LATEST HEADLINES👉

Your Ad Spot

Oct 18, 2020

DKT KALEMANI AAGIZA UMEME USIKATWE KIPINDI CHA UCHAGUZI

 


Waziri wa Nishati,Dkt Medard Kalemani akizungumza na waandishi wa Habari mara baada kumaliza kufanya ukaguzi wa kituo cha kupooza umeme kilichopo  Dege, Wilaya ya Kigamboni, jijini Dar es Salaamu.

……………………………………………………………………………………

Hafsa Omar-Dar es Saalam

Waziri wa Nishati,Dkt Medard Kalemani ameliagiza Shirika la Umeme Tanzania(TANESCO) na wakandarasi wote nchini kusimamia ipasavyo upatikanaji wa umeme wa uhakika katika kipindi chote cha Uchaguzi.

Alitoa agizo hilo, Oktoba 17,2020 wakati akizungumza na waandishi wa habari,mara baada ya kumaliza kufanya ukaguzi wa ujenzi wa kituo cha kupooza umeme kilichopo Dege,Wilaya ya Kigamboni,Jijini Dar es Salaam.

Amesema, Serikali inataka wananchi wafanye uchaguzi wao bila ya kujitokeza kwa  changamoto yoyote inayotokana na umeme, na kuwataka mameneja wote wa Tanesco kulisimamia agizo hilo ili isitokee changamoto yoyote inayohusiana na  umeme katika kipindi cha uchaguzi.

“ Nitoe rai kwa mameneja wote wa Tanesco umeme usikatike wakati wa uchaguzi, usikatike kwa maeneo yoyote na muda wowote lakini hasa wakati wa uchanguzi na hasa tarehe 28 wakati wa kupiga kura tunataka wananchi wapige kura bila ya kero yoyote ya umeme”alisema.

Pia, ameitaka Tanesco kuhakikisha kuwa  umeme wa uhakika unapatikana muda wote nchini ili wananchi watumie huduma hiyo katika kujiletea maendeleo mbalimbali katika maeneo yao.

Hata hivyo, amesema matumizi ya nguzo za zege zitasaidia na kupunguza kero ya kukatika kwa umeme nchini kwakuwa nguzo hizo zinauwezo wa kukaa muda mrefu bila ya kuharibika.

“ili wananchi waendelee kuwa na uhakika wa umeme lazima tutumie nguzo za zege, kwasababu maeneo mengine Dar es Salaam umeme unakatika kwasababu wataalamu wetu wanafanya marekebisho mara kwa mara yakiwemo ya kuondoa na kubadilisha nguzo zilizoharibika kwahiyo tukishaweka nguzo za zege tatizo hili litamalizika”alisema Dkt Kalemani.

Aidha, ameeleza kuwa tayari nguzo za zege zimeanza kusimikwa katika maeneo mbalimbali nchini, nguzo ambazo ni imara na zinadumu kwa miaka mingi zaidi bila ya kuharibika na ambazo zitaleta mageuzi makubwa ya upatikanaji wa umeme wa uhakika nchini.

Amesema,maeneo ambayo yamepewa kipaumbele kwa kuanza kutumika kwa nguzo hizo ni Pamoja na sehemu ambazo kuna majaruba au maeneo ambayo kuna majimaji ambapo nguzo zinaharibika kwa haraka

Pia, amewapongeza wakandarasi wote aliopewa kazi ya kutengeneza nguzo hizo, kwa kukamilisha kazi zao kwa haraka na kuwataka kutengeneza nguzo zenye ubora wa hali ya juu.

Katika ziara hiyo, Waziri wa Nishati aliambatana na Kamishna Msaidizi wa Umeme Mhandisi. Innocent Luoga, Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Umeme Tanzania(TANESCO) Dkt Tito Mwinuka,Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Wakala wa Nishati Vijiji(REA) Amos Maganga na waatalamu mbalimbali kutoka  Tanesco.

No comments:

Post a Comment

MAONI (COMMENTS)👇

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages