LATEST HEADLINES👉

Your Ad Spot

Aug 3, 2020

MKAPA 'UMELIPIZA KISASI' ALICHOKUFANYIA NYERERE? !!!

Rais wa Awamu ya Tatu, Benjamin William Mkapa *wakati wa uhai wake( akisalimiana na mwandishi wa makala haya, Richard Mwaikenda, wakati wa hafla ya kuwaapisha mawaziri na Waziri Mkuu, Frederick Sumaye wa mara ya pili kwenye viwanja vya Ikulu ya Chamwino, Dodoma 2000.





NADIRIKI kusema kwaheri  Mzee wa Uwazi na Ukweli, Benjamini William Mkapa umeondoka Tanzania bila kutuaga, tutakukumbuka daima hasa kwa mambo makubwa  ulioyoifanyia nchi yetu kabla ya kuwa rais, ukiwa rais na baada ya kustaafu urais.


Pia, nasikitika umeondoka duniani bila kutuaga watanzania na hasa viongozi wenzako wastaafu akina Jakaya Kikwete, Ali Hassan Mwinyi na  waliopo madarakani , Rais John Magufuli, Makamu wa Rais, Samia Suluhu Hassan, Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa pamoja na familia yako.


Kabla ya kuondoka duniani, Mzee wa Uwazi na Ukweli ulitupa matumaini ulipohudhuria Mkutano Mkuu wa 10 wa Chama Cha Mapinduzi (CCM),                    Julai 11,2020, kwenye Ukumbi wa Jakaya Kikwete jijini Dodoma, ambapo hakuna aliyewaza kuwa utaaga dunia siku 12 baadaye.


Siku hiyo nikiwa miongoni mwa wanahabari walioteuliwa kuingia ndani ya ukumbi wa Kikwete, kuripoti habari za mkutano huo wa ngazi ya juu wa CCM kitaifa, nilifurahi kukuona wewe na viongozi wastaafu wenzio pale meza kuu, Jakaya Kikwete na Ali Hassan Mwinyi mkiwa na nyuso za bashasha huku mkiangua vicheko baada ya kuchekeshwa na vionjo vya hotuba ya Rais Magufuli.


Kweli nilifarijika sana kuwaona, huku nikiwaza kwamba laiti angekuwepo Rais wa Awamu ya Kwanza, Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, safu ya marais wanne wastaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ingekamilika, lakini yote tunamwachia Mwenyezi Mungu kwani ndiye anayeamua nani atangulie na nani wa kufuata.


Kwa hali niliyoiona ilidhihirisha wazi kwamba mna ushirikiano, umoja, mashikamano na upendo, pia mmebeba dhamana kubwa ya kuhakikisha Taifa linaendelea kuwa la amani na utulivu kwa kupokezana madaraka kwa amani ili nchi yetu iendelee kuongozwa na viongozi mahiri, wazalendo kama ilivyo kwa kiongozi wetu wa sasa Rais John Magufuli.

Benjamin Mkapa (wa pili kulia) akiwa meza kuu na wastaafu wenzie, Ali Hassan Mwinyi (kulia) na Jakaya Kikwete  wakati Rais John Magufuli akihutubia  mara baada ya kuchaguliwa kuwa mgombea urais wa chama hicho katikaMkutano Mkuu wa 10 wa CCM, kwenye Ukumbi wa CCM wa Jakaya Kikwete, jijini Dodoma Julai 11,2020. PICHA NA RICHARD MWAIKENDA


Mkapa tutazimisi picha za pamoja tulizozizoea kuziona mkipiga na pacha wastaafu wenzako, Kikwete na Mwinyi pamoja na Rais Magufuli huku mkiwa mmeshikana mikono huku mkiwa na tabasamu usoni, kama mlivyopiga katika matukio ya hivi karibuni, Mliposhiriki ujenzi wa Ikulu ya Chamwino, wakati wa kuvunjwa Bunge la Jamhuri ya Muungano na mlipokaa kwa mara ya mwisho meza kuu mlipohudhuria Mkutano Mkuu wa CCM jijini Dodoma, Julai 11, mwaka huu.



Picha hizo zilikuwa zinatupa faraja kubwa sana watanzania, lakini pia picha  hizo zilizokuwa zinasambaa kwa kasi duniani kupitia mitandao mbalimbali ya kijamii, kilikuwa ni kisu kwa wasioitakia mema nchi yetu kwa umoja na mshikamano tuliokuwa nao. 

Baadhi  ya wananchi wa mataifa mengine kitendo hicho kilikuwa kinawafanya waitamani na kuionea wivu Tanzania, kwani katika nchi zao hakuna tunu kama hiyo.


Samahani kama nitakosea, lakini mimi sijawahi ona picha kama hizo katika nchi zinazotuzunguka kama vile; Kenya, Uganda, Rwanda, Burundi, Sudani kusini, DRC Congo, Congo Brazaville, Msumbiji, Zambia, Malawi, Zimbabwe, Madagascar, Comoro, Angola na hata Afrika Kusini. Hiyo inadhihirisha jinsi Nchi Yetu ilivyobarikiwa.


Lakini wakati tungali tunahitaji baraka zako, Mzee wa Uwazi na Ukweli,  umeondoka na kutuachia  pengo lingine, ukiwaacha bila kuwaaga mapacha zako wastaafu, Jakaya Kikwete na Ali Hassan Mwinyi ili jahazi waliongoze wenyewe. Je, ulikumbuka kuwaachia usia wowote? 


Mkapa, au ndiyo ulifanya ujanja wa kuacha wosia kwa watanzania wote na walimwengu kupitia kitabu chako ambacho kimesheheni mambo mengi muhimu kwa Taifa letu, Afrika  na Dunia kwa ujumla? Sasa kitabu hicho itabidi tukitafute kwa udi na uvumba tuusome wosia uliotuachia.


Nadiriki pia kusema kuwa kwa mtindo ulioondokea Mzee wa Uwazi na Ukweli, Mkapa ni sawa na kwamba 'umewapiga chenga ya mwili' na kuwaacha hoi  wasiamini kilichotokea, wastaafu wenzako, Mzee wa Nguvu Mpya, Ari Mpya na Kasi Mpya, Jakaya Kikwete na Mzee wa ruksa, Ali Hassan Mwinyi  lakini pia Rais aliye madarakani, Mzee wa Hapa Kazi Tu, John Magufuli.


Naamini siku hiyo ya mkutano kama ilivyokuwa kwangu, wengi walifarijika kuwaona lakini vile vile baadhi yetu pamoja na watanzania wengine waliokuwa wanaangalia tukio hilo kwenye luninga, ilikuwa ni siku ya mwisho kukuona ukiwa hai hadi Julai 24, aliposikika Mkuu wa Nchi, Rais Magufuli akiutangazia Umma kwamba hatuko na wewe tena.


Mkapa, mbona kama 'unalipiza kisasi' ulichofanyiwa na Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere ambaye alifariki 1999, mwaka mmoja kabla ya kushuhudia kuapishwa kwako mwaka 2000 kushika kipindi cha pili cha uongozi wako?


Kama siyo hivyo, kwa nini basi hukusubiri John Magufuli aapishwe mwaka huu, bali umeamua kuondoka miezi michache kabla ya tukio hilo muhimu? au lengo lako lilikuwa ni kushuhudia tu jina lake lipitishwe katika mkutano mkuu wa CCM?


Sasa unapoondoka, bila kuaga, Je, jukumu la kuendelea kuilea Tanzania yenye amani na utulivu kwa nini umelikimbia na kuwaachia Mwinyi, Kikwete na Magufuli? Nadiriki kusema umeamua 'kulipiza kisasi' alichokufanyia Baba wa Taifa.


Mkapa umewaachia machungu marais wastaafu wenzako na hasa Magufuli aliye  madarakani ambaye umemlea kisiasa na kiuongozi kiasi cha kumuita askari wa mwamvuli namba moja katika Baraza lako la Mawaziri.

Rais Mkapa enzi za uhai wake  akimnadi, John Magufuli alipogombea kwa mara ya kwanza ubunge mwaka 1995 wakati wa kampeni za urais ambapo yeye aligombea kwa mara kwanza kupitia CCM.

Kwa kukumbuka mambo mengi uliyomfanyia, ndiyo maana Rais Magufuli alishindwa kujizuia na kuanza kububujikwa na machozi mbele ya kadamnasi ya waombolezaji wa kitaifa na kimataifa pamoja na wananchi alipokuwa akitoa neno la kukuaga katika shughuli za kutoa heshima za mwisho kwenye Uwanja wa Uhuru, Dar es Salaam Julai 28, 2020. 


Magufuli alikuwa bado anahitaji msaada wako wa ushauri  wa kila hali wa kibinafsi na kiuongozi, lakini sasa mzigo huo umeamua kuwaachia pacha wastaafu wenzako, Kikwete na Mwinyi, na kwa hali ilivyo kutokana na uzee alionao Mzee wa Ruksa, Mwinyi.

Lakini, pasi na shaka jukumu hilo kubwa umemuachia Kikwete ambaye bado anaonekana ana nguvu za kuweza kukimbia huku na kule kumsaidia Rais Magufuli kuishauri na kumwakilisha kuongeza hadhi na heshima ya Tanzania katika baadhi ya matukio makubwa duniani kama ilivyotokea hivi karibuni katika shughuli ya kuapishwa Rais mpya wa Burundi na mazishi ya Rais wa zamani wa Burundi, Pierre Nkurunziza ambapo waliambatana na Makamu wa Rais, Samia Suluhu Hassan.
Rais Mstaafu wa Awamu ya Nne Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete na  Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan   wakimjulia hali na kumfariji Mjane wa marehemu Rais  Pierre Nkurunziza wa Burundi Bibi Rev Denise Nkurunziza wakati alipofika nyumbani kwa marehemu Nkurunziza  Jijini Bujumbura Nchini Burundi 


Mkapa, nakumbuka Desemba 21, 2005, katika uwanja huo wa Uhuru (zamani Uwanja wa Taifa ama shamba la bibi) ambao Julai 28, 2020, tumeutumia kukuaga, ulimkumbatia kwa furaha Jakaya Kikwete mara tu baada ya kumaliza awamu yako na kumkabidhi madaraka ya kuongoza nchi.


Nakumbuka siku hiyo nikiwa mmoja wa wapiga picha za habari walioshiriki kuripoti tukio hilo, nilishuhudia ukinusurika kuanguka kwa kukosea kukanyaga  ngazi ulipokuwa ukiondoka kwa furaha iliyopitiliza katika jukwaa maalumu la kuapishia. Kitendo hicho kiliambatana na furaha ya kuutua kwa usalama mzigo mkubwa wa kuiongoza nchi na vilevile hukuamini kama kweli umestaafu na kumuachia jahazi hilo Jakaya Mrisho Kikwete.


Pia, tukio hilo limenikumbusha wakati wa hafla ya uzinduzi wa kitabu chenye mkusanyiko wa hotuba zako kilichochapishwa na Kampuni ya Mkuki. ambapo ulimuuliza mchapishaji kuwa Dar es Salaam kuna bookshop ngapi? Mimi nilikuuliza kwa nini unauliza swali kama hilo? Ukajibu;  "Nikiondokana na rokapu (Ikulu) hii nataka niwe najisomea vitabu." Ukaulizwa tena, kwanini Ikulu unaiita rokapu? Ukajibu kwa kuhamaki; "Hapa Ikulu si pazuri kabisa, huna uhuru." Ukaondoka huku ukicheka na kutuacha tukitafakari juu ya hilo.

Pia,nakumbuka ukiwahutubia wananchi kwa mara ya kwanza katika ziara yako ya kwanza ulipopata madaraka ya kuiongoza nchi,kutoka kwa Rais wa Awamu ya Pili, Ali Hassan Mwinyi, Kigamboni Dar es Salaam, uliwaambia "Ndugu wananchi mkae mkijua matatizo yenu ndiyo mwanzo wa maendeleo yenu. Kauli hiyo iliwatatiza wananchi hao wa kawaida, wakabaki wanaulizana, hivi Rais amekuja kutudhihaki, yaani matatizo yetu ndiyo maendeleo, wapi na wapi?!!!

Baada ya kuona hawajakuelewa, ukairudia kauli hiyo na kuwaambia kuwa "wananchi huo ndiyo ukweli, bila kuwa na matatizo hamuwezi kupiga hatua za kimaendeleo. Unapotatua tatizo lako linalokukera kwa muda mrefu basi unakuwa umepiga hatua fulani ya maendeleo yako". ulifafana kidogo, lichaya kwamba baadhi yao walikuwa bado hawajakuelewa.


Ukifika huko tunaomba uwape salamu zetu baadhi ya viongozi wetu waliotangulia mbele ya haki; Baba wa Taifa, Julius Kambarage Nyerere, Rais wa zamani wa Zanzibar, Abeid Aman Karume, Makamu wa Rais, Dk. Omary Ali Juma, Waziri Mkuu wa zamani, Rashid Mfaume Kawawa, Spika wa zamani, Adam Sapi Mkwawa, Spika wa zamani, Samwel Sitta na Rais wa zamani wa Zanzibar, Aboud Jumbe. 


Mkapa, tutasema mengi, tutauliza maswali mengi na kuhoji mengi, lakini hatutaweza kupata majibu ya moja kwa moja kutoka kwako, kwani Mungu tayari keshachukua roho yako, amekupenda zaidi yetu na ndiyo aliyetuleta duniani na ana mamlaka ya kutuchukua, lakini tutaendelea kukuenzi kwa mema na mambo mengi uliyoitendea Tanzania. 


Lakini baadhi ya majibu tutaendelea kuyapata kupitia kwenye kitabu chako cha Maisha Yangu, Kusudio Langu pamoja na hotuba zako zilizojaa maneno yenye hekima, busara na yenye mafunzo mengi. Pia kizazi na kizazi kitaendelea kuifaidi mifumo mbalimbali ya kiuchumi uliyoianzisha wakati wa utawala wako, ambayo nimeitaja kwa uchache hapo chini katika makala hii. Kweli ulikuwa hazina na utaendelea kuwa hazina yetu.


Ulikuwa ni mmoja wa wanasiasa "senior" tuliokuwa tumebaki nao Tanzania na Afrika kwa ujumla uliyekuwa na kofia ya uongozi na kofia ya uanazuoni "intellectual" kwa wakati mmoja. Sio kwa sababu ya kupita Chuo kikuu. Ni kwa sababu hukuwa "mvivu wa kufikiri". Unaweza ukasoma sana na bado usiwe msomi "intellectual".  


Mkapa, alikuwa na uwezo wa kuona mzizi, mti , matawi na matunda yake kwa wakati mmoja. Ukisikiliza "maoni" yake wakiwa Afrika ya Kusini pamoja na Rais Thabo Mbeki, Paul Kagame, Olusegun  Obasanjo na wengineo anasema "Tatizo la Afrika tunaangalia matunda tunaacha mzizi, mti na matawi yake. Kwa kweli ujumbe huu unafikirisha.


“Tunalalamikia viongozi wanatuangusha wakati "hao viongozi"  wanatokana na aina ya jamii tuliyonayo. Mfano kama jamii imejaa ubinafsi, usitegemee "mjumbe" asiwe mbinafsi. Kwani mjumbe ni nani? ametoka wapi? anamwakilisha nani? wengine wako wapi? kwanini sio wajumbe? nani amewazuia?” Ni baadhi ya maneno yake mkapa yatakayondelea kuishi licha ya yeye kupumzishwa katika nyumba yake ya milele, kijijini kwake Lupaso, Masasi.


Baadhi mifumo ya uimarishaji uchumi aliyoianzisha Mkapa (Mr. Clean) wakati wa utawala wake;

Ilianzishwa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) kuimarisha ukusanyaji wa mapato Julai 1996.

Ukaanzishwa mfumo wa VAT Julai 1998

Public Service and Act pamoja na Public Procurement Regulatory

Authority vilianzishwa 2001

• Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora

Julai 2001

Taasisi ya Kuzuia Rushwa (Prevention of Corruption Bureau)

Regulatory Agencies nyingine zilianzishwa nyingi ikiwa ni pamoja na

Brela, EWURA, TCCRA, SUMATRA, Viwanja vya ndege,Maji safi

na taka, TANROADS,na Baraza la Taifa la Biashara (National Business Council)



Ili kuyapata hayo ikaanzishwa

Vision 2025

MKUKUTA

MKURABITA

Mini Tiger Plan 2020

• Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF).

Bima ya Taifa

Mageuzi katika Elimu, DEDP na SEDP

Mradi wa maji ziwa Victoria,

Mungu ailaze roho yako mahali pema peponi. Amen.



Ndimi, Richard Mwaikenda

Mpigapicha/Mwandishi

0754264203

No comments:

Post a Comment

ANDIKA MAONI (COMMENTS) HAPO👇

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages