. Watu wa mataifa yote waje kuchukua Ufahamu huu ulioanzia Tanzania.


 Bustani Mpya Imeanzia Tanzania

Wote tunafahamu Ezekieli 28:13-15 kwa Habari ya Bustani ya ADENI, au Bustani ya kerubi. Aidha, tunaifahamu zaidi Bustani ya EDENI katika Mwanzo 2:8-15, ambayo pia unaweza kusema ni Bustani ya Adamu. Pia, tunaifahamu Bustani ya Ibrahimu katika Mwanzo 13:10. Bustani zote hizi tatu, zilikuwa Magharibi, kupitia Lutu. Ndiyo maana kila Sera waliyokuwa wanatunga kule Magharibi ilikuwa inatekelezeka hata kama ni ngumu kiasi gani! Ni kwa sababu Bustani ya MUNGU BABA ilikuwa kwao kupitia Lutu.

 

Baada ya MUNGU BABA kuja juu ya Nchi, kupitia Tanzania, amekuja mkononi mwake akiwa na Bustani Mpya (2Petro 3:13). Wengi wanajiuliza “Kwa nini korona Tanzania haipo?” Hilo ni suala la Bustani Mpya. Korona huko kwingine haitoki kwa kuwa hawataki kukubali kuwa, Chanzo cha Baraka kwa sasa ni Tanzania. Maana huwezi kuwa Chanzo cha Baraka bila kuwa na Bustani ya Aliyeumba kila kitu.

 

Bustani ya MUNGU BABA inaletwa na Sauti yake. Sauti ya Moyo Halisi sasa hivi iko Tanzania, ndiyo maana Sera za Tanzania zinatekelezeka bila shida. Watu wa Mataifa yote sasa waipende Tanzania, mambo yao yataenda vizuri.

 

Shamba Jipya Limeanzia Tanzania

Katika Isaya 65:17-25, tunasoma kuwa MUNGU BABA alipanga kuumba Mbingu (Mfumo) Mpya na Nchi (Rasilimali) Mpya na kuwa mambo ya kwanza hayataingia Moyoni.


Katika Shamba Jipya, Simba (watu wakali) watakula majani kama Ng’ombe na Mwana Kondoo atalisha pamoja na Mwanasimba.  Haya yanafafanuliwa pia katika Isaya 11:7-9. Mistari niliyotangulia kuonyesha pale juu, inafafanua zaidi kuwa, sasa ukijenga utakaa wewe na ukilima utavuna wewe. Msomaji utakubaliana na mimi kuwa kuna Vijiji ulikuwa ukijenga nyumba ya bati hukai na ukifanya mambo mazuri ulikuwa huyafaidi wewe; bali wengine.

 

Wakati huu wa Shamba Jipya, yaani Maisha ng’ambo ya 1Wakorintho 4:6, uchawi umeisha. Unajimu pia na uganga haupo tena. Hiyo ndiyo maana ya Shamba Jipya. Maisha ni tofauti kabisa na majira saba zilizopita ambapo wengi walikuwa wanaogopa kufanya maendeleo kwa sababu ya uchawi. kumbuka.


Wote Waliotumwa waliuwawa na wachawi.  Kwa sababu hiyo, imebidi MUNGU BABA aje Mwenyewe kukaa ndani ya Moyo wa kila mmoja anayetenda kwa haki ili kufuta uovu huo (Isaya 57:15).

Hilo ndilo Shamba Jipya, tofauti na lile la zamani lililoua wote Waliotumwa (Mathayo 21:33-40). Mtu wa taifa lolote, Ukitaka Shamba Jipya, yaani Maisha Mapya kabisa, njoo ujifunze Tanzania.


Kanisa Halisi Limeanzia Tanzania, Katika Ufunuo 2 na 3, tunasoma Habari za Makanisa Saba ambayo yalishindwa kupenya kwa sababu ya kilichoandikwa katika Danieli 7:21 na Ufunuo 13:5-7 kuwa kila anayetenda kwa haki alishindwa majira zote.


Sasa Kanisa au jamii ya wanaotenda kwa haki halishindwi tena kwa kuwa limeingia katika Mji wa Raha. Hapo Katika Mji wa Raha limetunga Methali, baada ya waliokuwa wakitesa Atendaye kwa haki kukomeshwa (Isaya 14:4-5).  Siri kubwa ni kuwa na Uzao Halisi wa MUNGU BABA, badala ya Waumini (Isaya 61:9).

 

Tofauti iliyopo kati ya Waumini na Uzao Halisi ni Suala la Imani na Upendo. Katika 1Wakorinto 13:13, Kitabu kinasema kuwa kuna Imani, Tumaini na Upendo.  Katika hayo Matatu lililo Kuu ni Upendo.


Kanisa Halisi tumeenda zaidi ya Imani na Tumaini baada ya kuamua kuwa na Upendo tena Uliopitiliza. Imani na Tumaini vilitugawa mno.  Upendo hautugawi, bali unatuunganisha zaidi. Ndiyo maana tunahubiri mambo matatu peke yake:  Imani; Upendo Usiobagua; na           Uzalishaji.

 

Katika haya matatu, hatuwezi kupigana, badala yake tutapendana zaidi. Ukikuta kuna ambaye anachukia hayo matatu, basi ni mchawi.  Wote katika Mataifa mbalimbali waje wapokee ufahamu huo ulioanzia Tanzania.

 

Mbingu Mpya na Nchi Mpya Imeanzia Tanzania

Katika Isaya 66:22, tunasoma kuwa, MUNGU BABA alikusudia kuumba Mbingu Mpya na Nchi Mpya ambayo itakaa mbele zake daima huku Uzao wake nao ukiwa mbele zake daima. Katika Isaya 65:17 anasema mambo ya kwanza hayataingia katika Mbingu Mpya na Nchi Mpya.  Mambo hayo ya Kwanza ni yapi?



Maelewano ya Isaka na Ishmaeli yameanzia Tanzania


Katika Mwanzo 25:8-10, tunasoma kuwa Isaka na Ishmaeli walipomaliza kumzika Baba yao hawakusalimiana tena hadi jana! Sababu kubwa ni tofauti ya Imani ya Mama wa Isaka na Mama wa Ishmaeli.  Ibrahimu alimpenda MUNGU BABA, alipoondoka, Imani na Tumaini upande wa Sara na Hajiri vikachukua nafasi watoto wao wakatofautiana. 

 

Mafundisho mabaya pia yalianza kuwa Ishmaeli amechukua nafasi ya Isaka, wakati aliyewaibia wote wawili ni Lutu katika Mwanzo 13:10. Hayo ndiyo mambo ya kwanza ambayo hayaingii katika Mbingu Mpya na Nchi Mpya. Katika Mbingu Mpya na Nchi Mpya Isaka na Ishmaeli wanaabudu pamoja kama tunavyosoma katika Isaya 19:23-25.


 Kuelewana kwa Kaskazini na Kusini kumeanzia  Tanzania.


Kulikuwepo na maajabu (phenomenon) ambayo yalikuwa hayana majibu kwa kuangalia mwenendo wa kiuchumi katika maeneo yote ya Kaskazini na Kusini, kila Taifa na kila Bara. Kila Taifa na kila Bara Kaskazini ni matajiri na Kusini ni masikini.  Siri kubwa ilikuwa katika Isaya 14:13, baada ya nyoka kuamua kwenda upande wa Kaskazini, na kuhifadhi kule utajiri ambao anatamba nao katika Luka 4:5-9, aliomwibia Adamu.


Ufunuo 12:1 naye aliamua kwenda maeneo ya Kusini, wakapatana na kuweka Mkataba na nyoka.


Ukisoma Ufunuo 12 yote, utadhani hawaelewani, kumbe wako pamoja! Majira hii, baada ya MUNGU BABA kuja juu ya Nchi, amevunja kabisa hayo mapatano ya Ufunuo 12:1 na nyoka.  Hakuna shida tena kati ya kaskazini na Kusini chini ya Ikweta, kama ilivyokuwa kabla ya MUNGU BABA kuja. Wote katika mataifa mbalimbali waje kupokea ufahamu huu.

 

Mlima wa Utawala wa Amani Umeanzia Tanzania

Katika Isaya 2:4, tunasoma kuwa kuna majira ambayo watu watatengeneza silaha zigeuke pembejeo za kwenda Shambani kulima.  Hii ni kweli kwa kuwa jambo hili limethibitika Tanzania baada ya waliokuwa wanachochea fujo kujikuta haiwezekani. Moyo Halisi ndio unaotawala kila mahali sasa.  Rais Dkt Magufuli anaishi Moyo. Hili ni kubwa kuliko yote katika maajabu ya Rais wa Tanzania. Yeyote anayeishi Moyo ukimchokoza hachokozeki, utashindwa wewe.  Mlima wa Utawala wa Amani, umeanzia Tanzania na umeenda kila mahali. Wote waje kujifunza.

 

HITIMISHO

Watanzania sasa, wajue kuwa wao ni Chanzo cha Baraka, maana Ufalme wa MUNGU BABA umehamia kwao (Mathayo 21:43). Dunia inajua Tanzania ni Taifa la aina gani. Wahusika ndio walikuwa hawajijui.  Ni Majira ya kujitambua kuwa Tanzania ni Chanzo cha Baraka.  Ndiyo maana MUNGU BABA hakuruhusu korona asumbue Tanzania kwa kuwa ni Taifa lake. Maendeleo tunayoyaona Magharibi, yalitokana na Sauti. Magharibi walikuwa wanalazimika kutetea Taifa Mwana ili wawe sehemu ya Sauti iliyosikika kule. Sasa Sauti iko Tanzania.


UFAHAMU:  Kwa Nini Sijaanza na Ufahamu wa Kuanzia 2003 Hadi 2016?

 Kuanzia 2003 hadi 2016, watendao kwa haki walifika Ufunuo 11:1-3 na Ufunuo 12:6 peke yake.  Hapo, kitabu kinasema tulikuwa tunaruhusiwa kupima Behewa la Ndani tu. Behewa la Nje walikuwa wamepewa Mataifa. Wakati huo hatukuwa tunaruhusiwa kuhubiri Mikutano ya Nje, maana, walikuwa wamepewa Mataifa, ikiwa na maana ya Ufahamu ulioanzia Magharibi ndio uliokuwa unakubalika. Hakuna ambaye kule Nje ungemwambia kipindi kile kwamba kuna Ufahamu ulioanzia Tanzania akakuelewa, angeona umechanganyikiwa.


Katika Ufunuo 13, kuna Mnyama ambaye katika majira zote alishinda Wanaotenda kwa haki. Hivyo, tulikuwa hatujaruhusiwa kutoka Nje kusema chochote. Katika Ufunuo 14, Kitabu kinasema ilikuwa bado ni wakati wa Mashariki ya Kati, hasa Israeli. Kwa hivyo, ruhusa ya kutoka Nje ilikuwa bado.

 

Katika Ufunuo 16, kuna Vita ya Hermagedoni. Hivyo, kama tungetoka Nje, Kitabu kinasema hasira, chuki na wivu vingesababisha Vita hiyo.


Katika Ufunuo 17 na 18 kuna, kahaba mkuu na mama wa makahaba ambaye hakubali Viongozi wa Kijamii kupokea Mafundisho ya Moyo Halisi.  Hiyo ina maana kama tungetoka nje kungetokea adha na dhiki kuu.


Katika Ufunuo 19, kuna neno asiyevaa mwili, ikiwa na maana kuwa bado Sauti ilikuwa haijapata kibali. Kibali kilikuwa kiko mikononi mwa anayesema Neno lililoko chini ya wanajimu.

Katika Ufunuo 21, napo tunakutana na uongo ukiwa na nguvu kubwa. Hivyo, kama tungetoka Nje tungesingiziwa na kuzushiwa makubwa. Ndiyo maana Mwaka 2017 ilibidi Nafsi ya Baba ije juu ya Nchi ili kutuvusha Ufunuo 22:18-19, ambayo ndiyo mistari inayoonyesha Mto Usiovukika.


Hivyo, Ufahamu ninaosema umeanzia Tanzania kwenda Mataifa mengine ni wa MUNGU BABA, siyo wa Mwana (Yohana 4:23). Kwa kuwa MUNGU BABA alikuwepo kabla ya Behewa la Nje, anauwezo wa kulipima Behewa la Nje bila madhara. Ndiyo maana Mataifa yote wanakaribishwa kuupokea Ufahamu huu ili wapone.


6 comments:

MAONI (COMMENTS)👇

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages